Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa
Mvutano ulipozuka kati ya wanamgambo wa Wazalendo na mamlaka mjini Kinshasa, hasa kuhusiana na uwepo wa Jenerali Olivier Gasita huko Uvira, wanamgambo hao wametuma risala kwa Rais Félix Tshisekedi. Ingawa wanathibitisha uaminifu wao kwa Kinshasa, wameweka masharti kwa uaminifu huu. Madai haya yanatia wasiwasi, kwani uwepo wao unavuka mstari wa mbele pamoja na vikosi vya jeshi vya DRC (FARDC) mashariki mwa nchi.

Madai yao sasa yamevuka masuala ya usalama. Katika risala yao kwa ujumbe wa serikali huko Uvira, Wazalendo waliweka masharti kadhaa. Kwanza, wanadai kupiga marufuku mienendo ya watu kutoka maeneo yaliyo chini ya udhibiti wa kundi la AFC/M23. Ombi lingine: kwamba maafisa waliotumwa Uvira waishi katika jiji hilo, na sio Bujumbura, mji mkuu wa jirani wa Burundi.
Na wanaenda mbali zaidi. Wanapendekeza kupeleka wanajeshi wao kwenye lango kuu la kuingilia mkoa wa Kivu Kusini, ili, wanasema, kulilinda vyema eneo hilo dhidi ya watu kujipenyeza.
Lakini matamanio yao yanavuka zaidi masuala ya kijeshi. Wanadai waweze kushiriki katika mazungumzo ya amani, ikiwa ni pamoja na mazungumzo ya Doha. Pia wanataka viongozi wao wa kisiasa kuunganishwa katika serikali—za kitaifa na mikoa—na katika taasisi na huduma za serikali na mashirika ya umma.
Ili kuhakikisha ufuatiliaji, wanaomba hata kuteuliwa kwa mshauri maalum anayehusika na masuala ya Wazalendo pekee katika ngazi ya taifa.
Hadi sasa, hakuna jibu lililotolewa kwa Barua hii. Mshauri wa karibu na Félix Tshisekedi ameieleza RFI kwamba madai haya lazima yashughulikiwe na kitengo cha RAD, ambacho ni muundo wa wanamgambo ulioundwa mnamo mwaka 2023 kusaidia FARDC na kusimamia Wazalendo. Shida ni kwamba muundo huu bado haujatumwa huko Uvira.
Kwa sababu hiyo, maelfu ya Wazalendo waliopo Kivu Kusini wanaendelea kutegemea viongozi wao wenyewe, ambao mara nyingi hawasiti kulikosoa jeshi la FARDC, ambapo hawajioni kama msaada wa moja kwa moja kwa jeshi hilo.
Ni nani hasa anayewatawala Wazalendo? Na uhamasishaji wao unaweza kufikia wapi? Swali hili ni kiini cha ripoti kadhaa zilizochapishwa katika wiki za hivi karibuni na mashirika yasiyo ya kiserikali na Umoja wa Mataifa. Wazalendo hawako tu mstari wa mbele pamoja na FARDC: wanapatikana pia katika miji na vijiji kadhaa chini ya udhibiti wa Kinshasa, kutoka Maniema kwenda Kivu Kaskazini, hadi Kivu Kusini. Katika mji wa Uvira, uwepo wao unadhihirika haswa. Hivi majuzi walipinga uwepo wa Jenerali Olivier Gasita, naibu kamanda wa kanda ya 33 ya kijeshi.
All Rights Reserved © The Cantona Group PLC||2025
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.