Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa
Shirika la Mpango wa Chakula Duniani limetangaza kukosa fedha za kuwasaidia watu milioni 26 wanaokabiliwa na ukame kusini mwa Afrika, pamoja na visa milioni 25.6 vya utapiamlo nchini DRC.

Wakati wa mkutano na waandishi wa habari mjini Johannesburg, Afrika Kusini, mkurugenzi wa WFP nchini Msumbiji, Antonella d’Aprile, ameonya juu ya kuongezeka mno kwa utapiamlo, akitaka msaada wa haraka kwa sababu, amebainisha, msaada huu “hauwezi kusubiri”. Nchi zilizoathirika zaidi na uhaba wa chakula kutokana na ukame ni pamoja na Angola, Malawi, Msumbiji, Namibia, Zambia na Zimbabwe.
Umoja wa Mataifa umetoa picha mbaya ya mazingira ya kilimo nchini Msumbiji, ukielezea hali “mbaya” yenye msururu wa “mashamba tupu” nchini kote na kutaja familia ambazo “hazina chochote cha kula”.
Mwakilishi wa WFP nchini Malawi Paul Turnbull anasema “karibu nusu ya mavuno ya mahindi yaliharibiwa na ukame uliosababishwa na El Nino mapema mwaka huu.” Ametoa mfano wa visa vya watoto kufukuzwa shuleni ili kusaidia familia zao kifedha.
Kuhusu mwakilishi wa WFP nchini Zambia, Cissy Kabasuuga, anabaini kwamba nchi hii, inayochukuliwa kuwa “kapu la chakula kusini mwa Afrika“, “iko kwenye hatihati ya mgogoro wa chakula”.
DRC bado iko kwenye mstari mwekundu
Nje ya Kusini mwa Afrika, robo ya wakazi wanaendelea kukabiliwa na utapiamlo katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, imetahadharisha WFP, kupitia mwakilishi wake nchini humo, Peter Musoko, akisikitika pia kutoona maendeleo yoyote. Bw. Musoko amekumbusha kuwa hali hii inatokana na mambo kadhaa, hususan migogoro ya silaha na baina ya jamii, hatari za hali ya hewa na magonjwa ya milipuko ya ndui, kipindupindu na surua.
Tarehe 21 Novemba, WFP ilitoa ripoti kuhusu usalama wa chakula, ikifichua kuwa watu milioni 25.6 wanakabiliwa na uhaba wa chakula katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Hali katika mikoa ya Ituri, Kivu Kaskazini na Kivu Kusini imezorota kutokana na migogoro ya silaha, huku Tanganyika ikiwa ni mkoa ulioathiriwa zaidi na uhaba wa chakula, kutokana na mafuriko makubwa.
“Mwaka 2025, ni lazima tufanye kazi zaidi juu ya ustahimilivu na kuimarisha mifumo ya chakula nchini DRC ili kusaidia familia kuepuka njaa,” Peter Musoko alisema wakati huo. Mwakilishi wa WFP katika nchi hii kubwa aliongeza: “Katika hali tete kama hii, gharama ya kutochukua hatua ni jambo lisilofikirika. Kwa pamoja, lazima tushirikiane na serikali na jumuiya ya kibinadamu kuongeza rasilimali kwa mgogoro huu uliopuuzwa.”
WFP ambayo inakbainisha kuwa DRC ina ardhi yenye rutuba na rasilimali nyingi za maji, WFP imeielezea kukosekana kwa uwekezaji katika maendeleo ya vijijini, na hivyo kuzuia nchi hiyo kufikia kujitosheleza kwa chakula.
All Rights Reserved © Cantona Group PLC||2024
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.