Radio Fortune Africa -Ukweli na Burudani
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

Na: Cantona Joseph|RFA

Shirika la Reli Tanzania (TRC) limetoa taarifa kuhusu ajali ya treni ya umeme , EMU iliyokua ikisafiri kutoka Dar es Salaam kwenda Dodoma majira ya saa 2:00 asubuhi Oktoba 23, 2025 katika kituo cha Ruvu.
Shirika limesema kuwa ajali hiyo imetokana na hitilafu za kiuendeshaji na kwa taarifa za awali hakuna tukio la kifo.Taarifa ya leo Oktoba 23, 2025 iliyotolewa na TRC imebainisha kuwa Timu ya wataalamu inaendelea na uchunguzi wa kina na juhudi za kuhakikisha kwamba huduma zinarejea haraka.
Gavana aliyetoa matamshi yenye utata kuhusu kifo cha Raila ajipata mashakani Kenya

Tume ya Kitaifa ya Uwiani na Maridhiano nchini Kenyac(NCIC) imemtaka Gavana wa Nyeri, Mutahi Kahiga, kutoa maelezo rasmi kuhusu kauli zake zilizozua utata kuhusu kifo cha aliyekuwa kinara wa ODM Raila Odinga.
Kauli hizo zimezua hasira kubwa nchini Kenya, hasa baada ya Kahiga kusema kuwa kifo cha Odinga ni “mpango wa Mungu” ili kanda ya Mlima Kenya ipate faida kutoka kwa rasilimali za serikali ambazo zilikuwa zikitumika sehemu nyingine.
Kahiga alidai kuwa makubaliano ya kisiasa kati ya Rais William Ruto na marehemu Odinga yalibadilisha vipaumbele vya maendeleo ya serikali kuelekezwa zaidi katika kanda ya Nyanza, hali inayodaiwa kumfanya mkoa wa Mlima Kenya kupoteza fursa za kimaendeleo.
Tume ya NCIC imesema kuwa kauli hizo ziliharibu kwa kiasi kikubwa juhudi zilizofanywa kudumisha amani na mshikamano wa kitaifa, na kwamba Gavana Kahiga anapaswa kuwajibishwa kwa kuwa ni mtu anayeongoza katika nafasi ya umma.
Katika taarifa yao ya Jumatano, Tume ilionya kuwa kauli kama hizo si tu zinahuzunisha kumbukumbu za shujaa wa taifa, bali pia zinaweza kuchochea migogoro ya kikabila na mivutano ya kijamii wakati taifa linapolia kiongozi wake wa zamani.
Aidha, NCIC ilisifu Baraza la Magavana kwa kujitenga wazi na Gavana Kahiga na kumwondoa kutoka nafasi yake ya Makamu Mwenyekiti wa Baraza hilo.
Hatua hii imeonekana kama ishara chanya ya kuimarisha maadili ya umoja, heshima, na ujumuishwaji katika uongozi wa kitaifa.
Kauli hizi za Gavana Kahiga zilisababisha hasira kubwa katika umma, huku wengi wakimlaani kwa kuonyesha ukosefu wa hisia na taaluma katika kauli zake.
Hali hiyo ilisababisha Baraza la Magavana kuamua kwa kauli moja kumwondoa Kahiga kutoka nafasi ya Makamu Mwenyekiti baada ya yeye kutangaza kujiuzulu.
Baada ya shinikizo hilo, Kahiga aliomba radhi kwa familia ya Raila Odinga, chama cha Orange Democratic Movement (ODM), wenzake, na wananchi wa kanda ya Nyanza, akibainisha kuwa maneno yake yalikuwa ya kibinafsi na hayawakilishi maoni ya watu wa Nyeri wala Baraza la Magavana.
Pia, chama cha ODM, Waziri wa Kilimo Mutahi Kagwe, viongozi wa Kaunti ya Nyeri na viongozi wengine wa kisiasa wamekosoa vikali kauli hizo, wakitoa wito wa uvumilivu na mshikamano ili kuendeleza amani nchini.
Uchaguzi mkuu Tanzania 2025: Zanzibar yatangaza Jumatano kuwa siku ya mapumziko

Rais wa Zanzibar Dkt.Hussein Ali Mwinyi ametangaza Jumatano ya tarehe 29 Oktoba itakuwa ni siku ya mapumziko visiwani.
Tangazo hili amelitaja kuwa linawapa fursa wananchi kushiriki uchaguzi unaotarajiwa kufanyika siku hiyo.
“Uamuzi unalenga kuwapa wananchi wenye sifa ya kupiga kura fursa ya kutekeleza haki yao ya kidemokrasia,” ilisema taarifa yake.
Aidha,Rais Mwinyi amewasihi wananchi hasa wakazi wa Zanzibar kufuata miongozo na maelekezo iliyotolewa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, ZEC ili kudumisha utulivu wakati wa kupiga kura.
Hospitali ya Kenyatta yafanya upasuaji mkubwa zaidi kuondoa kilo 20.86 za tishu za matiti kwa msichana
Katika mafanikio makubwa ya kimatibabu, madaktari katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH) wamefanya upasuaji unaoaminika kuwa mkubwa zaidi kurekodiwa duniani wa gigantomastia, na kuondoa kilo 20.86 za tishu za matiti kutoka kwa msichana wa miaka 17.
Lydia Musivi alikuwa akiishi na aina kali ya gigantomastia, hali adimu ya ukuaji wa matiti kupita kiasi na mara nyingi kumdhoofisha.
Ingawa gigantomastia yenyewe ni nadra, kiasi kama hicho cha kuondolewa kwa tishu hakijasikika katika kesi yoyote iliyorekodiwa.
Upasuaji huo uliofanyika mapema mwezi huu, unasifiwa kama ushindi wa kiafya na wa kibinadamu.
Upasuaji huo mgumu sana uliongozwa na Dkt. Benjamin Wabwire, Mkuu wa Upasuaji Maalumu na Urekebishaji katika KNH.
Alisisitiza athari kubwa ya kibinadamu ya utaratibu huo. “Hii ilikuwa zaidi ya mafanikio ya upasuaji; ilikuwa ni kurejesha hadhi na mustakabali wa mwanamke mchanga,” Dk. Wabwire alisema.
Trump anasema mazungumzo ya Putin ‘hayaelekei popote’ huku akiweka vikwazo vipya

Marekani imetangaza vikwazo vipya vinavyolenga makampuni mawili makubwa zaidi ya mafuta nchini Urusi – Rosneft na Lukoil – katika juhudi za kuishinikiza Moscow kufanya mazungumzo ya makubaliano ya amani nchini Ukraine.
“Kila wakati ninapozungumza na Vladimir, ninakuwa na mazungumzo mazuri na kisha hawaendi popote,” Rais Donald Trump alisema, baada ya mkutano na Katibu Mkuu wa Nato Mark Rutte kujadili mazungumzo ya amani.
Tangazo la vikwazo hivyo limekuja siku moja baada ya Trump kusema kuwa mkutano uliopangwa kufanyika na Rais wa Urusi Vladimir Putin mjini Budapest utasitishwa kwa muda usiojulikana.
Mapema Jumatano, Urusi ilitekeleza mashambulizi makali ya mabomu dhidi ya Ukraine yaliyoua takriban watu saba wakiwemo watoto.
All Rights Reserved © The Cantona Group PLC||2025
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.