Radio Fortune Africa -Ukweli na Burudani
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

Na : Cantona Joseph|RFA

Mamlaka ya mahakama ya Uturuki imetoa hati ya kukamatwa kwa Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, waziri wake wa ulinzi na maafisa wengine 35 wakuu wa Israel kwa tuhuma za “uhalifu wa kivita na mauaji ya kimbari.”
Mahakama ya Uturuki yatoa vibali vya kukamatwa kwa Netanyahu na waziri wake

Mamlaka ya mahakama ya Uturuki imetoa hati ya kukamatwa kwa Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, waziri wake wa ulinzi na maafisa wengine 35 wakuu wa Israel kwa tuhuma za “uhalifu wa kivita na mauaji ya kimbari.”
Ofisi ya mwendesha mashtaka wa Istanbul ilisema hukumu hizo zinahusiana na vitendo vyao huko Gaza na dhidi ya kundi la kimataifa ambalo lilikuwa likijaribu kutoa msaada kwa Wapalestina waliozingirwa. Israel imekanusha vikali tuhuma za kufanya mauaji ya halaiki huko Gaza.
Hatua hiyo ya kiishara inakuja wakati serikali ya Marekani imezidi kukiri jukumu muhimu la Uturuki katika kusaidia kuwapokonya silaha Hamas na uwezekano wa kushiriki katika kikosi cha kimataifa cha kuunganisha mpango wa amani wa Donald Trump huko Gaza.
Ripoti zinaonyesha kuwa uamuzi wa mamlaka ya mahakama ya Uturuki ulifanywa ndani ya mfumo wa uchunguzi wa “uhalifu uliofanyika” wakati wa mashambulizi ya Israel dhidi ya raia, hospitali, na misafara ya misaada, hasa “Global Solidarity Convoy” huko Gaza.
Kufungwa kwa Serikali Marekani: Maelfu ya safari za ndege zaahirishwa

Zaidi ya safari 5,000 za ndege nchini Marekani zilisitishwa au kucheleweshwa jana baada ya mashirika ya ndege ya Marekani kuagizwa kupunguza safari za anga wakati wa kufungwa kwa serikali.
Safari za ndani katika viwanja 40 vya ndege vilivyo na shughuli nyingi zaidi nchini humo zimeathiriwa huku maafisa wakijaribu kupunguza mzigo kwa waongoza ndege.
Viwanja vya ndege vinakabiliwa na uhaba wa waongoza ndege kutokana na likizo za ugonjwa na ufanyaji kazi bila malipo wakati wa kufungwa kwa serikali ya Marekani.
Muungano wa wafanyakazi, ambao unawakilisha wahudumu 55,000 wa ndege nchini Marekani, ni sehemu ya kundi lililotoa wito wa kusitishwa ufungwaji wa shughuli za serikali, likisema usalama wa wafanyakazi wa anga uko hatarini.
“Sababu pekee sekta ya usafiri wa anga inaendelea kufanya kazi wakati wa kufungwa kwa serikali ni kutokana na waongoza ndege wa Marekani na maafisa wa usafiri wanafanya kazi bila malipo.
Wakati huohuo, kila mtu anayesaidia kazi yao ya kutuhakikishia usalama na ulinzi amerejeshwa nyumbani bila malipo,” alisema Sarah Nelson, rais wa Chama cha Wahudumu wa Ndege
Waziri wa Ulinzi wa Pakistan: Mazungumzo na serikali ya Taliban huko Istanbul ‘yamefeli’

Waziri wa Ulinzi wa Pakistan Khawaja Muhammad Asif anasema duru ya tatu ya mazungumzo ya Istanbul imeshindwa kwa sababu, kulingana naye, wawakilishi wa nchi yake hawakuweza kutatua “tofauti kubwa” na serikali ya Taliban nchini Afghanistan.
Ameongeza kuwa usitishaji vita kati ya nchi yake na serikali ya Taliban utaendelea kuwepo maadamu hakuna mashambulizi yoyote yatakayotekelezwa kutoka ardhi ya Afghanistan.
Duru ya tatu ya mazungumzo kati ya wawakilishi wa pande hizo mbili, iliyoanza mjini Istanbul siku ya Alhamisi kwa upatanishi wa Uturuki na Qatar, iliendelea kwa siku ya pili mfululizo hapo jana.
Wakati huo huo, Tahir Hussain Andrabi, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Pakistan, amesema katika mkutano na waandishi wa habari kwamba “hakuna mkwamo” katika mazungumzo ya amani yanayoendelea na serikali ya Taliban nchini Afghanistan.
Kwa upande mwingine, saa chache kabla ya matamshi ya Bwana Asif, Noorullah Noori, Waziri wa Mipaka na masuala ya Kikabila wa serikali ya Taliban, alionya Pakistan kutokuwa na “kiburi” kwa kuwa na teknolojia ya hali ya juu.
Israel yapokea jeneza, Hamas yasema lina mwili wa mateka wa Gaza

Israeli imepokea jeneza ambalo Hamas na Palestina Islamic Jihad walisema lina mwili wa mateka, jeshi la Israeli linasema.
Hamas walisema mwili huo ulipatikana Ijumaa huko Khan Younis kusini mwa Gaza. Mwili huo umesafirishwa hadi Israel kupitia Shirika la Msalaba Mwekundu kwa ajili ya utambuzi.
Kabla ya makabidhiano haya, Hamas ilikuwa imewarudisha mateka wote 20 walio hai na mateka 22 kati ya 28 waliokufa chini ya awamu ya kwanza ya makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyoanza tarehe 10 Oktoba.
Watano kati ya mateka sita waliokufa ambao bado wako Gaza walikuwa Waisraeli na mmoja alikuwa rais wa Thailand. Israel imeikosoa Hamas kwa kutorudisha miili yote. Hamas inasema ni vigumu kuwapata chini ya vifusi.
Mwanajeshi wa zamani wa Uingereza akamatwa kwa madai ya mauaji ya mwanamke Mkenya mwaka 2012

Mwanajeshi wa zamani wa Uingereza anakabiliwa na kesi nchini Kenya kuhusiana na madai ya mauaji ya mwanamke mwenye umri wa miaka 21 nchini humo mwaka wa 2012.
Shirika la Kitaifa la kushughulikia Uhalifu (NCA) lilisema Robert James Purkiss alikamatwa huko Tidworth, Wiltshire mnamo Novemba 6 na akafikishwa katika Mahakama ya Hakimu
Mkazi ya Westminster Ijumaa. Alikamatwa na maafisa maalum kutoka Kitengo cha Kitaifa cha a NCA kuhusiana na mauaji ya Agnes Manjiru baada ya hati kutolewa mwezi Septemba, shirika hilo liliongeza.
Bw. Purkiss, mwenye umri wa miaka 38, aliiambia mahakama kwamba alikusudia kupinga kesi hiyo ya kupelekwa Kenya na aliwekwa kizuizini kabla ya kufikishwa tena katika mahakama hiyo hiyo mnamo Novemba 14.
Mawakili wake waliiambia mahakama kwamba “anakana vikali” shutuma za mauaji dhidi yake.Mwili wa Bi. Wanjiru uligunduliwa kwenye tanki la maji taka karibu na hoteli katika mji wa Nanyuki, yapata maili 200 kaskazini mwa Nairobi, miezi mitatu baada ya kupotea mnamo Machi 31, 2012.
Alikuwa na mtoto wa miezi mitano wakati huo.
Mwili wake ulipatikana karibu na kambi ya mafunzo ya jeshi la Uingereza. Usiku aliouawa, inasemekana alikuwa kwenye baa na marafiki ambapo wanajeshi wa Uingereza pia walikuwepo.
Wanaharakati wa Kenya Bob Njagi na Nicholas Oyoo waachiliwa baada ya siku 38

Rais wa Chama cha Wanasheria nchini (LSK), Faith Odhiambo, ameunga mkono kuachiliwa kwa wanaharakati Nicholas Oyoo na Bob Njagi, ambao waliachiliwa huko Busia Alhamisi usiku baada ya siku 38 za kutoweka kwa lazima.
Katika taarifa yake kuhusu X, Odhiambo alisema kuwa pamoja na VOCAL Africa na Amnesty Kenya, wanakaribisha kuachiliwa kwao.
Alisema wawili hao walikuwa wametoweka kwa zaidi ya mwezi mmoja kabla ya kuachiliwa, na hivyo kuashiria kile alichokitaja kuwa wakati muhimu kwa watetezi wa haki za binadamu katika eneo hilo.
“Tunakaribisha kuachiliwa kwa Nicholas Oyoo na Bob Njagi jana usiku huko Busia baada ya siku 38 za kutoweka kwao,” taarifa hiyo ilisoma.
Odhiambo aliwashukuru wale waliofanya kampeni ya kuachiliwa kwao, ikiwa ni pamoja na familia za wanaharakati, Chama Huru cha Kenya, watetezi wa haki za binadamu, waandishi wa habari, na wizara za mambo ya nje nchini Kenya na Tanzania.
“Tunatoa shukrani zetu kwa familia zao, wenzao wa harakati Huru ya Kenya, watetezi wa haki za binadamu, waandishi wa habari, wizara za mambo ya nje nchini Kenya na Tanzania, na raia wote watendaji ambao wamefanya kampeni bila kuchoka kwa wakati huu,” alisema.
Trump aipatia Hungary msamaha dhidi ya vikwazo vya mafuta na gesi

Rais wa Marekani, Donald Trump, ameipatia Hungary mwaka mmoja wa msamaha wa vikwazo vinavyohusiana na ununuzi wa mafuta na gesi kutoka Urusi, afisa wa Ikulu ya White House amethibitishia BBC.
Awali, Trump alisema angefikiria kutoa msamaha huo wa vikwazo, ambavyo vinalenga kusaidia kumaliza vita vya Ukraine, kwa Waziri Mkuu wa Hungary, Viktor Orban.
Akizungumza Ijumaa wakati wa ziara ya Orban Ikulu ya White House, Trump alisema huenda kukatolewa kibali maalum kwa sababu “ni vigumu sana kwa Orban kupata mafuta na gesi kutoka maeneo mengine.”
Kauli hizo zinakuja baada ya Marekani kuwekea vikwazo makampuni mawili makubwa ya mafuta ya Urusi mwezi uliopita, na kutishia kuchukua hatua dhidi ya wale watakaonunua mafuta kutoka kwao.
Baada ya mkutano huo, Waziri wa Mambo ya kigeni wa Hungary, Péter Szijjártó, aliandika kwenye mtandao wa X kwamba Marekani imeipa Budapest “msamaha kamili na usio na mipaka dhidi ya vikwazo vya mafuta na gesi.”
Uamuzi huu wa Trump unachukuliwa kuwa ushindi mkubwa kwa Orban, ambaye awali alisema kuwa vikwazo hivyo vingedhoofisha uchumi wa nchi yake.
All Rights Reserved © The Cantona Group PLC||2025
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.