AFRIKA LEO JIONI -HABARI KAMILI

Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph

KINARA wa upinzani Raila Odinga Jumatatu aliongoza ODM kususia mkutano wa Baraza Kuu la Azimio la Azimio, kikao kilichostahili kuongozwa na Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta.

Tukio hilo sasa linaweka bayana kuwa huenda ukuruba wa kisiasa kati ya Bw Kenyatta na Raila katika uchaguzi mkuu wa 2022, umeisha na huenda kila moja ataenda njia zake mnamo 2027.

Mkutano wa baraza la Azimio ulikuwa uandaliwe saa 10 jioni na kuongozwa na Bw Kenyatta ambaye ni Mwenyekiti wa muungano huo. Hata hivyo, mambo yalibadilika baada ya ODM kuitisha kikao kingine na wanahabari na kutoa onyo kali dhidi ya Raila kutemwa Azimio.

Wawakilishi wa Wiper, DAP-Kenya, Kanu na PNU walikuwa tayari kwa mkutano huo ambao ulikuwa uandaliwe kupitia mtandao wa Zoom.

Hata hivyo, Narc Kenya ambayo kiongozi wake Martha Karua alishatangaza kuwa anaondoka Azimio na ODM haikuwa imethibitisha kuwa wangehudhuria kikao hicho.

‘Kuchezea kaa la moto’
Badala yake, ODM ikiongozwa na mwenyekiti wake Gladys Wanga (Gavana wa Homa Bay) waliitisha kikao na wanahabari ambapo walisema kuwa hawakuwa na ufahamu kuhusu mkutano huo. Isitoshe walionya dhidi ya jaribio lolote la kumbandua Raila kama kiongozi wa Azimio wakisema ni kama ‘kuchezea kaa la moto’.

Katika kile kilichoonekana kama ‘kiburi’ cha ODM, Bi Wanga pia alisema kuwa ni Katibu wa Azimio Junet Mohamed ndiye ana mamlaka ya kuitisha mkutano wa muungano huo wa upinzani.

Bw Mohamed ni mwandani wa Raila na Kiongozi wa Wachache kwenye Bunge la Kitaifa.

Kinara wa DAP-Kenya Eugene Wamalwa ambaye alikuwa tayari kwa mkutano huo alisisitiza kuwa Mabw Odinga na Mohammed walikuwa wakifahamu kuwa mkutano huo ulikwepo lakini wakaususia na kuusambaratisha.

“Mchana huu tulikuwa tuwe na mkutano wa baraza la Azimio ambao ulikuwa uongozwe na Uhuru Muigai Kenyatta. Sote tulialikwa na mkutano ulikuwa uanze saa 10 jioni lakini wenzetu wa ODM nao wakati huo wakaitishia kikao na kukashifu baraza la Azimio,” akasema Bw Wamalwa.

“Kwa hivyo, mkutano huo haukufanyika. Hii ina maana kuwa kila chama sasa kimeachwa kuamua mustakabali wake kuhusu kusalia au kuondoka Azimio jinsi ODM wamefanya,” akaongeza.

Jaribio la ‘kumtimua’ Raila Azimio
Katika kikao na wanahabari, ODM ilionya kuhusu jaribio lolote la kumpindua Raila Azimio. Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka alifichua kuwa Bw Kenyatta angeongoza mkutano kuamua mustakabali wa uongozi wake baada ya wanachama watano wa ODM kuteuliwa serikalini.

“Tulitarajia Uhuru ambaye ni mwenyekiti wa Azimio aongoze mkutano huo ili tujadiliane kuhusu changamoto zinazingira muungano wetu,” akasema Bw Musyoka.

Hata hivyo, Bi Wanga na Naibu Kiongozi wa ODM Geodfrey Osotsi ambaye pia ni Senata wa Vihiga, alisema kuwa mkutano wowote wa Azimio lazima ushirikishe ODM ili uwe na uzito.

Bw Osotsi alitoa onya kali kuwa jaribio lolote la kuandaa mkutano wa Azimio ili kumtimua Bw Odinga, utakumbana na vizingiti na adhabu kali kwa waliohudhuria.

“Ni Katibu Mkuu Junet Mohamed ndiye ana mamlaka ya kuitishia mkutano na hajafanya hivyo. Wakiendelea na kuwa na mkutano basi utakuwa wa kunywa chai au ule wa kangaroo na sio wa Azimio,” akasema Bw Osotsi.

Mgawanyiko unaojihidhirisha wazi unatokea tu baada ya Bw Odinga wiki jana kudai ni rais huyo mstaafu ndiye alimpigia simu aridhiane na Rais William Ruto.

Akiwa katika Kaunti ya Elgeyo Marakwet, Raila alisema alisukumwa na Uhuru kuchukua hatua hiyo ili kutuliza nchi wakati ambapo maandamano ya Gen Z yalikuwa yameteka nchi mwezi uliopita.


KIUNGO mahiri Luka Modric wa klabu ya Real Madrid, amejumuishwa katika kikosi cha wachezaji 24 wa timu ya taifa ya Croatia itakayoshiriki michuano ya UEFA Nations League, licha ya umri wake mkubwa.

Modric ambaye alisaini mkataba wa mwaka mmoja kuendelea kuchezea Madrid, ana umri wa miaka 39. Hata hivyo, kocha Zlatko Dalic, anaamini kwamba umri sio tatizo, huku akisisitiza kwamba nyota huyo angali na nguvu za kusaidia timu ya taifa baada ya kuzidi kutwaa tuzo za mchezaji bora katika mashindano mbalimbali.

Kiungo huyo mchezeshaji aliye kwenye orodha ya wachezaji wanaoongoza katika ufungaji mabao kwenye klabu ya Madrid, ndiye staa wa kutoa pasi za uhakika, hivyo mchango wake hauwezi kupuuzwa.

“Umri sio tatizo, bali kitu muhimu ni jinsi anavyocheza uwanjani na kusaidia timu. Bila shaka ataendelea kuwika kwa miaka mingi,” aliongeza kocha Dalic.

Modric amechezea Croatia mara 178 tangu apewe nafasi kwa mara ya kwanza mnamo 2006, alipokuwa na umri wa miaka 20. Tayari Domagoj Vida na Marcelo Brozovic wa rika lake wamestaafu kucheza soka ya kimataifa.

Croatia wamepangiwa katika Kundi A la Nations League ambapo wataanzia ugenini dhidi ya Ureno mnamo Septemba 5, kabla ya kualika Poland siku tatu baadaye.

MFANYABIASHARA bilionea Yagnesh Devani aliyekwepa mkono mrefu wa sheria miaka 15 alipokuwa ametorokea Uingereza, Jumatatu, Agosti 19, 2024 aliachiliwa kwa dhamana ya Sh20 milioni baada ya kukaa gerezani siku 13.

Devani alizuiliwa katika gereza la Viwandani, Nairobi baada ya kukanusha mashtaka ya kuifuja Benki ya Kenya Commercial 2008 ilipofadhili kampuni ya Triton Oil ununuzi wa mafuta ya ndege kwa thamani ya mabilioni ya pesa.

Devani, mmiliki wa Kampuni ya Triton Oil, aliyetiwa nguvuni Ulaya na kurudishwa nchini na polisi wa kimataifa Machi mwaka huu, 2024, alisukumwa gerezani Agosti 7, 2024 baada ya kukana mashtaka ya ulaghai na wizi wa Sh7.6 bilioni, katika kashfa ya mafuta ya ndege katika mabomba ya Kipevu, Kaunti ya Mombasa mwaka wa 2008.

Devani alikana aliilaghai Kenya Commercial Bank (KCB) mabilioni hayo.

Ni KCB iliyokuwa imeidhamini Triton mkopo wa kuwekeza katika biashara hiyo ya mafuta.

Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) Renson Ingonga kupitia kwa wakili wa serikali Jeremiah Walusala aliambia mahakama, Devani aliuza mafuta hayo yaliyokuwa yanamilikiwa na KCB.

Aliposhtakiwa Agosti 7, 2024 Bw Walusala alipinga Devani kuachiliwa kwa dhamana akisema “atatoroka jinsi alihepa kizimba kwa miaka15.”

Lakini hakimu mkuu mahakama ya kuamua kesi za ufisadi Thomas Nzioki alimwachilia Devani kwa dhamana ya Sh20 milioni na mdhamini mmoja wa kiasi hicho, ama, alipe dhamana ya pesa tasilimu Sh5 milioni.

Nzioki alisema ripoti ya idara ya urekebishaji tabia imewahoji watu wa familia ya mshtakiwa na wametoa ushuhuda ni mfanyabiashara aliyewekeza mali mengi na kwamba ameoa na yuko na mke na mtoto mmoja.

Hakimu alimwamuru mshtakiwa awasilishe pasipoti yake kortini na kumwonya ataona cha mtema kuni akivuruga mashahidi.

Kesi hiyo itatajwa manmo Agosti 29, 2024 kutengewa siku ya kusikizwa.

All Rights Reserved © Cantona Group Ltd||2024


Discover more from cantonadigital

Subscribe to get the latest posts sent to your email.

Leave a comment