Afrika Leo Jioni

Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph

https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

Karibu katika Matangazo yetu ya jioni moja kwa moja kutoka Communication Center. Tumekuandalia mengi ikiwa ni pamoja

Muhtasari

  • Balozi wa Marekani nchini Kenya Meg Whitman ajiuzulu
  • Trump amemteua Pete Hegseth kama Waziri wa Ulinzi
  • Rais wa shisikisho la soka Afrika Kusini akamatwa kwa tuhuma za ulaghai
  • Tamisemi kuzingatia rai ya Chama Cha Mapinduzi kuhusu uenguliwaji
  • Israel na Gaza Marekani yasema Israel haijakiuka sheria yake kuhusu kuzuia misaada huko Gaza
  • Uganda Watumiaji wa TikTok wafungwa Uganda kwa kuitusi familia ya rais
  • Kanisa Uingereza Askofu Mkuu wa Canterbury ajiuzulu kwa kashfa ya unyanyasaji iliyokumba Kanisa
  • Tanzania Polisi Tanzania yachunguza picha za watu wakimkamata mfanyabiashara kwa nguvu
  • Elon Musk Musk apata kazi aliyoahidiwa baada ya kumuunga mkono Trump
  • Israel na Iran Netanyahu azungumzia “kuharibu uchumi wa Iran”
  • Mashambulizi Lebanon Watu 23 wauawa kutokana na mashambulizi ya Israel nchini Lebanon, wizara yaasema

Naam,Natumai U buheri wa afya popote pale ulipo duniani kwa mwoyo mkunjufu na mikono miwili Hujambo na karibu katika matangazo yetu Afrika Leo Jioni ya moja kwa moja ikiwa ni tarehe 13-11-2024

Marekani yafungua kituo cha makombora kaskazini mwa Poland

TH

Marekani inafungua kambi mpya ya makombora kaskazini mwa Poland, ambayo Kremlin iliikosoa kama jaribio la “kuidhibiti” Urusi kwa kusogeza miundombinu ya kijeshi ya Marekani karibu na mipaka yake.

Iko katika mji wa Redzikowo karibu na pwani ya Baltic, kituo kikuu kitakachozinduliwa rasmi siku ya Jumatano kimekuwa kikifanya kazi tangu miaka ya 2000.

Wakati Poland inataka kuwahakikishia raia wake juu ya dhamira ya NATO kwa usalama wao kufuatia ushindi wa rais wa Donald Trump, ilisema msingi huo unaonyesha kuwa muungano wake wa kijeshi na Washington unabaki thabiti, yeyote ambaye yuko katika Ikulu ya White House.

Kambi hiyo iko kama kilomita 250 (maili 155) kutoka kwa eneo la Urusi la Kaliningrad.

“Ilichukua muda, lakini ujenzi huu unathibitisha azimio la kijiografia la Marekani,” Waziri wa Mambo ya Nje wa Poland Radoslaw Sikorski alisema katika video iliyowekwa kwenye mtandao wa kijamii la X siku ya Jumanne.

Rais wa Poland Andrzej Duda, mwanahafidhina ambaye amesisitiza uhusiano wake mzuri na Trump, alitarajiwa kuhudhuria sherehe za ufunguzi pamoja na wawakilishi wa NATO.

Kremlin ilisema kutumwa kwa mfumo wa ulinzi wa makombora nchini Poland kulionyesha “miundombinu ya kijeshi ya Marekani inasonga mbele kuelekea mipaka yetu” kama “sehemu ya jaribio la kuidhibiti kijeshi”.

Msemaji wa Kremlin Dmitry Peskov alionya Jumatano kwamba Urusi itachukua hatua za kuhakikisha “usawa” katika kujibu, lakini hakutaja itakuwa hatua gani .

Balozi wa Marekani nchini Kenya Meg Whitman ajiuzulu

th

Balozi wa Marekani nchini Kenya Meg Whitman amewasilisha barua yake ya kujiuzulu kwa Rais Joe Biden; Balozi Mdogo Marc Dillard atasimamia ubalozi huo.

Katika taarifa iliyotumwa kwa vyombo vya habari ,Whitman amesema iekuwa fahari yake kuhudumu katika nafasi hiyo nchini Kenya na kumshukuru rais Biden kwa kumpa fursa hiyo .

Balozi huyo maajuzi amekuwa akizungumziwa mitandaoni nchini Kenya baada ya baadhi ya Wakenya katika mtandao wa X kumtaka ajiuzulu kwa madai ya kuwa na ushirikiano wa karibu na utawala wa Rais William Ruto wakidai kwamba hakuwa akiiwajibisha serikali ya Kenya ipasavyo katika kulaani matukio ya utekaji nyara na mauaji ya watu nchini .

Whitman katika taarifa yake amesema amefanikiwa kuendeleza miradi ya manufaa kwa Kenya na Marekani ikiwemo vita dhidi ya ugonjwa wa Mpox na kuleta wawekezaji wa Marekani kuja nchini Kenya.

Trump amemteua Pete Hegseth kama Waziri wa Ulinzi

xx

Rais mteule wa Marekani, Donald Trump, amemteua Pete Hegseth, mtangazaji wa Fox News na mstaafu wa kijeshi, kuwa waziri wake mpya wa ulinzi.

Hegseth, aliyehudumu katika vita vya Afghanistan na Iraq, atakuwa na jukumu la kusimamia jeshi la Marekani.

Trump alimtaja Hegseth mwenye umri wa miaka 44 kama mtu “mwenye nguvu, mwenye akili, na mzalendo wa kweli wa Marekani.

”Uteuzi huu ulitangazwa siku moja baada ya Trump kutangaza bwenyenye wa dunia Elon Musk kupewa nafasi ya kusimamia kupunguza gharama serikalini.

Hegseth ni miongoni mwa walioteuliwa kwa nyadhifa muhimu za usalama, ikiwa ni pamoja na John Ratcliffe kama mkuu wa kitengo cha ujasusi cha CIA.

Ikiwa ataidhinishwa na Seneti ya marekani, Hegseth atakutana na changamoto za kufanya maamuzi kuhusu masuala ya msaada wa kijeshi kwa Israel na Ukraine.

Trump anataka Marekani ijiondoe katika migogoro ya kigeni. Alikosoa utawala wa rais wa Marekani anayeondoka Joe Biden kwa matumizi ya fedha kusaidia Ukraine katika vita vyake na Urusi.

Hii leo seneti la Republican inatarajiwa kuchagua kiongozi mpya ,siku ambayo Trump anatarajiwa kukutana na rais anayeondoka ,Joe Biden,katika ikulu ya White house kama sehemu ya kupokezana mamlaka ya kiongozi wa nchi.

Pete Hegseth ni nani?

Ni mzaliwa wa Minneapolis,Eneo la ,Minnesota na amehitimu shahada katika chuo cha ivy League na awali amekuwa mtangazaji wa habari za kihafidhina .Na ameripoti masuala ya haki za wanajeshi katika runinga ya habari ya fox,na kumpa ushawishi kwa masuala yanayofungamana na hayo.

Pia rais mteule aligusia utendakazi wa Hegseth kama mwandishi mahiri akitaja kitabu chake cha “The War on Warrior”ambacho kinadhihirisha usaliti unaokumba wanajeshi na sasa kuna haja ya kuhaisha na kuipa hadhi kikosi cha kijeshi cha Marekani.

Rais wa shisikisho la soka Afrika Kusini akamatwa kwa tuhuma za ulaghai

Danny Jordaan amekuwa rais wa Shirikisho la Soka la Afrika Kusini tangu 2013
Maelezo ya picha,Danny Jordaan amekuwa rais wa Shirikisho la Soka la Afrika Kusini tangu 2013

Rais wa Shirikisho la Soka la Afrika Kusini (Safa) Danny Jordaan amekamatwa kutokana na madai ya kutumia fedha za shirika hilo kujinufaisha binafsi.

Kitengo cha uchunguzi wa uhalifu uliopangwa nchini humo, Hawks, kimekuwa kikichunguza madai ya ulaghai na wizi katika Safa kati ya 2014 na 2018 ya dola 72,000.

Mnamo mwezi Machi, Hawks walivamia ofisi za Safa mjini Johannesburg, na kunyang’anya kompyuta mpakato, USB, diski kuu za nje na nyaraka.

Jordaan anadaiwa kuajiri kampuni ya ulinzi binafsi kwa ajili ya ulinzi wake binafsi na kampuni ya mahusiano ya umma bila kibali kutoka kwa bodi ya Safa.

Jordaan mwenye umri wa miaka 73, ambaye alichangia pakubwa kuleta Kombe la Dunia la Fifa 2010 nchini Afrika Kusini amekuwa rais wa Safa tangu 2013.

Afisa mkuu wa fedha wa Safa Gronie Hluyo na mfanyabiashara Trevor Neethling walionekana pamoja na Jordaan, wakiwa wamekamatwa kuhusiana na kesi hiyo.

Jordaan aliripotiwa kuwasilisha ombi la mahakama siku ya Jumanne, akiwa na hati ya kiapo kukana makosa yoyote, katika jaribio la kuzuia kukamatwa kwake na Hawks.

Afisa wa Safa aliambia BBC Michezo Afrika kuwa hana maelezo zaidi kuhusu kisa hicho.

Jordaan amekuwa akikabiliwa na uchunguzwa huku kukiwa na tuhuma zinazoendelea za usimamizi mbaya na ufisadi ndani ya soka la Afrika Kusini – lakini amedumisha kutokuwa na hatia na anaripotiwa kuwania muhula wa nne kama rais wa Safa.

Wakosoaji wa Jordaan wamemtaka ajiuzulu, wakiashiria kushindwa kwa timu ya taifa ya wanaume kufuzu kwa Kombe la Dunia tangu 2010 pamoja na kuzorota kwa miundombinu ya soka ya mashinani nchini.

Tamisemi kuzingatia rai ya Chama Cha Mapinduzi kuhusu uenguliwaji

TH

Na Sammy Awami

Dar es Salaam.

Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), yenye dhamana ya kusimamia uchaguzi wa serikali za mitaaa, imesema itazingatia wito wa chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM), kama ambavyo imekuwa ikipokea na kuzingatia wito kutoka kwa wadau wengine.

Jana Katibu Mkuu wa CCM Dr Emmanuel Nchimbi aliwasilisha wito wa chama chake kwa TAMISEMI kikiitaka wizara hiyo kupuuza makosa madogo madogo yaliyotumika kuwaengua maelfu ya wagombea wa uchaguzi, hasa kutoka vyama vya upinzani, akidai kwamba chamba hicho kinatambua demokrasia ya Tanzania bado changa.

Mwanasheria mwandamizi wa TAMISEMI Mihayo Kadete amesema wizara hiyo imeendelea kuwasisitiza wasimamizi na wasimamizi wasaidizi kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa sheria na kutenda haki

“Ukitekeleza majukumu yako kwa mujibu wa sheria utakuwa umetenda haki, kwasababu sheria na kanuni zimetungwa na wadau wote wa uchaguzi”amesema Kadete

Kadete amesema anaamini wagombea waliokata rufaa baada ya kuenguliwa kwasababu kama vile kuandika chanzo cha kipato chao ni ujasiliamali na wale waliandika majina mbalimbali kifupi watakuwa wamerejeshwa kuendelea kushiriki katika uchaguzi.

Jana Waziri wa Tamisemi Mohamed Mchengerwa alitangaza kuongeza muda wa siku mbili – kutoka tarehe 13 Novemba hadi 15 Novemba saa kumi na mbili jioni – kwa ajili ya kushughulikiwa kwa rufani zilizowasilishwa na maelfu ya wagombea walioenguliwa kwasababu mbalimbali

Mchengerwa ameagiza pia kurejeshwa kwa wagombea wote walioenguliwa kwasababu ya kutodhaminiwa na vyama vyao katika ngazi ya Kijiji/Mtaa pamoja kuwa vyama vyao viliainisha kuwa ngazi ya chini ya udhamini kuwa ni Kata.

“Ninavihimiza vyama vya siasa ambavyo wagombea wao wameenguliwa kutumia vizuri muda huu wa siku mbili uliongezwa endapo hawakuridhika na uamuzi wa wasimamizi wasaidizi kuhakikisha wanawasimamia wagombea wao waweze kuwasilisha rufaa zao kwa kamati zilizopo katika kila wilaya husika” amesema Mchengerwa

Hapo jana, Makamu Mwenyekiti wa chama kikuu cha upinzani Chadema Tundu Lissu alisema hana Imani kwamba uchaguzi huu utafanyika kwa uhuru na haki akidai tayari kuna makosa mengi na makubwa ambayo yamefanyika kuanzia mwanzo wa mchakato wa uchaguzi.

“Ukiniuliza mimi nikwambie ukweli wa Mungu, nisizungumze mambo ya kisiasa siasa, kama uchaguzi huu kuna namna yoyote ile ya kuuokoa, takwambia haipo. Labda tuanze upya. Tuanze mchakato wa uchaguzi upya. Kwa uchaguzi wa mwaka huu umekwisha,” alisema Lissu

Vyama vya upinzani nchini vimekuwa vikifananisha kile kinachoendelea sasa na yale yaliyotokea mwaka 2019 ambapo wagombea wa vyama vya upinzani karibu kote nchini walienguliwa kushiriki katika uchaguzi wa serikali za mitaa.

Marekani yasema Israel haijakiuka sheria yake kuhusu kuzuia misaada huko Gaza

Mwanamke na mtoto

Marekani inasema Israel haijakiuka sheria za Marekani za kuzuia usambazaji wa misaada, baada ya muda wa mwisho wa siku 30 kuipa Israel kuongeza ufikiaji wa misaada ya kibinadamu huko Gaza au hatari ya kusitishwa kwa msaada wa kijeshi.

Maafisa walisema Jumanne kwamba Israel imechukua hatua kadhaa kushughulikia madai yake ya kuongeza usambazaji wa bidhaa Gaza, lakini wakaongeza kuwa maendeleo zaidi lazima yafanywe.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje Vedant Patel alitoa mfano wa kufunguliwa kwa njia mpya ya kuvuka ardhi, na uwasilishaji kuanza tena kaskazini, ingawa hakusema kuwa kuna walioingia kwenye kambi ya wakimbizi ya Jabalia iliyozingirwa.

Licha ya madai hayo ya Marekani, Umoja wa Mataifa umeonya kwamba kiwango cha misaada kinachoingia Gaza ni cha chini kabisa katika kipindi cha mwaka mmoja.

Ripoti inayoungwa mkono na Umoja wa Mataifa hivi karibuni ilionya kwamba kuna uwezekano wa kutokea njaa kaskazini mwa Gaza, ambako hakuna msaada wowote ulioingia katika kipindi cha mwezi uliopita.

Joyce Msuya, Kaimu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa chini ya anayeshughulikia masuala ya kibinadamu, alisema uhalifu wa kimataifa unafanywa huko Gaza.

Bi Msuya alitoa taarifa kwa wajumbe wa baraza katika Umoja wa Mataifa siku ya Jumanne, akiripoti kuwa mamlaka za Israel zinazuia usaidizi wa kibinadamu kuingia Gaza Kaskazini, ambako mapigano yanaendelea.

Watumiaji wa TikTok wafungwa Uganda kwa kuitusi familia ya rais

Rais Yoweri Museveni

Raia wawili wa Uganda wamekamatwa kwa tuhuma za kuwatusi Rais Yoweri Museveni, mkewe Janet Museveni na mtoto wa Rais, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, kwenye mtandao wa kijamii wa TikTok.

Jaji Stella Maris Amabilis aliamuru kuwa David Ssengozi, mwanzilishi wa Lucky Choice, mwenye umri wa miaka 21, na Isaya Ssekagiri mwenye umri wa miaka 28, warudishwe rumande katika gereza la Kigo hadi Jumatano, ambapo wanatarajiwa kufikishwa mahakamani.

Wanadaiwa kutumia matamshi ya chuki na kueneza habari mbaya kuhusu familia ya rais na wanamuziki wanaohusishwa na chama tawala cha NMR.

Walipofika mahakamani Jumatatu, wawili hao walikanusha mashtaka dhidi yao.

Wanashtakiwa pamoja na Julius Tayebwa, 19, ambaye tayari amefikishwa mahakamani alikini akiwa bado yuko gerezani kwa makosa sawa na hayo. Waendesha mashtaka wanasema kwamba waliochapisha habari hizo kwenye TikTok wanalenga “kukashifu, kudharaulisha, na kueneza chuki” dhidi ya familia ya Rais Museveni na watu wengine.

Hakimu aliidhinisha kuzuiliwa kwao baada ya polisi kusema kuwa bado wanachunguzwa.

Septemba 9 mwaka huu, msemaji wa jeshi la polisi nchini Uganda, Rusoke Kituuma alionya kuwa kumtukana rais aliyemtaja kuwa ni chanzo cha heshima ni kosa.

Haijabainika ni ujumbe gani uliosababisha kukamatwa kwake, lakini katika video iliyochapishwa kwenye TikTok tarehe 4 Aprili mwaka huu kwenye ukurasa wa LuckyChoice70, wenye kichwa “maadui wangu wa kwanza”, aliikosoa familia ya rais kwa kutumia lugha chafu zinazohusiana na ngono.

Askofu Mkuu wa Canterbury ajiuzulu kwa kashfa ya unyanyasaji iliyokumba Kanisa

Askofu Justin Welby

Askofu Mkuu wa Canterbury ametangaza kujiuzulu wadhifa wake kufuatia ripoti ya kulaaniwa kuhusu mnyanyasaji mkubwa wa watoto anayehusishwa na Kanisa la Uingereza.

Uchunguzi uligundua kuwa Justin Welby, 68, “angeweza na alipaswa” kuripoti unyanyasaji wa John Smyth kwa wavulana na vijana kwa polisi mnamo 2013.

Katika taarifa, Bw Welby alisema kuwa “ni wazi kabisa kwamba lazima nichukue jukumu binafsi na la kitaasisi” kwa majibu yake baada ya kuambiwa mara ya kwanza kuhusu unyanyasaji huo.

“Ninaamini kwamba kujiondoa ni kwa manufaa ya Kanisa la Uingereza.”

“Natumai uamuzi huu unaonyesha wazi jinsi Kanisa la Anglikana linaelewa kwa uzito hitaji la mabadiliko na kujitolea kwetu kwa kina kujenga kanisa salama.

Msemaji wa Waziri Mkuu Keir Starmer alisema “anaheshimu uamuzi ambao umechukuliwa na kuwa yuko pamoja na waathiriwa wote”.

Haijabainika mara moja ni lini askofu huyo mkuu ataacha wadhifa wake lakini huenda mchakato wa kumpata mtu mwingine ukachukua takribani miezi sita.

Polisi Tanzania yachunguza picha za watu wakimkamata mfanyabiashara kwa nguvu

Polisi Tanzania

Jeshi la Polisi Tanzania limesema linachunguza picha ya video inayosambaa kwenye mitandao ya kijamii ikionesha watu ambao wanajaribu kumkamata na kujaribu kumuingiza kwa nguvu ndani ya gari, Bw. Deogratius Tarimo ambaye ni mfanyabiashara na mkazi wa mkoa wa Pwani.

Kwa mujibu wa ushahidi uliowasilishwa kituoni hapo na mwathirika huyo, chanzo cha tukio na kilichomsukuma kufika katika hoteli ya Rovenpic jijini Dar es Salaam, ni kufanya mazungumzo ya biashara ambayo amekuwa akiwasiliana kuifanya na aliokuwa akiwasiliana nao tangu Oktoba 25, mwaka 2024. Taarifa ya polisi imeeleza.

Jeshi la polisi limesema litawakamata watu waliokuwa wakijaribu kumkamata na kumuingiza kwenye gari, kama ilivyokuwa ikionekana kwenye picha, na kulingana na ushahidi uliokusanywa na unaoendelea kukusanywa ili hatua nyingine zichukuliwe.

Musk apata kazi aliyoahidiwa baada ya kumuunga mkono Trump

Elon Musk

Ni jukumu gani ambalo bilionea wa teknolojia na mfuasi maarufu wa Trump Elon Musk anaweza kuchukua katika utawala mpya limekuwa suala la uvumi na matarajio makubwa.

Sasa “Wizara ya Ufanisi wa Serikali” ambayo tayari imetangazwa, Doge kwa kifupi, inaonekana kuibuka.

Musk ataongoza Doge, jina lake rejeleo dhahiri la sarafu ya siri ya Dogecoin, pamoja na mjasiriamali na mgombea wa zamani wa urais Vivek Ramaswamy.

Hatahivyo, taarifa inasema “Wizara” itaongoza kutoka nje ya serikali, ikionesha kuwa inaweza kuchukua jukumu zaidi la ushauri.

Ukweli ni kwamba hatujui sura yake kamili, rasilimali na uwezo wake, lakini Trump daima alikuwa na uwezekano wa kutaka kuwatuza wawakilishi hawa waaminifu wa kampeni.

Netanyahu azungumzia “kuharibu uchumi wa Iran”

Netanyahu

Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu,alihutubia watu wa Iran katika video mpya ambayo aliichapisha kwenye mtandao wa kijamii wa X. ambayo imezingatia “kuangamizwa kwa Israeli”.

Bw. Netanyahu anadai katika video hiyo kwamba shambulio la hivi punde la kombora la Iran dhidi ya nchi hiyo liliigharimu serikali ya Iran “dola bilioni mbili na nusu”, ingawa video haitoi maelezo ya kina kuhusu jinsi takwimu hizi zilivyohesabiwa.

Kwa kuwasilisha takwimu hizi, anawashutumu watawala wa Iran kwa “kuhangaishwa na uharibifu wa Israeli” badala ya kutumia rasilimali hizi katika afya, elimu na maendeleo. Bwana Netanyahu anaendelea kusema kwamba ikiwa Iran itaishambulia tena Israel, matokeo yatakuwa “kupooza kwa uchumi wa Iran”.

Likiangazia matamshi ya Bwana Netanyahu, gazeti la The Times la Israel liliandika kwamba tafsiri moja ya sehemu hii ya hotuba ya Waziri Mkuu wa Israel inaweza kuwa kwamba anasema katika kujibu mashambulizi mengine ya Iran, Israel itajaribu kutoa “pigo kubwa kwa uchumi wa Iran”.

Hata hivyo, inaonekana kwamba kauli za Waziri Mkuu wa Israel, ambaye alituma ujumbe kwa watu wa Iran katika video kama hiyo muda si mrefu uliopita, zimejikita zaidi katika gharama kubwa za silaha na makabiliano ya kijeshi ya moja kwa moja yanayofanywa na serikali nchini humo.

Wakati hali ya kiuchumi na kimaisha Nchini Iran si ya kuridhisha miongoni mwa watu wake.

Kauli za Benjamin Netanyahu kuhusu gharama za mivutano ya hivi karibuni ya kijeshi kati ya Israel na Iran zimetajwa huku wakosoaji wa serikali ndani ya Israel wakizungumzia gharama kubwa “zisizokuwa na kifani” za vita vya Gaza na Lebanon kwa nchi hii.

“Tuko katika vita virefu na vya gharama kubwa zaidi katika historia ya Israeli,” Waziri wa Fedha wa Israeli Betsal Smotrich aliambia Knesset Septemba mwaka jana, akiongeza kuwa hatua za kijeshi zinaweza kugharimu shekeli bilioni 200 hadi 250 (kati ya dola bilioni 54 na 68).

Watu 23 wauawa kutokana na mashambulizi ya Israel nchini Lebanon, wizara yasema

Athari za mashambulizi

Takribani watu 23 wameuawa katika mashambulizi ya anga ya Israel dhidi ya nyumba mbili katikati mwa Lebanon ambako familia zilizopoteza makazi ziliripotiwa kuishi, wizara ya afya ya Lebanon inasema.

Watu 15, wengi wao wakiwa wanawake na watoto, waliuawa huko Joun na wengine wanane waliuawa karibu na Baalchmay. Vijiji vyote viwili viko katika eneo la Mlima Lebanon na maeneo ya nje ambako kundi lenye silaha la Hezbollah lina uwepo mkubwa.

Jeshi la Israel lilisema lilikuwa likichunguza mashambulizi hayo, ambayo yalikuja baada ya kugonga kile ilichosema ni malengo kadhaa ya Hezbollah katika vitongoji vya kusini mwa Beirut.

Wakati huohuo, watu wawili waliuawa kutokana na kurushwa kwa roketi ya Hezbollah katika mji wa Nahariya kaskazini mwa Israel.

Ilikuja siku moja baada ya waziri wa ulinzi wa Israel kukataa kusitisha mapigano na Hezbollah hadi malengo yake ya vita yatimizwe.

Jeshi la Israel lilifanya mashambulizi dhidi ya Hezbollah, ambayo inaidhinisha kama shirika la kigaidi, baada ya karibu mwaka wa mapigano ya kuvuka mpaka yaliyosababishwa na vita huko Gaza.

Israel inasema inataka kuhakikisha wanarejesha salama makumi ya maelfu ya wakaazi wa eneo la mpaka wa kaskazini mwa Israel waliokimbia makazi yao kutokana na mashambulizi ya roketi, ambayo Hezbollah ilianzisha kuunga mkono Wapalestina siku moja baada ya shambulio baya la mshirika wake Hamas dhidi ya Israel tarehe 7 Oktoba 2023.

Zaidi ya watu 3,200 wameuawa nchini Lebanon tangu wakati huo, ikiwa ni pamoja na 2,600 katika wiki saba tangu Israel ianzishe kampeni kali ya anga na kufuatiwa na uvamizi wa ardhini kusini, kulingana na wizara ya afya ya Lebanon. Watu wengine milioni 1.2 wamelazimika kuyahama makazi yao.

All Rights Reserved © Cantona Group PLC||2024


Discover more from cantonadigital

Subscribe to get the latest posts sent to your email.

Leave a comment