Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa
Rais William Ruto ametembelea mtangulizi wake Uhuru Kenyatta nyumbani kwa familia yake huko Gatundu, ikiwa ni maongezi ya kwanza ya moja kwa moja tangu mzozo kati yao, wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita.

Katika ziara hiyo, Rais Ruto alimpongeza Rais mstaafu Kenyatta kwa umahiri wake wa ajabu katika kusimamia mchakato wa kukabidhi mamlaka kwa amani baada ya uchaguzi mkuu wa 2022.
Kulingana na taarifa ya ikulu ya Nairobi, miongoni mwa maswala waliyozungumzia ni pamoja na athari za kutatiza za COVID-19, vita vinavyoendelea nchini Ukraine, changamoto za kuyumba kwa soko la sarafu na hali mbaya ya uchumi.

Kwa upande wa utawala, viongozi hao wawili walisisitiza umuhimu wa kufikia maelewano mapana ya kisiasa ili kuharakisha ukuaji wa umoja na kufikia malengo ya maendeleo ya nchi.
Katika maswala ya kikanda, Rais Ruto na mtangulizi wake walithibitisha tena jukumu la Kenya kama Mlinda amani mkuu katika eneo la Afrika Mashariki.

Pia walionyesha uungaji mkono kwa Raila Odinga kuwania nafasi ya Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika, wakihimiza Wakenya na washirika wa kimataifa kumuunga mkono.
Mkutano kati ya wawili hawa umefanyika wakati huu wakenya wanaendelea kulalamikia maswala kadhaa ikiwemo kudorora kwa uchumi na kutokuwepo kwa tume ya uchaguzi.

Mkutano wa wawili hawa umejiri siku chache baada ya aliyekua naibu wa Rais Rigathi Gachagua kuondolewa madarakani.
All Rights Reserved © Cantona Group PLC||2024
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.