Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

Miezi mitatu baada ya Marekani na Israel kushambulia maeneo ya nyuklia ya Iran, picha mpya za satelaiti zinaonesha dalili za kazi ya ujenzi katika vituo vyake viwili muhimu vya urutubishaji.
Uchambuzi wa picha za satelaiti zenye ubora zilizonaswa na Maxar Technologies tarehe 18 Septemba unaonesha kazi kwenye eneo jipya na handaki kusini mwa jumba la uboreshaji la Natanz.
Magari mengi ya ujenzi yanaonekana katika eneo la kusini mwa jengo hilo huku kazi ya kuchimba ikionekana kuwa inaendelea.
Picha pia zinaonesha kazi ya kupanua eneo karibu na eneo hilo hilo.
Natanz ni kituo kikuu cha kurutubisha nyuklia cha Iran ambacho kinahifadhi mamia ya Sentifu (centrifuges) chini ya ardhi.
Ilipigwa na Israel na Marekani wakati wa vita vya siku 12 mwezi Juni, na kusababisha uharibifu wa majengo kadhaa ya ardhini.
Wakati huo huo, picha za satelaiti zilizonaswa na Maxar wa jumba la urutubishaji la Fordo tarehe 23 Septemba zinaonesha kuwa volkeno sita, ambazo hapo awali zilionekana kufuatia mashambulizi ya Marekani, sasa zimefunikwa.
Fordo, ambayo imefichwa ndani kabisa ya mlima, ililengwa na washambuliaji wa siri wa Jeshi la Anga la Marekani B-2 tarehe 22 Juni, kabla ya kushambuliwa tena na Israel siku moja baadaye.
Mkuu wa Shirika la Nishati ya Atomiki la Iran, Mohammad Eslami, aliiambia Sky News wiki hii kwamba Tehran imejitolea kujenga upya mitambo yake ya nyuklia nje.
Kulitambua taifa la Palestina ni ‘wazimu mtupu’- Netanyahu

Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu amezungumzia uamuzi wa nchi zikiwemo Ufaransa na Uingereza kutambua taifa la Palestina, na kuuita “kujiua kitaifa”.
Ni “wazimu mtupu, ni wazimu na hatutafanya hivyo,” Waziri Mkuu wa Israel anasema.
Katika hatua nyingine, Netanyahu amezungumzia shutuma kwamba Israel “inalenga raia makusudi”. “Kinyume chake ni kweli,” anasema, akisema kuwa Israel imeangusha “mamilioni ya vipeperushi na kutuma mamilioni ya maandishi” ili kuwafanya raia kuhama mji wa Gaza.
Wakati huo huo, “Hamas inajipandikiza kwenye misikiti, shule, hospitali, majengo ya ghorofa” anasema, ili kuwalazimisha raia “kukaa katika hatari” , “mara nyingi wakiwatishia kwa mtutu wa bunduki”.
Akiendelea na madai ya mauaji ya halaiki, Netanyahu anauliza ikiwa nchi inayofanya mauaji ya halaiki inawasihi watu kutoka katika hatari, “Je, Wanazi waliwataka Wayahudi kuondoka?”
Kisha anakana shutuma kwamba Israel inawaua watu kwa njaa huko Gaza kwa makusudi. Iwapo kuna watu wa Gaza ambao hawana chakula cha kutosha ni kwa sababu Hamas “huiba, huihifadhi na kuiuza”.
Mapema mwezi huu, tume ya uchunguzi ya Umoja wa Mataifa ilisema Israel imefanya mauaji ya halaiki dhidi ya Wapalestina huko Gaza.
Wizara ya mambo ya nje ya Israel ilishutumu ripoti hiyo kama “iliyopotoshwa na ya uwongo”.
Netanyahu amezungumza katika Mkutano Mkuu wa 80 wa Umoja wa Mataifa.
Wanamibia waonywa dhidi ya kufanya karamu kwenye makaburi baada ya tukio ‘la aibu’

Mamlaka ya Namibia imeonya watu kutofanya karamu kwenye makaburi baada ya mkusanyiko kwenye eneo la makaburi katika mji mkuu, Windhoek, kuzua hasira wikendi iliyopita.
Kulingana na maafisa wa Jiji la Windhoek, tukio katika makaburi ya Gammams “lilionesha viti vilivyokuwa vimepangiliwa kwa ajili ya kuketi, masanduku ya kutunza pombe baridi” vikiwa vinaonekana.
Mkazi mmoja wa Windhoek ambaye alishuhudia karamu hiyo alisema “lilikuwa jambo la aibu”.
Katika chapisho la Facebook, alielezea tukio ambalo alikutana na waombolezaji wakiingia eneo la makaburini, akisema “kutoka mlangoni hadi ndani, buti za gari zilikuwa wazi, watu walikuwa wakinywa, na makaburi yakaonekana kama vilabu vya pombe badala ya mahali pa kupumzika”.
Pia alisema makaburi hayo yaliachwa katika hali mbaya, huku chupa na makopo yakiwa yameachwa.
Katika taarifa iliyotolewa siku ya Alhamisi, Jiji la Windhoek lilisema hili “halikubaliki”, na kuongeza kuwa “inadharau utu wa marehemu [na] inasumbua familia zingine zinazoomboleza”.
Pia iliwakumbusha wakazi kuwa kuacha takataka kwenye makaburi ni kosa la jinai na kusema kutakuwa na “ufuatiliaji na utekelezaji mkali” ili kuhifadhi maeneo ya kuzikia.
“Makaburi ni maeneo matakatifu yaliyotengwa kwa ajili ya mazishi na ukumbusho wa marehemu,” ilisema. “Mikusanyiko ya kijamii, unywaji pombe, na kutupa takataka ndani ya maeneo ya makaburi ni marufuku kabisa.”
Hii si mara ya kwanza kwa Gammam kugonga vichwa vya habari.
Mnamo 2021 mwanaume mmoja alikamatwa baada ya video kusambaa ikimuonesha akifyatua risasi wakati wa mazishi yaliyofanyika huko.
Mazishi hayohayo pia yalishuhudia magari yakizungushwa katika eneo la maegesho karibu na eneo la mazishi.
Watu wengi wakamatwa kwa ulaghai wa ngono na mapenzi katika operesheni kali kote barani Afrika

Takribani watu 260 wanaoshukiwa kuwa matapeli wa mtandaoni wamekamatwa katika operesheni kali iliyotekelezwa katika nchi 14 za Afrika.
Operesheni hiyo, iliyoratibiwa na Interpol na kufadhiliwa na Uingereza, ililenga mitandao ya wahalifu inayotumia mitandao ya kijamii na majukwaa ya kidijitali kuchota pesa kutoka kwa waathiriwa katika ulaghai wa mapenzi, na katika kile kinachoitwa “ulaghai”, ambapo waathiriwa wanadanganywa kwa kutumia picha chafu.
“Haichukui muda mrefu kabla ya kujenga uhusiano na mtu fulani… na kwa haraka sana uaminifu huu unasambaratika,” mkurugenzi wa uhalifu wa mtandaoni wa Interpol Neal Jetton aliambia kipindi cha Newsday cha BBC, akielezea mbinu za wahalifu hao.
Zaidi ya waathiriwa 1,400 kote nchini Ghana, Kenya, Angola na kwingineko walitambuliwa.
Interpol inakadiria kuwa waathiriwa walipoteza jumla ya karibu $2.8m (£2.1m).
Watu wa rika mbalimbali walichukizwa na walaghai, Jetton aliongeza, lakini “kawaida ulaghai huu huathiri watu wazee”.
Wakati wa msako mkali ambao ulifanyika kati ya Julai na Agosti, polisi walitambua anuani za IP, miundombinu ya kidijitali na wasifu wa mitandao ya kijamii unaohusishwa na wanachama wa mashirika ya ulaghai.
Mtandao wa polisi wa kimataifa ulisema umejitolea “kuvuruga na kusambaratisha vikundi vinavyowawinda watu walio hatarini mtandaoni”.
Uholanzi na Uganda zafikia makubaliano ya kuwapokea kwa muda waomba hifadhi waliokataliwa

Uholanzi na Uganda wameingia katika makubaliano ya dhamira ya kushirikiana kuwapokea kwa muda waomba hifadhi waliokataliwa na Uholanzi, kwa mujibu wa taarifa rasmi iliyotolewa na serikali ya Uholanzi siku ya Alhamisi.
Makubaliano hayo yalitiwa saini jijini New York na Waziri wa Uhamiaji na Mambo ya Nje wa Uholanzi, David van Weel, pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje wa Uganda, Odongo Jeje Abubakhar, wakati wa Mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.
Mpango huo unalenga raia kutoka mataifa jirani na Uganda ambao wamekataliwa kupewa hifadhi nchini Uholanzi na hawawezi kurejea moja kwa moja katika nchi zao kwa sababu mbalimbali.
Kupitia mpango huo, wahusika wataruhusiwa kukaa Uganda kwa kipindi cha mpito hadi hali itakapowaruhusu kurejea makwao.
“Tunalichukulia hili kama hatua ya pamoja ya kudhibiti uhamiaji. Haki za msingi za watu wanaorudi kupitia Uganda zitaheshimiwa na kulindwa,” alisema Van Weel.
Aidha, alibainisha kuwa serikali ya Uholanzi inapanga kufanya mashauriano ya karibu na Umoja wa Ulaya pamoja na mashirika ya kimataifa kama IOM (Shirika la Uhamiaji Duniani) na UNHCR (Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi).
Mpango wa EU wa vituo vya nje Makubaliano hayo yanakuja miezi michache baada ya Tume ya Ulaya kupendekeza nchi wanachama wa EU kuanzisha vituo vya wahamiaji katika mataifa yasiyo wanachama wa Umoja huo mpango ambao bado unazua maswali kuhusu uhalali wake kisheria, hasa kwa Uholanzi.
Uhamiaji waendelea kuwa ajenda kuu kisiasa nchini Uholanzi mwezi ujao, kufuatia kusambaratika kwa serikali ya sasa ya mpito mwezi Juni kwa sababu ya mivutano ya kisera kuhusu uhamiaji.
Takwimu zinaonyesha kuwa mwaka 2024, Uholanzi ilipokea waomba hifadhi wapatao 32,175, idadi iliyo chini kwa asilimia 16 ikilinganishwa na mwaka 2023.
Tony Blair kuendesha mamlaka ya mpito ya Gaza – ripoti

Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza Sir Tony Blair ameshiriki majadiliano kuhusu uendeshaji wa mamlaka ya mpito ya Gaza endapo mpango wa kusitisha mapigano utafikiwa, BBC imedokezewa.
Sir Tony, ambaye aliingiza Uingereza katika Vita vya Iraq mwaka 2003, amefanya mazungumzo ya ngazi ya juu na pande zote ili kumaliza vita na ili kuangazia mustakabali wa baada ya mzozo wa eneo hilo la Palestina.
Kiini cha pendekezo la hivi punde – lililojadiliwa na Rais wa Marekani Donald Trump na viongozi wa Kiarabu katika Umoja wa Mataifa wiki hii – ni wazo la Gaza kuendeshwa kupitia mamlaka ya mpito itakayouungwa mkono na Umoja wa Mataifa na Ghuba, kabla ya kurejeshwa kwa udhibiti wa Palestina.
Mojawapo wa pendekezo linalosemekana kupata uungwaji mkono huko Washington ni kwa Sir Tony kuongoza mamlaka hiyo, ingawa ofisi yake imesema kuwa hataunga mkono mpango wowote utakaolenga kuwahamisha Wapalestina katika eneo la Gaza.
Kwanini Slovenia imeamua kumpiga marufuku Netanyahu kuingia nchini mwake?

Serikali ya Slovenia imeweka marufuku ya kusafiri dhidi ya Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, hatua iliyotangazwa rasmi siku ya Alhamisi kupitia taarifa ya serikali.
Hii inafuatia msimamo wa nchi hiyo kuhusu mzozo wa Palestina, ikiwa ni pamoja na kuitambua rasmi Palestina mwaka jana na kupiga marufuku mawaziri wawili wa mrengo mkali wa kulia wa Israel mwezi Julai.
Katibu wa Serikali katika Wizara ya Mambo ya Nje, Neva Grašič, alisema kupitia akaunti rasmi ya serikali katika mtandao wa X: “Kwa hatua hii, Slovenia inathibitisha dhamira yake kwa sheria za kimataifa, maadili ya msingi ya haki za binadamu, na sera ya nje yenye misimamo thabiti na ya kanuni.”
Slovenia, ambayo ni mwanachama wa Umoja wa Ulaya, tayari imechukua hatua kadhaa dhidi ya Israel.
Mwezi Agosti, iliweka vikwazo vya silaha na kupiga marufuku uagizaji wa bidhaa kutoka maeneo ya Palestina yanayokaliwa na Israel kinyume cha sheria za kimataifa.
Aidha, ilipitisha msaada wa ziada kwa watu wa Gaza.
Kuhusu Netanyahu, Grašič alisema kuwa serikali imechukua hatua hiyo kwa sababu anashutumiwa na Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ) kwa kutenda uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya ubinadamu huko Gaza.
“Umma unafahamu kuwa kuna mashauri yanayoendelea dhidi yake kwa tuhuma hizo,” aliongeza. “Kwa uamuzi huu, serikali inatuma ujumbe wazi kwa Israel: Slovenia inatarajia utii wa kweli wa maamuzi ya mahakama za kimataifa na sheria ya kimataifa ya kibinadamu.”
Slovenia imekuwa miongoni mwa mataifa ya Ulaya yaliyo mstari wa mbele kutaka kusitishwa kwa mapigano Gaza na kuongezwa kwa misaada ya kibinadamu kwa raia wa Palestina.
Mwezi Julai, serikali hiyo ilitangaza marufuku ya kuuza, kununua na kupitisha silaha kwenda au kutoka Israel, wiki mbili tu baada ya kumtangaza Waziri wa Usalama wa Taifa wa Israel, Itamar Ben-Gvir, na Waziri wa Fedha, Bezalel Smotrich, kuwa watu wasiotakiwa kuingia nchini humo, kutokana na matamshi yao ya “kuchochea mauaji ya halaiki” na vurugu dhidi ya Wapalestina.
Slovenia sasa inaendelea kuwa sauti yenye msimamo wa wazi katika kutetea haki za binadamu na sheria za kimataifa, hata inapokinzana na mataifa yenye nguvu duniani.
Trump atangaza ushuru mpya kwa bidhaa zinazoingia Marekani

Rais wa Marekani, Donald Trump, ametangaza ushuru mpya kwa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje, ikiwemo dawa na malori.
Ametangaza kuongeza ushuru hadi asilimia 100 kwa dawa zinazotengenezwa nje kwa kutumia leseni za kampuni za Kimarekani, au zile zinazozalishwa ndani ya Marekani lakini kuuzwa kwa majina tofauti.
Hatua hii itaanza kutekelezwa kuanzia Oktoba 1, isipokuwa kwa kampuni zitakazojenga viwanda vya uzalishaji ndani ya Marekani.
Aidha, serikali ya Marekani imeweka ushuru wa asilimia 25 kwa malori makubwa ya kubeba mizigo, huku ushuru kwa vifaa vya jikoni na vya bafuni ukiongezwa kwa asilimia 50.
Rais Trump amesema kuwa hatua hiyo inalenga kulinda masoko ya ndani.
“Bidhaa nyingi kutoka nje zinaingizwa kwa bei ya kutupwa nchini mwetu, hali ambayo imeyasukuma bidhaa za ndani nje ya soko,” alisema kupitia ukurasa wake wa Truth Social.
Hata hivyo, hatua hiyo imezua pingamizi kutoka kwa wafanyabiashara wa Marekani, ambao wametoa wito kwa Ikulu ya White House kusitisha ushuru huo wa ziada.
Israel yashambulia ngome za Wahouthi mjini Sanaa, yaua na kujeruhi kadhaa

Israel imetekeleza mashambulizi dhidi ya mji mkuu wa Yemen, Sanaa, siku ya Alhamisi, kwa mujibu wa vyombo vya habari vinavyohusiana na Wahouthi pamoja na Waziri wa Ulinzi wa Israel.
Mashambulizi hayo yamesababisha vifo na majeruhi kadhaa.
Mashambulizi hayo yanakuja siku moja baada ya watu kadhaa kujeruhiwa katika mji wa Eilat, Israel, siku ya Jumatano, kufuatia shambulizi la ndege zisizo tumia rubani lililodaiwa na kundi la Wahouthi.
Ofisi ya Waziri Mkuu wa Israel imeripoti kuwa Benjamin Netanyahu ndiye aliyeagiza shambulizi hilo dhidi ya Yemen siku ya Alhamisi, wakati akiwa safarini kuelekea New York.
Ofisi hiyo iliongeza kuwa Netanyahu alikuwa akipokea taarifa za moja kwa moja kuhusu operesheni hiyo kutoka kwa Waziri wake wa Ulinzi, Mkuu wa Majeshi, na Katibu wake wa Kijeshi.
Baadaye, kundi la Houthi Ansar Allah nchini Yemen lilitangaza kuzindua kombora la kisasa la kasi kubwa linaloitwa Palestine 2 kuelekea Israel, wakidai kuwa kombora hilo limesababisha kusitishwa kwa shughuli katika Uwanja wa Ndege wa Ben Gurion.
Televisheni ya Al Masirah, inayohusiana na Wahouthi, ilinukuu chanzo kutoka Idara ya Usalama na Ujasusi kikisema kuwa “uvamizi wa Israel dhidi ya Sanaa ulilengwa katika kituo cha marekebisho ya tabia (gereza) kinachosimamiwa na idara hiyo, ambacho kinahifadhi wafungwa na mahabusu.”
Hapo awali, kituo hicho cha habari kiliripoti kuhusu “uvamizi wa Israel unaolenga mji mkuu Sanaa,” uliotokea wakati huo huo na matangazo ya hotuba ya kila wiki ya kiongozi wa Wahouthi, Abdulmalik al-Houthi.
Mwandishi wa shirika la habari la AFP aliyepo Sanaa aliripoti kusikia milipuko mikubwa na kuona moshi ukipanda kutoka maeneo matatu tofauti ya jiji hilo.
Waziri wa Ulinzi wa Israel, Yisrael Katz, alituma ujumbe kupitia mtandao wa kijamii X akirejea tishio lake kwa Wahouthi, akisema: “Wahouthi, magaidi wa Yemen, wamekataa kujifunza kutoka Iran, Lebanon na Gaza sasa watalazimika kujifunza kwa njia ngumu.”
Aidha, alisisitiza kwamba, “yeyote anayehujumu Israel, atajibiwa kwa nguvu mara saba zaidi.”
Kwa upande wake, Meya wa Eilat, Eli Lankri, katika mahojiano na Kituo cha Televisheni cha 12 nchini Israel, alitoa wito wa “mashambulizi makali dhidi ya Wahouthi,” akibainisha kuwa “mashambulizi yao ya mara kwa mara yamevuruga shughuli katika bandari ya Eilat.”
Mwisho wa mwezi Agosti, shambulizi la anga la Israel lilimuua Waziri Mkuu wa Wahouthi, Ahmed Ghaleb al-Rahwi, pamoja na mawaziri na maafisa wengine tisa waliokuwa kwenye kikao mjini Sanaa.
Mapema mwezi Septemba, watu wasiopungua 46 waliuawa katika mashambulizi ya Israel yaliyolenga mji mkuu wa Yemen, Sanaa, na mkoa wa kaskazini wa Al-Jawf wakiwemo watu 38 waliouawa Sanaa ambapo vituo vya habari na taasisi zinazohusiana na Wahouthi vililengwa.
Mkurugenzi wa zamani wa FBI James Comey ashitakiwa

Aliyekuwa wa shirika la upelelezi la Marekani FBI James Comey ameshitakiwa kwa tuhuma za kutoa taarifa za uongo kwa Bunge la Marekani na kuzuia haki kutendeka.
Rais Trump alimfuta kazi Bwana Comey mnamo mwaka 2017,muda mfupi tu baada ya kuthibitika kuwa Rais huyo alikuwa anachunguzwa kuhusiana na madai kuwa Urusi iliingilia uchaguzi mkuu wa Marekani wa mwaka 2016.
Mwanasheria Mkuu wa Marekani Pam Bondi alisema katika taarifa kwamba hati ya mashtaka “inaonyesha dhamira ya Idara hii ya Haki ya kuwawajibisha wale wanaotumia vibaya nyadhifa zao kuwapotosha Warekani”.
Inaaminika kuwa mashitaka dhidi ya Comey yanahusiana na ushahidi alioutoa mbele ya kamati la Baraza la Seneti la masuala ya sheria ambapo alikanusha madai kuwa alifichua kwa vyombo vya habari taarifa nyeti kuhusu namna Urusi iliuingia uchaguzi wa Marekani.
Comey ni mkurugenzi wa kwanza wa zamani wa FBI kushtakiwa kwa uhalifu, ingawa anashikilia kuwa hajadanganya chini ya kiapo.
Ikiwa atapatikana na hatia, atakabiliwa na kifungwa cha hadi miaka mitano jela.
FIFA: Timu ya soka ya wanawake Afghanistan kucheza mechi za kimataifa kwa mara ya kwanza

Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) limetangaza kuwa timu ya wanawake wakimbizi kutoka Afghanistan itashiriki kwa mara ya kwanza katika mashindano ya kirafiki ya kimataifa yatakayofanyika mjini Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), kuanzia Oktoba 23 hadi 29, 2025.
Kwa mujibu wa taarifa ya FIFA, mashindano hayo ya kihistoria yajulikanayo kama “FIFA United” yatazikutanisha timu nne za wanawake: Afghanistan (wakimbizi), Chad, Libya na timu ya taifa ya UAE.
Rais wa FIFA, Gianni Infantino, amesema kuwa hatua hii inaonesha dhamira ya FIFA katika kuhakikisha wanawake na wasichana kote duniani wanapata haki ya kushiriki michezo, kutimiza ndoto zao za soka, na kuendeleza vipaji vyao kupitia michezo.
“Zaidi ya kuwa mashindano ya kirafiki, mechi hizi ni alama ya matumaini kwa wanawake duniani kote,” alisema Infantino.
Kwa upande wake, timu ya taifa ya wanawake ya Afghanistan imethibitisha taarifa hiyo kupitia tovuti yao rasmi na kuandika: “Kutoka uhamishoni, wachezaji wetu watashiriki mechi yao ya kwanza ya kirafiki ya kimataifa chini ya FIFA, kama ‘Timu ya Wanawake Wakimbizi wa Afghanistan’.”
Timu hiyo imetaja ushiriki huu kama “hatua muhimu kuelekea kutambuliwa rasmi”, hasa baada ya miaka ya kunyimwa nafasi ya kushiriki michezo tangu Taliban waliporejea madarakani mnamo 2021.
Mnamo Mei 2025, FIFA ilitoa ruhusa ya kuundwa rasmi kwa timu ya wanawake wa Afghanistan walioko uhamishoni, na kumteua Pauline Hamel, mwenye umri wa miaka 53, kuwa kocha mkuu wa timu hiyo.
Bi Hamel alielezea furaha yake akisema: “Tumepata fursa ya kufanya kazi nao na sasa tutaangalia kwa karibu maendeleo yao.”
Tangu kuingia kwa serikali ya Taliban, wanawake nchini Afghanistan wamezuiwa kushiriki michezo, elimu, ajira na shughuli nyingi za kijamii.
Hata hivyo, kupitia uhamishoni, timu hii sasa inapigania haki ya kushiriki mashindano ya kimataifa, ikiwemo Kombe la Dunia, na imetoa wito kwa wachezaji wa kike kote duniani kuunga mkono juhudi zao.
All Rights Reserved © The Cantona Group PLC||2025
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.