Radio Fortune Africa -Ukweli na Burudani
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

By : Cantona Joseph|RFA

Idadi ya watu wanaojulikana kuuawa katika msako mkali wa polisi katika mji wa Rio de Janeiro nchini Brazil siku ya Jumanne imeongezeka hadi 132, maafisa wanasema.
Hii ni zaidi ya mara mbili ya idadi iliyotajwa baada ya operesheni ya polisi katika favelas (vitongoji maskini) vya Alemão na Penha, kaskazini mwa Rio de Janeiro, Jumanne.
Ofisi ya mtetezi wa umma, ambayo hutoa usaidizi wa kisheria kwa maskini, ilitangaza idadi mpya ya vifo hadharani baada ya wakaazi waliokuwa na huzuni kuweka maiti kadhaa katika mraba mapema Jumatano.
Uvamizi huo wa polisi ulikuwa mbaya zaidi katika jiji hilo, ambapo mamlaka kwa miongo kadhaa imejaribu kudhibiti magenge ambayo yanadhibiti vitongoji vingi masikini.
Gavana Castro alisema kuwa uvamizi huo ulipangwa kwa miezi miwili na ulitokana na uchunguzi wa kina.
Miongoni mwa waliokamatwa ni mwanamume anayedaiwa kuwa mfanyabiashara mkuu wa dawa za kulevya katika kikosi cha Red Command.
Gavana huyo pia alichapisha picha kwenye mitandao ya kijamii za maafisa wanne wa polisi waliouawa kwenye operesheni hiyo.
Aliwasifu maafisa waliouawa katika kile alichokiita “siku ya kihistoria” ambapo alisema “walikabiliana na uhalifu uliopangwa”.
Rafael Soares, mwandishi wa habari wa Brazil anayeangazia uhalifu mjini Rio, aliiambia BBC News Brasil kwamba genge la Red Command imekuwa kwenye mashambulizi mjini Rio katika miaka ya hivi karibuni, na kutwaa maeneo ambayo ilipoteza kwa wapinzani wake, First Capital Command (PCC).
Soares aliongeza kuwa operesheni ya polisi ni sehemu ya juhudi za Gavana Castro kukabiliana na uhalifu katika jiji hilo kabla ya uchaguzi mwaka ujao.
Uvamizi huo wa polisi pia unakuja siku chache kabla ya jiji hilo kuandaa Mkutano wa Mameya wa Dunia wa C40 – mkutano wa takriban mameya 100 kutoka miji inayoongoza duniani – na Tuzo ya Earthshot – tuzo ya mazingira ambayo itatolewa na Mwanamfalme William mnamo 5 Novemba.
Kimbunga Melissa: Jamaica yakumbwa na giza baada ya dhoruba kali

Huko Jamaika, mamia ya watu bado wamekwama juu ya mapaa ya nyumba zao wakisubiri msaada, huku umeme ukiwa umekatika kote nchini.
Waziri Mkuu Andrew Holness alielezea hali ya sasa kama “uharibifu wa kutisha kabisa”, akibainisha kuwa: “Takribani asilimia 80 hadi 90 ya paa za nyumba zimeanguka, na miundombinu muhimu kama hospitali, maktaba, vituo vya polisi, na majengo ya bandari imeathiriwa vibaya.”
Amesema juhudi za uokoaji zinaendelea, lakini zimekuwa ngumu kutokana na barabara zilizosombwa na maji na mawasiliano yaliyokatika.
Mfalme Charles wa Uingereza, ambaye pia ni Mkuu wa Nchi wa Jamaika, alitoa ujumbe wa rambirambi akisema kwamba ana “huzuni kuu na wasiwasi mkubwa” kutokana na maafa yaliyosababishwa na Melissa kote Kisiwani.
“Kimbunga hiki cha kihistoria kinatukumbusha haja ya dharura ya kurejesha usawa wa asili, kwa manufaa ya wale wote ambao maisha na riziki zao zimevunjwa na janga hili la majonzi,” alisema Mfalme huyo katika taarifa yake rasmi.
Shirika la Caribbean Meteorological Organisation (CMO) limeonya kuwa athari za Melissa bado hazijaisha, likisema kuwa upepo mkali na mvua kubwa zitaendelea kwa siku kadhaa katika baadhi ya maeneo ya Bahamas, Cuba na Hispaniola.
Limewataka wakazi wa maeneo hatarishi kuendelea kuwa makini, wakati timu za uokoaji na mashirika ya misaada ya kibinadamu yakiharakisha kufikisha chakula, maji safi, na huduma za afya kwa waathiriwa.
Kimbunga Melissa kimeelezwa kuwa ndicho kimbunga kikali zaidi kuwahi kupiga Kisiwa hicho katika kipindi cha zaidi ya miaka 30, na wataalamu wa mazingira wanasema matukio kama haya yanaonyesha ongezeko la athari za mabadiliko ya tabianchi katika eneo hilo linalokabiliwa na dhoruba mara kwa mara.
Watu wawili wakiri kuhusika na wizi wa vito katika makumbusho Louvre nchini Ufaransa

Mwendesha mashtaka wa Paris, Laure Beccuau, amesema wanaume wawili waliokamatwa kuhusiana na wizi wa kihistoria uliofanyika katika Makumbusho ya Louvre wiki mbili zilizopita wamekiri kwa sehemu kuhusika katika tukio hilo lililohusisha uporaji wa vito vya kifahari vya kifalme.
Kwa mujibu wa maafisa wa uchunguzi, wawili hao wanashukiwa kuwa sehemu ya genge lililotumia vifaa vya kukata kwa nguvu za umeme kuvunja milango ya Ukumbi wa Apollon, na kuiba baadhi ya vito vya kifalme vya Ufaransa vyenye thamani ya zaidi ya euro milioni 88 (takribani pauni milioni 76 au dola milioni 102 za Kimarekani).
Wizi huo ulifanyika mchana wa tarehe 19 Oktoba, ambapo wezi wanne walivamia jengo hilo maarufu la sanaa linalojulikana kuwa na idadi kubwa zaidi ya wageni duniani na kutokomea na mali hiyo ya thamani kubwa.
“Tunashtushwa na ujasiri wa wahalifu hawa na ubunifu wa uhalifu huu wa waziwazi,” alisema Beccuau akizungumza na waandishi wa habari mjini Paris.
Beccuau alisema kuwa vito hivyo bado havijapatikana, na uchunguzi unaonyesha huenda genge lililohusika lina washiriki wengi zaidi ya wale wanne waliorekodiwa kwenye kamera za usalama za jengo hilo.
Aidha, alibainisha kuwa watuhumiwa hao, wote wakiwa na umri wa miaka thelathini, wana rekodi za uhalifu na walitambuliwa kupitia vinasaba (DNA) vilivyopatikana kwenye eneo la tukio.
Mmoja wao alikamatwa akiwa anajaribu kupanda ndege ya kuelekea Algeria, huku mwenzake akibainika hakupanga kuondoka nchini, kinyume na taarifa za awali za vyombo vya habari.
Mwendesha mashtaka huyo alisisitiza kuwa hakuna ushahidi unaoashiria ushirikiano wa ndani, akisema: “Kwa sasa, hakuna dalili zinazoonyesha kuwa mtu yeyote kutoka ndani ya makumbusho alihusika.”
Hata hivyo, uchunguzi bado unaendelea, na Beccuau hakufuta uwezekano wa kuwepo kwa washirika zaidi, wakiwemo wale waliopanga kupokea vito vilivyoibwa.
Aliongeza: “Ninabaki na matumaini kuwa [vito hivyo] vitapatikana na kurejeshwa Louvre, na hatimaye kurudishwa kwa taifa la Ufaransa.”
Uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa wezi hao walikaa ndani ya jengo kwa dakika nne pekee, kabla ya kutoroka saa 3:38 asubuhi kwa kutumia pikipiki mbili, kisha kubadilisha magari walipokuwa njiani kuelekea mashariki mwa Paris.
Katika harakati za kutoroka, taji lililowahi kumilikiwa na Malkia Eugenie, mke wa Napoleon wa Tatu, liliachwa nyuma na wezi hao.
Maafisa wa makumbusho wamesema uharibifu wa taji hilo bado unakaguliwa.
Hakuna mtu aliyedhuriwa katika uvamizi huo, ingawa tukio hilo limeibua maswali mazito kuhusu usalama wa urithi wa kitamaduni wa taifa hilo.
All Rights Reserved © The Cantona Group PLC||2025
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.