Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa
Wapiganaji wa Hezbollah wamesema wamerusha roketi kuelekea kaskazini mwa Israeli, ikiwemo kambi ya jeshi karibu na mji wa Haifa hatua inayokuja baada ya Israeli kuripoti mashambulio kutokea nchini Lebanon.
Kwa mujibu wa Hezbollah, walilenga kambi ya jeshi kaskazini mwa mji wa Haifa, kundi hilo likiahidi kuongeza kasi ya mashambulio dhidi ya Israeli zikiwa zimepita wiki kadhaa tangu kuzuka upya kwa makabiliano Septemba 23.
Katika taarifa yake ya awali, wapiganaji hao wanaoungwa mkono na Iran walithibitisha kurusha makombora kuelekea kaskazini mwa mji wa Haifa.
Watu watano walijeruhiwa katika eneo la Kiryat Ata, katika mji wa Haifa kwa mujibu wa taarifa ya msemaji wa idara ya mambo ya dharura Magen David Adom.
Kombora pia liliharibu jengo lenye orofa tatu pamoja na kuteketeza magari mawili katika eneo la Kiryat Ata, magari ya kuzima moto na yale ya kuwabeba wagonjwa yakiwa yametumwa kwenye eneo hilo wakati tukichapisha taarifa hii.
Mashambulio ya Haifa yamekuja baada ya Israeli kuripoti kutokea kwa shambulio dhidi ya mojawapo ya makazi ya Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu katika mji wa katikati mwa Israeli wa Caesarea.
Ofisi ya Netanyahu imesema Waziri Mkuu na mkewe hawakuwa kwenye makazi yao wakati wa shambulio hilo na kwamba hakuna watu waliojeruhiwa.

Wapiganaji wa Hezbollah wanaoungwa mkono na Iran wamesema wanaanzisha aina mpya ya makabiliano dhidi ya Israeli.
Mapigano hayo yamesbabisha vifo vya karibia watu 1,418 nchini Lebanon, kwa mujibu wa takwimu za shirika la habari AFP likinukuu wizara ya afya ya Lebanon japokuwa huenda idadi hiyo ikawa kubwa.
Israeli imetekeleza mauaji ya kiongozi wa Hezbollah Hassan Nasrallah kusini mwa Beirut katika shambulio la anga la tarehe 27 ya mwezi Septemba.
All Rights Reserved © Cantona Group PLC||2024
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.