Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

Moto ulizuka katika jengo la ghorofa kubwa huko Boryspil, karibu na Kyiv, na kuharibu magari na nyumba za watu binafsi, na kumjeruhi mtu, waokoaji walisema awali.
Usiku wa kuamkia Jumatatu , vikosi vya Urusi viliishambulia Ukraine kwa ndege zisizo na rubani 141, zikiwemo takriban ndege 80 za aina ya Shahed kamikaze, Jeshi la anga la Ukraine liliripoti.
Jumla ya ndege 132 za UAV zilidunguliwa na kuzuiwa kaskazini, kusini, mashariki na katikati mwa nchi, huku ndege tisa zisizo na rubani zikipigwa katika maeneo saba, huku vifusi vikianguka, ilisema taarifa hiyo .
Aidha, kati ya saa kumi na saa kumi na mbili asubuhi, shambulio la anga lilifanywa “kwenye miundombinu ya jiji la Zaporizhzhia,” huku vifo vya raia vikiripotiwa, jeshi lilisema.
Mamlaka ziliripoti vifo vitatu huko Zaporizhzhia. Mikoa ya Kyiv na Sumy pia ilikumbwa na mashambulizi , mamlaka ilisema. Urusi haijazungumza lolote kuhusu mashambulizi hayo.
“Kwa bahati mbaya, muujiza haukutokea. Mara tu waokoaji walipotoa mwili wa mwanamke mwenye umri wa miaka 75 kutoka kwenye kifusi cha nyumba iliyoharibiwa,” Ivan Fedorov, mkuu wa Utawala wa Kijeshi wa Mkoa wa Zaporizhzhia, aliandika kwenye Telegram.
Korea Kusini itakubali mpango wa Trump na Kim wa kusimamisha mpango wa nyuklia, kwa sharti

Rais wa Korea Kusini amesema atakubaliana na makubaliano kati ya Donald Trump na Kim Jong Un ambapo Korea Kaskazini ilikubali kusimamisha uzalishaji wa silaha zake za nyuklia, badala ya kuziondoa.
Hii ni mara ya kwanza kwa Bwana Kim kusema anaridhia kufanya mazungumzo tangu mazungumzo ya viongozi hao wawili kuvunjika mwaka 2019.
Lee Jae Myung ameiambia BBC kuwa atakubali makubaliano na Korea Kaskazini ambapo Pyongyang itasitisha utengezaji wa silaha za kinyuklia kwa sasa badala ya kuziharibu kabisa.
Kutokana na shinikizo la Marekani la kuwepo mazungumzo kati ya nchi hizo mbili,kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un amesema yuko tayari kwa mazungumzo na Marekani ilimradi yasijikite katika sharti la nchi yake kuachana na mpango wake wa kinyuklia.Kauli hiyo ameitoa kwenye hotuba yake kwa bunge hapo jana Jumapili.
Kim amesisitiza kuwa zana zake za kinyuklia ni ulinzi dhidi ya kitisho kutoka kwa Korea Kusini na Marekani lakini amesema ana kumbukumbu nzuri za mkutano wake na Rais Trump ambaye amekutana naye mara tatu kipindi cha nyuma.Rais Trump mwezi uliopita alisema angependa kukutana na Kim katika siku za usoni.
Mazungumzo kati ya kima na Trump yalisambaratika mnamo 2019 baada ya Marekani kuitaka kuvunjilia mbali vituo vyake vya kinyuklia na badala yake iiondolee vikwazo.
Suala la Korea Kaskazini kuachana na mpango wa kinyuklia limekuwa mzozo wa muda mrefu kati yake na jirani yake Korea Kusini.
Licha ya Korea Kaskazini kuwekewa vikwazo chungunzima,kiongozi wake anasema vikwazo hivyo vimeisadia nchi yake kuwa imara zaidi,kujenga ustahimilivu na haiwezi kutetereka.Kim anasisitiza kuwa haiwezi kamwe kuacha kutengeza na kuimarisha silaha za kinyuklia.
Aidha Kim amesema hakuna sababu ya kuketi chini na kufanya mazungumzo na rais mpya wa Korea Kusini Lee Jae Myung akiongeza kuwa tayari amekwishaelezea bayana kuwa hawatashirikiana nao kwa lolote au kwa vyovyote vile. Lee anajaribu kutuliza uhasama kati ya nchi hizo mbili.
Rais Trump anatarajiwa kufanya ziara mwezi ujao kuelekea Seoul, Korea Kusini.
Pingamizi za Lissu zakwama, kesi ya uhaini iko pale pale

Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Dar es Salaam imetupilia mbali hoja zote za pingamizi la Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu kuhusiana na ubatili wa hati ya mashtaka.
Lissu, ambaye anakabiliwa na mashtaka ya uhaini, alidai kuwa hati ya mashtaka ni batili kwa kuwa haioneshi maelezo ya kosa wala nia ya kutenda kosa la uhaini ambayo ni viini muhimu katika hati ya mashtaka.
Kwa mujibu wa gazeti la Mwananchi, katika uamuzi uliotolewa leo Jumatatu, Septemba 22, 2025 uliosomwa na kiongozi wa jopo la majaji, Jaji Dunstan Ndunguru – imesema baada ya kupitia hati hiyo imeridhika ipo sahihi, kwani inatoa maelezo ya kosa kama sheria inavyoelekeza.
Pia, imeeleza kuhusu suala la nia ya kutenda kosa la uhaini hilo ni suala la ushahidi unaotarajiwa kuwasilishwa.
Kuhusu hoja kuwa maelezo ya mashahidi ni batili kutokana na kukiuka amri ya Mahakama Kuu ya kuwalinda mashahidi wa Jamhuri ambao ni raia, na maelezo ya askari Polisi kuchukuliwa kinyume na sheria, Mahakama imeeleza hoja hizo zinagusa mwenendo kabidhi (committal proceedings) suala ambalo ilishalitolea uamuzi.
Hivyo, Mahakama hiyo imehitimisha kuwa pingamizi la Lissu halina msingi na imelitupilia mbali na kesi ya uhaini itaendelea.
Riek Machar kufikishwa mahakamani Juba kujibu katika kesi inayoibua hofu ya kurejea kwa machafuko

Kesi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Sudan Kusini Dk. Riek Machar na viongozi saba waandamizi wa upinzani wa SPLM-IO imefunguliwa Jumatatu mjini Juba chini ya ulinzi mkali lakini iliahirishwa hadi Jumanne kufuatia mzozo juu ya mamlaka ya Mahakama Maalum.
Machar alifikishwa mahakaman pamoja na Waziri wa petroli aliyesimamishwa kazi Puot Kang Chol na washirika wengine wakuu. Wanakabiliwa na mashtaka ikiwa ni pamoja na uhaini, mauaji, kula njama, kufadhili ugaidi, na uhalifu dhidi ya ubinadamu, unaohusishwa na mapigano mnamo Machi katika Kaunti ya Nasir, Jimbo la Upper Nile, ambayo yaliua zaidi ya wanajeshi 250 na jenerali mwandamizi wa jeshi.
Upande wa utetezi, ukiongozwa na Dk. Garry Raymondo, ulipinga mamlaka ya mahakama hiyo na kusema kuwa inakiuka katiba ya mpito ya Sudan Kusini na Mkataba wa Amani Uliofufuliwa wa 2018. “Katiba ya Mahakama hii Maalum sio tu haina msingi wa mamlaka, lakini pia inaiweka Jamhuri ya Sudan Kusini katika ukiukaji wa wazi wa majukumu yake chini ya sheria za ndani na za kimataifa,”Dk.Raymondo aliiambia mahakama
Upande wa utetezi ulisema kuwa Dk. Machar hawezi kukabiliwa na mashtaka ya jinai akiwa ofisini bila idhini ya bunge, akitoa mfano wa ulinzi wa kikatiba.
“Vifungu vya 103 na 104 vya katiba ya mpito vinasema kwamba Makamu wa Kwanza wa Rais hatakabiliwa na kesi za jinai akiwa ofisini, isipokuwa baada ya kuondolewa kwa kinga na theluthi mbili ya wajumbe wote wa Bunge la Kitaifa,” upande wa utetezi ulisema.
Upande wa mashtaka unaoongozwa na wakili Ajo Ohisa ulitupilia mbali changamoto ya upande wa utetezi, ukisisitiza kuwa Mahakama Maalum ina mamlaka kamili ya kusikiliza kesi hiyo.
“Hoja ni dhaifu na haina msingi. Wajumbe wa Mahakama hii Maalum wote ni majaji wa Mahakama Kuu na kwa hivyo wana uwezo wa kusikiliza suala hilo. Hata kama mamlaka ya Mahakama Kuu yanatumika, Mahakama Kuu ina mamlaka yasiyo na kikomo, na uhalifu uliofanywa chini ya Sura ya 5 na 6 uko ndani ya uwezo wake, “Bw.Ohisa aliiambia mahakama.
” Kikao hiki sio kumondoa au kumshtaki Makamu wa Kwanza wa Rais. Hii ni kesi ya mahakama ndani ya uwezo wa mahakama ya Jamhuri ya Sudan Kusini. Haina uhusiano wowote na kuondolewa ofisini,” aliongeza
Usalama mjini Juba uliimarishwa wakati kesi ilipofunguliwa, huku askari wakipelekwa katika jiji lote kuwalinda wafungwa na kuzuia machafuko. Waangalizi wamesema uwepo mkubwa wa maafisa wa usalama ulichochea wasiwasi kati ya wakazi, na biashara zingine zimefungwa huku raia wengine wakiamua kukaa nyumbani
Majaji waliahirisha kesi hiyo hadi Jumanne, wakielekeza upande wa mashtaka kuwasilisha jibu la maandishi kwa pingamizi za mamlaka.
Mke wa Charlie Kirk amsamehe aliyemuua mumewe

Erica Kirk, mke wa mwanaharakati Charlie Kirk, ambaye aliuawa kwa kupigwa risasi, aliwaambia hadhira katika sherehe iliyohudhuriwa na makumi ya maelfu ya watu, akiwemo rais Donald Trump wa Marekani a watu wengine maarufu kama vile Elon Musk, kwamba aliongozwa na mafundisho ya Kikristo kumsamehe mtu huyo aliyemshambulia na kumuua mumewe.
Erica Kirk, ambaye ana shahada ya chuo kikuu ya theolojia na huendesha podcast inayohusu mafundisho ya Kikristo, alisema Jumapili, Septemba 21, baada ya kusoma vifungu kutoka katika Biblia, kwamba kama mumewe, Charlie Kirk, angekuwa hai, angekubaliana naye juu ya “kuwapenda maadui zetu na kuwapenda wale wanaotutesa.”
Baada ya ibada ya kidini ambayo ilikuwa sehemu kubwa ya sherehe ya kumkumbuka Charlie Kirk huko Arizona, Marekani na mwishoni mwa hotuba ya Erica Kirk, Donald Trump alipanda jukwaani na kuiambia hadhira, “Charlie bila shaka angejifunza fahari kubwa kuwasikia watu wakimpa Mungu utukufu leo.”
Aliongeza: “Tunahitaji kuirejesha dini nchini Marekani, na tunataka kumrejesha Mungu katika ardhi yetu nzuri kama ilivyokuwa hapo awali.”
Mhariri wa BBC wa Amerika Kaskazini, Sarah Smith, ambaye alihudhuria hafla hiyo, alisema misa hiyo ilikuwa zaidi kama mkutano wa kisiasa kuliko misa ya kumbukumbu ya msiba.
Mbali na Donald Trump, makamu wa rais wa Marekani, J.D. Vance, na viongozi wengine wakubwa Marekani walihudhuria tukio hilo.
Botswana yatangaza siku ya mapumziko kwa umma baada ya kupata medali ya dhahabu ya ‘kihistoria’

Botswana imetangaza sikukuu ya kusherehekea ushindi wa nchi hiyo katika mbio za mita 4×400 wanaume kwenye Mashindano ya Riadha ya Dunia mjini Tokyo, baada ya taifa hilo kuwa la kwanza la Afrika kushinda mashindano hayo.
Rais Duma Boko alipongeza medali ya dhahabu kama “ushindi wa kihistoria wa Afrika”, katika hotuba ya mtandaoni ya kusifu timu kwa namana walivyoshiriki.
Alitangaza Jumatatu, Septemba 29, kama sikukuu ya kusherehekea mafanikio hayo – siku moja kabla ya siku ya uhuru wa nchi.
Siku ya Jumapili, timu ya Botswana ya Lee Bhekempilo Eppie, Letsile Tebogo, Bayapo Ndori na Busang Collen Kebinatshipi waliishinda Marekani, ambao ni washindi wa mataji 10 ya mwisho ya dunia, katika mbio zilizokimbiwa huku mvua ikinyesha. Afrika Kusini ilishika nafasi ya tatu.
“Nitakuwa na uhakika wa kumwambia kila mtu, almasi ya asili ya Botswana sio tu ardhini, ni wanariadha wetu Bingwa wa Dunia,” rais alisema, akizungumza kutoka New York ambako anahudhuria kikao cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.
All Rights Reserved © The Cantona Group PLC||2025
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.