Afrika Leo Mchana-08,Oktoba 2024

Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph

https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

Karibu katika Matangazo yetu ya jioni moja kwa moja kutoka Communication Center. Tumekuandalia mengi ikiwa ni pamoja

Muhtasari

  • Rigathi Gachagua: Hoja ya kumuondoa madarakani Naibu wa Rais wa Kenya yaanza kujadiliwa bungeni
  • Israel inasema imeongeza operesheni ya ardhini kusini mwa Lebanon
  • Israel yasema ilimuua kamanda wa Hezbollah huko Beirut
  • Cissy Houston, mwimbaji nguli na mama wa Whitney Houston, afariki dunia
  • Waziri Mkuu wa zamani wa Lebanon asema nchi yake imetelekezwa na jumuiya ya kimataifa
  • ‘Jinsi Israeli inavyojilinda ni muhimu,’ asema Kamala Harris
  • Israel yaadhimisha mwaka mmoja tangu shambulio la Hamas huku mapigano yakiendelea

Naam,Natumai U buheri wa afya popote pale ulipo duniani kwa mwoyo mkunjufu na mikono miwili Hujambo na karibu katika matangazo yetu Afrika Leo Mchana ya moja kwa moja ikiwa ni tarehe 08/10/2024 Jina langu ni Cantona Joseph,karibu.

Rais wa Korea Kaskazini, Kim amuita Putin ‘rafiki wa karibu zaidi’

Kim (Kulia) na Putin (kushoto) walifurahia urafiki wao walipokutana Korea Kaskazini mwezi Juni

Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un ametuma ujumbe wa siku ya kuzaliwa kwa Rais wa Urusi Vladimir Putin, akimtaja kuwa “rafiki wake wa karibu zaidi”.

Kim akimpongeza Putin kwa kutimiza miaka 72, aliongeza kuwa uhusiano kati ya nchi hizo mbili utaimarishwa.

Uhusiano kati ya Pyongyang na Moscow umeongezeka tangu kuanza kwa vita vya Ukraine, katika hatua ambayo inaitia wasiwasi Magharibi.

Katika hatua nyingine siku ya Jumanne, Kim alisema Pyongyang itaharakisha hatua za kuifanya nchi yake kuwa nchi yenye nguvu kubwa ya kijeshi yenye silaha za nyuklia.

Kwa mujibu wa mtandao wa Yonhap News ukinukuu vyombo vya habari vya serikali ya Korea Kaskazini KCNA, Kim alisifu uhusiano kati ya nchi zote mbili, akisema umekuwa “usioshindwa na wa milele”, tangu ziara ya Putin huko Pyongyang mwezi Juni.

“Mikutano na uhusiano wa kindugu kati yetu… utatoa mchango chanya katika kuimarisha zaidi msingi wa milele wa urafiki wa DPRK na Urusi,” aliongeza, akimaanisha Korea Kaskazini kwa jina lake rasmi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Korea.

Mapema mwaka huu, Putin na Kim walitia saini makubaliano ya kuahidi kwamba watasaidiana katika tukio la “uchokozi” dhidi ya nchi zote mbili – ingawa haikuwa wazi ni nini kilimaanisha uchokozi.

Kim ameshutumiwa kuisaidia Urusi katika vita dhidi ya Ukraine kwa kuipatia silaha badala ya msaada wa kiuchumi na kiteknolojia.

Rigathi Gachagua: Hoja ya kumuondoa madarakani Naibu wa Rais wa Kenya yaanza kujadiliwa bungeni

.

Bunge la Kitaifa nchini Kenya limeanza kujadili hoja ya kuondolewa madarakani kwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua.

Hatua hii inawadia baada ya Mbunge wa Kibwezi Magharibi Mwengi Mutuse kuwasilisha sababu 11 kupitia hoja ya kutaka kumuondoa madarakani mnamo tarehe 26 Septemba.

Baadaye, naibu wa rais atakuwa na fursa ya kujitetea.

Gachagua amekanusha shutuma zote dhidi yake katika kikao na wanahabari siku ya Jumatatu.

Mchakato huo umeanza kwa kuwasilishwa kwa Ripoti ya zoezi la Ushirikishwaji wa Umma ambalo liliendeshwa kuhusu kuondolewa kwake madarakani, ambapo Wakenya walitoa maoni yao kwa kila tuhuma 11 zinazomkabili Gachagua.

Iwapo hoja hiyo itapata uungwaji mkono wa thuluthi mbili (233) ya wabunge 349, itawasilishwa kwa Seneti.

Hata hivyo ikiwa wabunge 117 wataikataa, naibu wa rais atasalia madarakani.

Israel inasema imeanza operesheni ya ardhini kusini-magharibi mwa Lebanon

Jeshi la Ulinzi la Israel limetangaza hivi punde kwamba limeanza operesheni ndogo ya ardhini dhidi ya Hezbollah katika sehemu ya magharibi ya kusini mwa Lebanon tangu jana.

Operesheni ya ardhini ya Israel kusini mwa Lebanon ilianza tarehe 30 Septemba – hadi sasa, ilikuwa imelenga upande wa mashariki wa mpaka.

IDF pia inasema ni mara ya kwanza kwa wanajeshi wa akiba wa IDF kutumika katika operesheni za mapigano kusini mwa Lebanon.

Hezbollah inasema imerusha makombora zaidi kaskazini mwa Israel

Wakati huo huo, Hezbollah inasema ilirusha makombora zaidi kaskazini mwa Israel usiku kucha.

Kundi hilo linasema lililenga maeneo yenye makombora ya Israel huko Dishon na Dalton kaskazini mwa Israel.

Pia inasema ilirusha makombora kwenye “mkusanyiko wa vikosi vya adui” huko Yir’on, makazi mengine kaskazini mwa Israel, karibu na mpaka wa Lebanon.

Mapema usiku, Hezbollah ililenga makazi ya Waisraeli magharibi zaidi, ilisema kwenye mtandao wake wa Telegraph ya lugha ya Kiingereza.

Israel yasema ilimuua kamanda wa Hezbollah huko Beirut huku mashambulizi ya anga yakiendelea

.

Jeshi la Israel linasema kuwa limemuua kamanda wa Hezbollah katika shambulio lililofanyika jana katika eneo la Beirut.

Vikosi vya Ulinzi vya Israel vinasema Suhail Hussein Husseini alitekeleza jukumu “muhimu” katika kusafirisha silaha kati ya Iran na Hezbollah.

Bado hatujaona uthibitisho wowote wa kifo chake kutoka kwa Hezbollah.

Kulikuwa na milipuko zaidi jana usiku katika mji mkuu wa Lebanon, huku vyombo vya habari vya Lebanon vikiripoti angalau mashambulizi 10 ya anga huko Dahieh – kitongoji cha kusini mwa Beirut kikichukuliwa kuwa ngome ya Hezbollah.

Kaskazini mwa Israel, ving’ora vya kuonya mashambulizi ya roketi viliendelea kusikika usiku kucha na miji kadhaa zaidi ilitangazwa kuwa maeneo ya kijeshi yaliyofungwa.

Hapo awali Hezbollah ilisema ililenga viunga vya Tel Aviv kwa roketi, na Israel ilisema Hezbollah ilikuwa imerusha makombora 190 kufikia Jumatatu.

Cissy Houston, mwimbaji nguli na mama wa Whitney Houston, afariki dunia

.

Cissy Houston, mwimbaji mashuhuri wa nyimbo za injili na mamake Whitney Houston, amefariki dunia Jumatatu asubuhi akiwa na umri wa miaka 91, familia yake ilisema katika taarifa.

Houston, mwimbaji aliyeshinda Tuzo ya Grammy mara mbili, alifariki nyumbani kwake New Jersey alipokuwa katika huduma ya wagonjwa wa Alzheimer, binti-mkwe wake Pat Houston alisema.

“Mioyo yetu imejaa uchungu na huzuni. Tumempoteza mama wa familia yetu,” alisema, akiongeza kuwa mama-mkwe wake alikuwa “mtu hodari na imara” katika maisha ya familia hiyo.

Houston alifurahia kazi ya uimbaji yenye mafanikio ya miongo kadhaa, ambapo aliigiza pamoja na wasanii maarufu kama Elvis Presley na Aretha Franklin.

Waziri Mkuu wa zamani wa Lebanon asema nchi yake imetelekezwa na jumuiya ya kimataifa

.

Aliyekuwa waziri mkuu wa Lebanon wakati wa vita vyake vya mwisho na Israel mwaka 2006 ameambia BBC kuwa nchi yake imetelekezwa na jumuiya ya kimataifa.

Fouad Siniora alisema ni jambo lisilokubalika kuiacha Lebanon isambaratike, na kulikuwa na ukosefu wa kujitolea linapokuja suala la kujaribu kurejesha amani.

“Sasa tuko katika hali ngumu sana inayohitaji juhudi za kweli ndani ya nchi, pia kwa upande wa Waarabu na kimataifa.

“Unaweza kushinikiza mambo – wakati mwingine hadi kufikia hatua ya kukaribia kusambaratika – katika janga kubwa bila kutambua baadaye itakuwa inamaanisha nini.

“Inatokea wakati utawala wa Marekani una shughuli nyingi na uchaguzi.

“Na hatuna uwezo wa kumchagua rais, kwa sababu baadhi ya makundi hasa Hezbollah, yamekuwa yakisisitiza kwamba wanataka rais ambaye hatakuja kusaliti kundi hilo baadaye,” Siniora alisema.

Vita vya mwisho kati ya Lebanon na Israel, karibu miaka 20 iliyopita, vilianza pale wapiganaji wa Hezbollah walipovuka mpaka na kuwashambulia wanajeshi wa Israel.

Wawili walitekwa nyara na watatu waliuawa, na kusababisha vita vya mwezi mzima.

Katika siku zilizofuata, Siniora alitoa taarifa kwa umma kuitenganisha serikali ya Lebanon na kile kilichotokea.

Anafikiria, viongozi wa sasa wa nchi wameshindwa kufanya kile ambacho raia waliwaamini nacho, kufanya kama ilivyotokea wakati ule.

“Serikali hii haikufanya kile ambacho serikali yangu ilifanya siku hiyo. Serikali yangu ilikuwa wazi na ilidhamiria kusema kwamba hatukujua, na hatukuwa tumearifiwa juu ya mpango wa Hezbollah wa kuvuka mpaka na kuteka nyara na kuua wanajeshi wa Israel.

“Wakati huu hakujakuwa na hatua yoyote iliyofanywa na serikali ya Lebanon. Faida ya tulichofanya ni kwamba tuliweka mpaka kati ya serikali ya Lebanon na Lebanon upande mmoja, na Hezbollah kwa upande mwingine,” alielezea.

Siniora hajaegemea upande wowote katika tathmini yake ya uhuru uliopotea wa Lebanon.

“Kiuhalisia, Lebanon kama taifa imetekwa nyara na Hezbollah. Na nyuma ya Hezbollah ni Iran.

“Bunduki hii iliyokuwa inashikiliwa na Hezbollah, badala ya kunyooshewa Israel, ilianza kunyooshewa ndani ya nchi na ikaanza kutumika kama njia ya Iran kuingilia Syria, Iraq na Yemen. Lebanon haiwezi kujihusisha na vita vya namna hiyo.

” Siniora pia alikuwa mmoja wa wasanifu wa azimio la UN 1701, makubaliano ambayo yalimaliza vita vya 2006

‘Jinsi Israeli inavyojilinda ni muhimu,’ asema Kamala Harris

.

Makamu wa Rais wa Marekani Kamala Harris amefanya mahojiano ya dakika 60 na shirika la habari la CBS News ambapo amebanwa kuhusu masuala kama vile Mashariki ya Kati, Ukraine, umiliki wa bunduki na uhamiaji.

Katika mahojiano hayo yaliyorekodiwa, Harris aliulizwa nini Mashariki ya Kati inaweza kufanya kuzuia vita kuenea au hata kufikia kiwango cha “kutoweza kudhibitika”.

“Israel ina haki ya kujilinda,” alisema. “Tungefanya hivyo. Na namna inavyofanya hivyo ni muhimu. Wapalestina wengi mno wasio na hatia wameuawa. Vita hivi lazima vikome,” Harris alijibu.

Pia aliulizwa jinsi Marekani ilivyomwomba Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu kukubali kusitishwa kwa mapigano, ili kutoingia Lebanon – lakini maombi yote mawili yamepuuzwa.

Harris alisema Marekani “haitaacha kutafuta kile ambacho ni muhimu kwa Marekani, kuwa wazi kuhusu wapi tunasimama ili vita hivi viishe”.

Aliongeza kuwa muungano wa Israel na Marekani bado ni imara.

Israel yaadhimisha mwaka mmoja tangu shambulio la Hamas huku mapigano yakiendelea

.

Israel imefanya sherehe za kuwakumbuka wahanga wa mauaji ya watu na utekaji nyara uliofanywa na Hamas tarehe 7 Oktoba 2023, huku mapigano yakiendelea katika Ukanda wa Gaza na Lebanon.

Mwaka mmoja baada ya shambulio hilo – ambalo lilishuhudia takriban watu 1,200 wakiuawa na 251 kuchukuliwa mateka – Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu aliapa kusitisha shambulio kama hilo kutokea tena, akisema vikosi vya kijeshi vya Israel “vilikuwa vinabadilisha uhalisia wa hali ya usalama” eneo hilo.

Tangu tarehe 7 Oktoba, karibu watu 42,000 wameuawa wakati wa mashambulizi ya Israel huko Gaza, kulingana na wizara ya afya inayoendeshwa na Hamas.

Wakati siku ya kumbukumbu hiyo ikiendelea, Israel ilisema imenasa zaidi ya makombora 100 yaliyorushwa na Hezbollah nchini Lebanon pamoja na makombora yaliyorushwa na Wahouthi wa Yemen na Hamas huko Gaza.

Oktoba iliyopita, watu wenye silaha kutoka Hamas huko Gaza walivunja uzio wa mpaka na kuvamia vijiji vya karibu vya Israel, Kibbutzim, vituo vya kijeshi na tamasha la muziki la Nova.

Siku ya Jumatatu, familia za mamia waliouawa na makumi ya watu waliochukuliwa mateka katika tamasha hilo walikusanyika kwenye eneo kwa hafla ya kumbukumbu ya kwanza ya siku hiyo.

Wakiwa wameshikilia picha za wapendwa wao walisikiliza wimbo wa mwisho uliochezwa kwenye tamasha hilo kabla ya Rais wa Israel Isaac Herzog kuongoza kimya cha dakika moja saa 06:29, muda ambao shambulio hilo lilianza.

Mamlaka nchini Uganda imezimepiga marufuku sherehe za mazishi zinazohusishwa na densi na vitendo vya kimapenzi na ambazo hufanyika nyakati za usiku, maarufu kama Disco matanga, kutokana na ripoti za unyanyasaji wa kingono kwa mujibu wa mashirika ya haki ambayo yameendlea kukashifu sherehe hizo.

Mamlaka nchini Zambia, zimethibitisha watu kumi kufariki na wengine watano kujeruhiwa baada ya mgodi kuporomoka katika wilaya ya Mimbwa kusini mwa nchi hiyo, mamlaka ya polisi ikisezma imeanzisha uchunguzi kubaini chanzo cha ajali hiyo wakati pia wakifanya kazi kubaini idadi kamili ya waliokuwa kwenye mgodi huo wakati wa ajali hiyo.

Makamau wa rais wa Marekani na mgombea wa urais wa chama cha Democratic, Kamala Harris amesema katika mahojiano hapo jana kwamba iwapo atachaguliwa katika uchaguzi wa mwezi ujao, hatokutana na rais Vladimir Putin kwa mazungumzo ya amani yakuamaliza vita ikiwa Ukriane haitakuwa imewakilishwa, akisema lazima Ukraine iwe na usemi kuhusu mustakabali wa Ukraine.

Mahakama moja ya umoja wa ulaya, mwezi ujao inatarajiwa kusikiliza kesi kuhusu kuvuja kwa ujumbe wa kibinafsi unaoripotiwa kutumwa na rais wa tume ya EU Ursula von der Leyen uliohusu ununuzi wa chanjo ya virusi vya Corona, ambapo gazeti moja la Marekani limeishtaki tume ya EU kwa kukataa kuweka wazi maudhui ya jumbe hizo za Von der Leyen kwa mkuu wa kampuni ya kutengeneza chanjo ya Pfizer Albert Bourla, licha ya uhuru wa kupata taarifa.

Nchini Afrika Kusini, walinzi sita wanaripotiwa kuuawa kwa kupigwa risasi wakati walikuwa wanajiandaa kuenda kupiga doria kwenye shule moja, tukio linaloripotiwa kutokea mita chache kutoka eneo ambapo watu wengine 18 waliuawa takriban wiki moja iliopita, polisi ikisema tayri wanawashikilia washukiwa sita.

Ufaransa imetoa hakikisho la kufuata kanuni za matumizi za umoja wa ulaya, wakati huu waziri mpya wa fedha akitarajiwa kuwasilisha bajeti ya kitaifa kwa bunge siku ya Alhamisi, bajeti ambayo utawala wa rais Emmanuel Macron unatumai utakabiliana na deni la taifa kupitia kupunguza matumizi na kodi mpya.

Kuelekea uchaguzi wa wabunge nchini Senegal, rais mstaafu Macky Sall ametuma barua ya kujiuzulu kwa rais wa Ufaransa Emmanuel Macron, ambaye alikuwa amemteua kushikilia wadhifa wa mjumba maalum wa mkataba wa Paris, hatua mabayo ameichukua ili kuelekea nguvu zake kwenye uchaguzi huo wa Novemba 17 akiwa kiongozi wa muungano wa upinzani Takku-Wallou

Bunge la Ethiopia limeidhinisha uteuzi wa Taye Astike Selassie, kuwa rais mpya, kuchukua nafasi ya rais wa kwanza mwanamke Sahle-Work Zewde, ripoti zikieleza hatua hii imeafikiwa kufuatia tofauti zilizoibuka kati ya Zewde na Waziri mku Abiy Ahmed katika miaka ya hivi karibuni, na kwamba Zewde alikuwa akisubiri muda wake kutamatika baadyae mmwezi huu.

Nchini Nigeria, zaidi ya watu 350 wanaripotiwa kufariki kutokana na ugonjwa wa kipindundu katika kipindi cha miezi tisa ya kwanza ya mwaka huu, hii ikiwa ni ongezeko la asilimia 239 ikilinganishwa na kipindi sawia mwaka uliopita, takwimu za kituoa cha kudhibiti magonjwa nchini humo NCDC zikionesha mji mkuu wa Lagosa kuathirika zaidi.

Habari Mseto

Aidha idadi ya visa pia vimeongezeka hadi 10,837 kutoka 3,387 katika kipindi sawia mwaka uliopita.

Nchi ya Marekani, imewataka raia wake kutosafiri nchini Rwanda, kutokana na tishio la mlipuko wa virusi hatari vya Marburg, ambavyo tayari vimesababisha vifo vya 12, wakati huu taifa hilo la Afrika Mashariki likiwa mbioni kutoa chanjo kukabiliana na mlipuko wa ugonjwa huo.

Jeshi la Sudan, limeendelea kusonga mbele katika majimbo kadhaa, sambamba na makabiliano ilioanzisha jijini Khartoum karibu wiki mbili zilizopita, haya yakijiri baada ya jeshi mwishoni mwa juma lililopita kutangaza kuchukua udhibiti wa eneo la Jebel moya baada ya mapigano makali dhidi ya wapiganaji wa RSF.

Jaji wa nchini Marekani ameamuru kampuni kubwa ya teknolojia ya Google kufungua simu zake mahiri za Android kwa maduka pinzani ya programu.

Agizo hilo linakuja baada ya kesi ya kutokuaminika ambapo mahakama iliamua kwamba Google ilikuwa na mamlaka ya ukiritimba kinyume cha sheria kwa jinsi inavyoendesha duka lake la AndroidPlay.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Haiti amepuuza sera iliyotangazwa wiki iliyopita na Jamhuri ya Dominika kuwafukuza makumi ya maelfu ya wahamiaji kurejea Haiti, ambako ghasia za magenge zinachochea mgogoro mkubwa wa kibinadamu.

Raia wa Msumbiji watapiga kura kesho Jumatano kumchagua rais ambaye wengi wanatarajia alete amani katika jimbo la kaskazini lenye utajiri wa mafuta na gesi ambalo limeharibiwa na wanajihadi wa kiislamu kwa takriban miaka saba.

Serikali mpya ya Ufaransa, inayoongozwa na Waziri Mkuu wa kihafidhina Michel Barnier, italazimika kuegemea kwenye uungwaji mkono wa mrengo wa kulia wakati inakabiliwa na kura ya kutokuwa na imani na bunge siku ya Jumanne.

Kiongozi wa muda wa Bangladesh Muhammad Yunus amekataa kutoa muda wa kufanyika kwa uchaguzi kufuatia kuondolewa madarakani kwa mtangulizi wake wa kiimla, akisema katika mahojiano yaliyochapishwa Jumanne kwamba mageuzi yanahitajika kabla ya uchaguzi.

All Rights Reserved © Cantona Group PLC||2024


Discover more from cantonadigital

Subscribe to get the latest posts sent to your email.

Leave a Reply