Marekani yatoa onyo kuhusu sheria mpya ya usalama wa mtandao ya Zambia

Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph

https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

.

Ubalozi wa Marekani nchini Zambia umewaonya raia wake kuwa waangalifu na sheria mpya “ya utata” ya usalama wa mtandao iliyoanzishwa katika nchi hiyo ya kusini mwa Afrika.

Ubalozi huo ulitoa tahadhari kuwaambia Wamarekani “waliopo au wanaopanga kuzuru Zambia kuhusu sheria mpya inayohitaji kuzuiliwa na ufuatiliaji wa mawasiliano yote ya kielektroniki nchini humo”.

Hii ni pamoja na simu, barua pepe, maandishi na maudhui yaliyopeperushwa hewani “nchi hiyo kuweza kuyafikia ikiwa yanajumuisha uwasilishaji wowote wa ‘taarifa muhimu,’ neno ambalo sheria inafafanua kwa upana kwamba linaweza kutumika kwa karibu shughuli yoyote”, ubalozi unasema.

Serikali ya Zambia ilisema sheria hiyo inahitajika ili kukabiliana na ulaghai mtandaoni na ponografia ya watoto, pamoja na kuenea kwa taarifa potofu.

Kufuatia tahadhari hiyo kutoka kwa ubalozi wa Marekani, wizara ya mambo ya nje ya Zambia ilitoa taarifa ikisema kwamba Sheria mpya ya Usalama wa Mtandao “haikusudiwa kuvamia usiri wa mtu yeyote” – iwe Wazambia au raia wa kigeni.

“Sheria hairuhusu ufuatiliaji wa watu wengi au bila mpangilio. Uingiliaji wowote au ombi la data linahitaji kibali kilichotolewa na mahakama,” ilisema.

Taarifa hiyo iliongeza kuwa “uainishaji wa ‘taarifa muhimu'” ulirejelea usalama wa taifa, “na tathmini au hatua zozote zinazochukuliwa hufanywa na taasisi zilizoidhinishwa, kulingana na utaratibu unaofaa”.

Kuna hofu kwamba sheria hiyo inaweza kutumika dhidi ya yeyote anayeikosoa serikali, haswa wakati uchaguzi unakaribia mwaka ujao.

All Rights Reserved © The Cantona Group PLC||2025


Discover more from cantonadigital

Subscribe to get the latest posts sent to your email.

Leave a comment