Radio Fortune Africa -Ukweli na Burudani
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

Na: Cantona Joseph|RFA

Polisi jijini Dar es Salaam wametawanya kundi la vijana waliokuwa wakijaribu kuandamana katika eneo la Kimara Kibo, umbali wa kati ya Ubungo na Kimara, wakati huu wa uchaguzi mkuu unaoendelea nchini.
Mashuhuda wamesema kundi hilo la vijana lilianza kujikusanya karibu na Kanisa la Ufufuo na Uzima, ambalo lilifungiwa hivi karibuni. Kanisa hilo la Askofu Josephat Gwajima, ambaye alikuwa mbunge wa chama tawala, CCM, kuanzia mwaka 2015 hadi mwaka huu. Gwajima amekuwa akijulikana kwa misimamo yake ya kupinga vitendo vya utekaji na ukiukwaji wa haki za binadamu, hatua ambayo iliwahi kumuweka kwenye mvutano na mamlaka za serikali.
Hadi kufikia muda huu, polisi wanaendelea kudhibiti hali ya eneo hilo huku magari ya doria yakionekana katika barabara kuu ya Morogoro Road. Hakuna taarifa rasmi za majeruhi wala idadi kamili ya waliokamatwa.
Maandamano haya ni sehemu ya mwitikio wa mitandaoni wa makundi ya wanaharakati na vijana wakitaka mageuzi zaidi ya kisiasa. Hata hivyo, hadi sasa, maandamano hayo yalikuwa hayajashuhudiwa kwa kiwango kikubwa nchini kote.
All Rights Reserved © The Cantona Group PLC||2025
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.