Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

Karibu katika Matangazo yetu ya jioni moja kwa moja kutoka Communication Center. Tumekuandalia mengi ikiwa ni pamoja
Muhtasari
- Mlipuko wa ugonjwa DR Congo huenda ulisababishwa na malaria
- Fury na Usyk waangaliana kwa dakika 11 baada ya kukutanishwa kabla ya pigano lao wikendi
- Usiwadharau wanajeshi wa Korea Kaskazini walioko Urusi
- Kiongozi wa waasi wa Syria apinga mjadala kuhusu kupiga picha na mwanamke
- Norway yatuma mfumo wa Ulinzi wa anga na wanajeshi karibu na mpaka na Ukraine – Kunani?
Naam,Natumai U buheri wa afya popote pale ulipo duniani kwa mwoyo mkunjufu na mikono miwili Hujambo na karibu katika matangazo yetu Afrika Leo Mchana ya moja kwa moja ikiwa ni tarehe 20/12/2024 Jina langu ni Cantona Joseph,karibu.
Mlipuko wa ugonjwa DR Congo huenda ulisababishwa na malaria

Malaria imetambuliwa kama sababu inayowezekana ya ugonjwa ambao umeua zaidi ya watu 80 kusini-magharibi mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, shirika kuu la afya la Afrika lilisema.
Waathiriwa wa ugonjwa ambao haukujulikana hapo awali walikuwa wakiugua dalili kama za mafua kama vile homa, maumivu ya kichwa, shida ya kupumua na anemia.
Sampuli nyingi ambazo zimejaribiwa zilionyesha kuwa wana malaria – ambayo husababishwa na vimelea vinavyobebwa na mbu na ni janga katika ukanda huo – huku utapiamlo ukiendelea kuzidisha hali hiyo kuwa mbaya zaidi.
Hata hivyo wataalam wa afya hawaondoi uwezekano wa sababi zingine katika eneo la afya la Panzi.
Wasiwasi kuhusu ugonjwa huo umeongezeka kufuatia kifo cha mgonjwa wa kiume aliyekuwa akionyesha dalili zinazohusiana na homa ya kuvuja damu.
Hii ilisababisha uvumi kuhusu uwezekano wa maambukizi ya virusi kuanzia wakati huo huo kama malaria, Dk Ngashi Ngongo, kutoka Vituo vya Afrika vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Africa CDC), aliwaambia waandishi wa habari siku ya Alhamisi.
Sampuli za mgonjwa aliyefariki zimetumwa katika mji mkuu wa Kongo, Kinshasa, kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi, huku matokeo yakitarajiwa ndani ya wiki ijayo.
Afrika CDC, Shirika la Afya Duniani la Umoja wa Mataifa, na mashirika mengine yanazidisha uchunguzi kuhusu mlipuko huo, huku majaribio zaidi yakiendelea.
Fury na Usyk waangaliana kwa dakika 11 baada ya kukutanishwa kabla ya pigano lao wikendi

Tyson Fury na Oleksandr Usyk waangaliana ana kwa ana kwa kwa dakika 11 na sekunde 20 katika moja ya tukio la kipekee, pengine refu zaidi katika historia ya ndondi.
Briton Fury, 36, atakutana ulingoni kuwania taji la uzito wa juu la Usyk nchini Saudi Arabia Jumamosi.
Akizungumza katika mkutano wa wanahabari, Usyk alisema: “Mimi? [Niangalie kando?] Hapana.”
Hakuna kati yao aliyekuwa na la kusema katika mkutano wa wanahabari wa Alhamisi, wote wakisisitiza muda wa mazungumzo umepita.
Fury na Usyk waliangaliana kwa ghadhabu na wote walikataa kuangalia kando.
Dakika chache baadaye, waandaaji walianza kupanga mpango wa kuwatenganisha wawili hao. Rais wa WBC Mauricio Sulaiman alikuwa wa kwanza kujaribu kuwashawishi, lakini hakuna mpiganaji aliyewatazama.
Kipande cha kadi na leso kiliwekwa kati yao.
Jasho lilimtiririka Fury huku wapiganaji hao wakianza kurushiana maneno.
“Ni wakati wa sungura sasa. Kuchinjwa. Kukatwa vipande vipande,” Fury alimwambia Usyk.
“Usiogope,” Usyk alijibu.
Mnamo mwezi Mei, Usyk mwenye umri wa miaka 37 alimshinda Fury na kuwa bingwa wa kwanza wa uzani wa juu bila kupingwa katika kipindi cha miaka 25.
Usiwadharau wanajeshi wa Korea Kaskazini walioko Urusi – wanajeshi wa zamani waliambia BBC

Wanajeshi na wataalam wengine wa Korea Kaskazini waliotumwa Ukraine kusaidiana na vikosi vya Urusi vitani hawapaswi kudharauliwa, wamesema wanajeshi wa zamani.
Kulingana na ujasusi wa Korea Kusini, wengi wao ni wa kitengo cha wasomi wa Storm Corps, na “wana ari ya juu”, lakini “hawana ufahamu wa vita vya kisasa”.
Mwasi Lee Hyun Seung, alifundisha kikosi maalum cha Korea Kaskazini mapema miaka ya 2000 kabla ya kuasi mwaka 2014.
‘’Niliwafundisha sanaa ya kijeshi, jinsi ya kurusha visu na kutengeneza silaha kwa vipandikizi na vyombo vingine vya jikoni’’, amesema.
Lakini ingawa mafunzo ya kikosi cha Storm Corps ni ya hali ya juu zaidi kuliko yale ya vikosi vya kawaida vya Korea Kaskazini, wanajeshi hao hawapati chakula cha kutosha na isitoshe wana utapiamlo.
Haneul ambaye ni mwanajeshi wa zamani wa Korea Kaskazini, anachokumbuka zaidi kuhusu wakati wake katika jeshi la Korea Kaskazini ni njaa ya kila siku.
Alipoteza kilo 10 katika mwezi wake wa kwanza wa huduma, kwa sababu ya lishe ya mahindi na kabichi kila siku.
Miezi mitatu ya mafunzo, anasema karibu kikosi chake kizima kilikuwa na utapiamlo na walihitaji kupelekwa kwenye kituo cha matibabu ili kuongeza uzito.
Baadaye walipowekwa kama walinzi vitani kwenye mpaka na Korea Kusini, mchele ulichukua nafasi ya mahindi. Lakini ilipofika mabakuli yao, kiasi kikubwa ulikuwa ushaliwa na vitengo vya nyuma, na uliobaki mara nyingi ulikuwa na mchanga.
Haneul anasema kitengo chake kilikuwa miongoni mwa waliolishwa vyema zaidi, kama mbinu ya kuwazuia kuhamia Korea Kusini. Lakini ilishindikana kumzuia Haneul.
Mnamo mwaka wa 2012, alifunga safari ambayo iwapo angekamatwa adhabu yake ingekuwa kifo katika eneo lisilo na kijeshi (DMZ) – ukanda wa ardhi unaogawanya Kaskazini na Kusini.
Uzoefu wake na wa waasi wengine wa kijeshi unasaidia kutoa mwanga kuhusu hali ya maelfu ya wanajeshi wa Korea Kaskazini waliowekwa mstari wa mbele katika vita vya Urusi dhidi ya Ukraine.
Pyongyang imeripotiwa kutuma karibu wanajeshi 11,000 kusaidia vikosi vya Urusi kurudisha sehemu ya eneo lake la Kursk lililotekwa na Ukraine katika shambulio la majira ya joto.
Mapema wiki hii, Seoul, Washington na Kyiv walisema “idadi kubwa” ya wanajeshi hao sasa wameingia kwenye mapigano, na kuripoti majeruhi wa kwanza, huku maafisa wa Korea Kusini wakikadiria zaidi ya 100 tayari wameuawa na wengine kujeruhiwa. Takwimu hii haijathibitishwa.
Kiongozi wa waasi wa Syria apinga mjadala kuhusu kupiga picha na mwanamke

Kiongozi wa waasi nchini Syria, Ahmed al-Sharaa, ametupilia mbali mabishano ya mtandaoni kuhusu video zinazomuonyesha akimpa ishara msichana ili afunike nywele zake kabla ya kupiga naye picha wiki iliyopita.
Tukio hilo lilizua ukosoaji kutoka kwa wachambuzi wasio na misimamo mikali na wahafidhina huku kukiwa na uvumi kuhusu mwelekeo wa siku za usoni baada ya waasi kuingia madarakani.
Wanaopendelea mabadiliko waliona ombi hilo kutoka kwa mkuu wa kundi la waislamu wa Sunni Hayat Tahrir al-Sham (HTS) kama ishara kwamba anaweza kutaka kutekeleza mfumo wa Kiislamu nchini Syria baada ya kuongoza kupinduliwa kwa Bashar al-Assad, huku wahafidhina wenye misimamo mikali wakimkosoa kwa kukubali kupigwa picha na mwanamke huyo.
“Sikumlazimisha. Lakini ni uhuru wangu binafsi. Nataka nipigwe picha jinsi inavyonifaa,” Sharaa alisema katika mahojiano na mwandishi wa BBC Jeremy Bowen .
Mwanamke huyo, Lea Kheirallah, pia amesema kwamba hakuona ubaya wowote wa ombi hilo.
Hata hivyo, tukio hilo lilionyesha baadhi ya matatizo ambayo kiongozi yeyote wa baadaye wa Syria anaweza kuwa nayo katika kuomba na kuunganisha nchi hiyo yenye dini tofauti.
Waislamu wa madhehebu ya Sunni ndio idadi kubwa ya watu, na waliobaki wamegawanyika kati ya Wakristo, Alawites, Druze na Ismailis.
Norway yatuma mfumo wa Ulinzi wa anga na wanajeshi karibu na mpaka na Ukraine – Kunani?

Wizara ya Ulinzi ya Poland imesema mfumo wa ulinzi wa anga wa NASAMS na wanajeshi 100 wa Norway wamewasili kama sehemu ya ujumbe wa NATO kulinda kituo cha anga cha Rzeszow karibu na mpaka wa Ukraine.
Ujumbe uliotumwa kwenye mtandao wa X ambao (zamani ulijulikana kama Twitter) ulisema kuwa Rzeszow, kituo kikuu cha usafirishaji ambacho nchi za Magharibi hutumia kutuma msaada wa kijeshi kwa Ukraine, pia kitalindwa na wapiganaji wa F-35.
Misheni hiyo inatarajiwa kudumu hadi kipindi cha Pasaka, idara ya jeshi la Poland ilisema.
Mfumo wa hali ya juu wa ulinzi wa anga wa Norway umewekwa kuzuia makombora yanayorushwa kwa umbali mdogo na wa kati katika hali zote za hali ya hewa.
Mfumo huo ulitengenezwa na kampuni ya Norway ya Kongsberg pamoja na kampuni ya Marekani ya Raytheon na tayari unatumiwa na jeshi la Ukraine.
Ukraine imekuwa ikitoa wito kwa washirika wake wa Magharibi kuangusha makombora na ndege zisizo na rubani za Urusi ikiwa zitaruka juu ya eneo la NATO (siku za nyuma zilipita juu ya anga ya Poland na Romania) au hata karibu na mipaka ya magharibi ya Ukraine.
KIPENGA CHA MICHEZO
‘Barca walimuachia vipi?’ Kutana na ‘nyota’ wa siku zijazo wa Chelsea mwenye umri wa miaka 18

Saa 2 zilizopita
Kwa vyovyote si chipukizi pekee wa Chelsea aliyevutia macho kwenye Ligi ya Conference League, lakini Marc Guiu lilikuwa jina kwenye midomo ya kila mtu baada ya ushindi wa hivi punde wa The Blues katika shindano hilo.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 18 ndiye aliyekuwa kinara katika ushindi wa 5-1 wa The Blues dhidi ya Shamrock Rovers siku ya Alhamisi, akifunga hat-trick katika kipindi cha kwanza na kusaidia timu ya Enzo Maresca kuongoza awamu ya ligi na kudumisha rekodi yao isiyo na dosari katika mashindano hayo.
Guiu alitumia vibaya mpira wa kichwa wa Darragh Burns na kufungua bao la kwanza kabla ya kushika pasi ya nyuma ya Daniel Cleary na kumalizia kutoka eneo lenye kona kali zaidi kwa bao lake la pili, ambalo lilirejesha uongozi wa Chelsea baada ya Markus Poom kusawazisha.
Na chipukizi huyo alikamilisha bao lake la tatu katika muda wa dakika za lala salama, akimalizia krosi sahihi ya Noni Madueke na kuongoza mpira wa kichwa hadi kona ya mbali kwa bao lake la awamu ya sita la ligi – zaidi ya mchezaji mwingine yeyote kwenye shindano hilo.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Kihispania, ambaye alijiunga na Chelsea kutoka Barcelona majira ya joto, nafasi yake ilichukuliwa na Joao Felix – lakini bila shaka huu ulikuwa usiku wa Guiu.
“Wazo langu na Guiu ni je, Barcelona wamemuacha vipi?” kiungo wa zamani wa Chelsea Joe Cole aliambia TNT Sports. “kijana huyu – katika muda wa miaka miwili – anaweza kuwa nambari tisa.”
“Nadhani Barcelona wamefanya makosa.”
Guiu ni nani na kwanini Barca walimwachia kuondoka?
Kusema kwamba Guiu aliondoka baada ya kujiunga na kikosi cha kwanza Barcelona itakuwa ni upuuzi.
Mwanafunzi huyo wa La Masia alionyesha mchango wao mara moja kunako dakika ya 79 katika mechi ya Barcelona ya La Liga dhidi ya Athletic Bilbao Oktoba 2023, akifunga sekunde 33 tu baadaye na kuipatia timu ya Xavi ushindi wa 1-0.
Njia yake ya kujiunga na kikosi cha kwanza haikuwa moja kwa moja kinda huyo hakuanzishwa mara kwa mara nyakati zake akiichezea timu ya vijana.
“Alikosa michezo mingi,” Albert Capellas, mkurugenzi msaidizi wa zamani wa Barcelona wa soka la vijana, aliambia Sky Sports mapema mwaka huu. “Hakuweza kuushiriki mazoezi.
“Kinachotokea katika vilabu vingi, kama huwezi kufanya mazoezi au kucheza, lazima uondoke. [Lakini] Barcelona, tunajua kiwango cha wachezaji, tunawapa muda.”
Subira ya klabu ya Kikatalani ilimsaidia Guiu. Alicheza mechi sita zaidi kwa timu ya wakubwa mwaka 2023-24, akifunga tena katika kichapo cha 3-2 kutoka kwa Royal Antwerp kwenye Ligi ya Mabingwa.
“Marc Guiu ni mfungaji,” aliongeza Capellas. “[Yeye] si mchezaji ambaye ana ujuzi wa ajabu ikija sulala la mmoja dhidi ya mmoja, ambaye anaweza kuwapiga chenga wachezaji. Ni aina nyingine ya mchezaji, lakini ni wa kipekee katika nafasi yake. Ana uwezo wa kufunga mabao.”
Barcelona wanaaminika kujaribu kuondoa kipengele cha Guiu cha pauni milioni 5 cha kutolewa kwenye kandarasi yake kwa kumuongezea muda, lakini Chelsea waliamirisha kipengele hicho mwezi Juni kabla ya kumsaini kinda huyo kwa mkataba wa miaka mitano, huku kukiwa na chaguo la mwaka mmoja zaidi uwanjani Stamford Bridge. .
‘Namfananisha na Suarez’
Guiu anaweza kuwa alipewa msaada wa mabao yake mawili kati ya matatu dhidi ya Shamrock Rovers, lakini alionyesha umahiri wake wa kuwa mshambuliaji mwenye uzoefu kwa kutumia makosa ya upinzani kama fursa katika kipindi cha kwanza.
Bao lake la tatu – mpira wa kichwa kutoka kwa Madueke – halikuweza kuzuilika .
“Lilikuwa bao la ujasiri,” Cole alisema, akitafakari juu ya mataji matatu ya kinda huyo mwenye umri wa miaka 18. “Ninamfananisha na [mshambulizi wa zamani wa Barcelona, Liverpool na Uruguay] Luis Suarez.
“Sisemi kuwa yeye ni Suarez kwa sasa, lakini ana uwezo wa ushujaa huo.
“Kijana huyo anaweza kufunga mabao. Anaweza kuwa nyota mkubwa wa klabu hii.”
Kiernan Dewsbury-Hall, mfungaji wa bao la tatu la Chelsea, alimsifu mchezaji mwenzake.
“Sijawahi kuona mtu akitoa shinikizo kama yeye,” alisema. “Yeye kamwe hupunguzi kasi yake.”
Je, ni lini atapata fursa ya kushiriki katika ligi ya Premier?
Licha ya kushiriki mechi zote za Ligi ya Conference ya Chelsea msimu huu – ikiwa ni pamoja na mchujo wa kufuzu dhidi ya Servette – nafasi za Guiu zimekuwa finyu katika ligi ya Premia.
Hajacheza Ligi ya Premia tangu The Blues walipofungwa 2-0 na mabingwa Manchester City katika mchezo wao wa ufunguzi, alipochukua nafasi ya Nicolas Jackson aliyejeruhiwa.
Alikuwa mbadala wa kipindi cha pili katika ushindi wa 5-0 wa The Blues wa 5-0 Kombe la Carabao dhidi ya Barrow – lakini kutolewa kwao raundi ya nne mikononi mwa Newcastle kulimnyima Guiu fursa zaidi za kuonesha kiwango kizuri katika mchuano huo.
Imekuwa hadithi tofauti barani Ulaya, hata hivyo, Guiu akiweka wastani wa bao kila baada ya dakika 47 katika awamu ya Ligi ya Conference – ambayo rekodi bora zaidi katika mashindano.
Mabao yake sita yametokana na mikwaju 19, na kumfanya abadilike kwa asilimia 32%.
Kiwango kizuri cha Jackson katika Ligi Kuu ya Uingereza na uchezaji wa mabao wa Christopher Nkunku kwenye Ligi ya Conference huenda vilichelewesha ufanisi mzuri wa kikosi cha kwanza, lakini Maresca alipendekeza kuwa ni suala la muda tu kabla ya kijana huyo kupewa nafasi ya kuangaza zaidi mara kwa mara.
“Hana raha kwani Nicolas na Christopher wanaendelea vyema,” Muitaliano huyo alisema baada ya ushindi wa Alhamisi.
“Unapokuwa na miaka tisa na wengine tisa wanafanya vizuri, ni suala la kuhojiwa. Ni muhimu wafanye kazi kwa bidii siku baada ya siku.
KOMBE LA CARABAO.



Timu ya Manchester United imeondolewa kwenye michuano ya Carabao Cup baada ya kushindwa na Tottenham Hotspur kwa mabao 4-3 katika mechi ya robo fainali iliyochezwa katika uwanja wa Tottenham Hotspur.
Tottenham sasa itakutana na Liverpool katika hatua ya nusu fainali, huku Arsenal ikipangiwa kuchuana na Newcastle.
All Rights Reserved © Cantona Group PLC||2024
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.