Msumbiji: Wafungwa 1,500 watoroka jela katikati ya ghasia za baada ya uchaguzi

Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph

https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

Nchini Msumbiji, serikali imethibitisha, jioni ya Desemba 25, kutoroka kwa wafungwa wengi kutoka gereza lenye ulinzi mkali karibu na Maputo. Zaidi ya wafungwa 1,500 walitoroka mchana, katika mazingira ambayo bado hayajafahamika. Kutoroka huku kunatokea wakati nchi imekuwa na vurugu mpya tangu Desemba 23 na baada ya Baraza la Katiba la uchaguzi kuthibitisha ushindi wa Daniel Chapo kama mkuu wa nchi kwa asilimia 65 ya kura.

Polisi wakiwa kazini katika mitaa ya Maputo, wakati maandamano ambayo yalisababisha kutoroka kwa wafungwa 1,500 kutoka gereza la Machava mnamo Desemba 25, yameendelea kwa wiki kadhaa. Hapa tarehe 7 Novemba 2024.
Polisi wakiwa kazini katika mitaa ya Maputo, wakati maandamano ambayo yalisababisha kutoroka kwa wafungwa 1,500 kutoka gereza la Machava mnamo Desemba 25, yameendelea kwa wiki kadhaa. Hapa tarehe 7 Novemba 2024. © Carlos Uqueio / AP

Akizungumza na waandishi wa habari, mkuu wa polisi wa Msumbiji, Bernardino Rafael, amethibitisha kutoroka kwa wafungwa 1,534 kutoka gereza kuu la Machava, lililoko takriban kilomita kumi na tano kutoka mji mkuu, Maputo. Video zilikuwa zikisambazwa tangu alasiri ya Desemba 25 zikionyesha umati wa watu ukikimbia kutoka nje ya jengo hilo, kisha kutawanyika katika mitaa iliyo jirani ambapo milio mingi ya risasi ilisikika, wengine wakichukua silaha za walinzi wakati wakitoroka.

Wafungwa 150 pekee ndio wamekamatwa tena wakati wa taarifa ya polisi kwa vyombo vya habari. Wakati huo huo wafungwa 33 waliuawa na 15 kujeruhiwa wakati wa makabiliano na wafanyakazi wa magereza na polisi, amesema Bernardino Rafael. Kulingana na mkuu huyo wa polisi wa Msumbiji, wafungwa hao walitumia fursa ya mkanganyiko, uliosababishwa na kuwepo kwa waandamanaji karibu na gereza hilo, kuangusha ukuta wa jengo hilo.

Wanajihadi miongoni mwa wafungwa waliotoroka

Gereza hili ni kituo cha ulinzi wa hali ya juu. Wafungwa wanaohusishwa na makundi ya wanajihadi wenye silaha wanaoendesha harakati zao katika jimbo la Cabo Delgado ni miongoni mwa waliotoroka. Takriban thelathini kati yao ni miongoni mwa waliotoroka, akiwemo mmoja anayechukuliwa kuwa “hatari sana,” amesema mkuu wa polisi, ambaye alionyesha wasiwasi wake.

Kulingana na shirika lisilo la kiserikali la Plataforma Decide, watu 248 walifariki katika muda wa siku 65 katika ghasia zilizotikisa nchi.

Kutokana na mgogoro Msumbiji, ANC yashtumiwa

Wakati Msumbiji inatumbukia katika mgogoro mkubwa wa baada ya uchaguzi, mtazamo wa Afrika Kusini, jirani na mamlaka ya kikanda, unazidi kukosolewa. Saa chache baada ya kupitishwa kwa matokeo ya mwisho na Mahakama ya Katiba ya Msumbiji, Jumatatu Desemba 23, katibu mkuu wa chama tawala nchini Afrika Kusini cha African National Congress (ANC), ametuma pongezi zake kwa “rafiki” Daniel Chapo kwa kuchaguliwa kwake.

Taarifa ambayo inatofautiana na majibu kutoka Washington, ikieleza wakati huo huo “wasiwasi” wake kuhusu “ukosefu wa uwazi” wa uchaguzi wa Msumbiji. Waangalizi wa ndani wanalaani kile walichokiita “aibu”, hata “kuwa na wasiwasi”, kwa serikali ya Afrika Kusini, inayotawaliwa na ANC, katika kukabiliana na hali ya mbaya inayotokea upande mwingine wa mpaka.

Vyama vya ukombozi, ambavyo bado viko madarakani katika eneo hilo, ANC Afrika Kusini, Zanu PF nchini Zimbabwe au MPLA nchini Angola, vinahofia upepo wa mabadiliko unaovuma nchini Msumbiji, ambao unaweza pia kufanya upinzani kuchukuwa madaraka katika nchi zao.

All Rights Reserved © Cantona Group PLC||2024


Discover more from cantonadigital

Subscribe to get the latest posts sent to your email.

Leave a comment