Radio Fortune Africa -Ukweli na Burudani
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa


Kuachiliwa kwa mateka 48 wa Israeli – 20 kati yao wanaaminika kuwa hai – inatarajiwa kuanza muda mfupi ujao, pamoja na kuachiliwa kwa mamia ya wafungwa wa Palestina.
Na:Cantona Joseph|RFA
Trump awasili Israel

Huku kuachiliwa kwa mateka hao wa Israel kukiendelea, Rais wa Marekani Donald Trump amewasili nchini Israel.
Ndege ya Trump imetua hivi punde katika Uwanja wa Ndege wa Ben Gurion viungani mwa Tel Aviv, huku akianza ziara yake ya siku chache nchini humo.
Watu kadhaa wakuu wamefika kumkaribisha – akiwemo Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu na mkewe Sara, Mjumbe Maalum wa Marekani Steve Witkoff, mshauri Jared Kushner na mkewe – na bintiye Trump – Ivanka Trump.
Netanyahu anamkaribisha Trump
Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu ameshuhudiwa akipeana mkono na Donald Trump wakati akimkaribisha rais huyo wa Marekani nchini Israel.

Waisraeli wakusanyika kusubiri mateka ‘huku Trump akisema’ Vita vimekwisha ‘Gaza

Hamas inatazamiwa kuwaachilia mateka 48 waliosalia Gaza ifikapo saa sita mchana (09:00 GMT). Kati ya hao, 20 wanaaminika kuwa hai, na wanatarajiwa kupelekwa haraka kwa matibabu kabla ya kuunganishwa tena na wapendwa wao. Miili ya wengine 28 inastahili kurejeshwa.
Haya yanajiri wakati Rais wa Marekani Donald Trump anafanya ziara nchini Israel kufuatia makubaliano yaliyosimamiwa na Marekani, Misri na Qatar.
Trump atalihutubia bunge la Israel kabla ya kusafiri hadi mji wa wa Misri wa Sharm El-Sheikh kuandaa mkutano wa kilele wa amani katika Mashariki ya Kati, utakaojumuisha takriban viongozi wengine 20 wa dunia.
Trump atapokelewa na “makundi ya Waisraeli kwa shukrani na urafiki”, Rais wa Israel Isaac Herzog alisema Jumapili, huku Waisraeli wengi wakimsifu rais wa Marekani kwa makubaliano ya kusitisha mapigano.
Kwa mabadilishano ya kurejesha mateka hao, Israel itawaachia huru wafungwa 250 wa Kipalestina, wakiwemo wanaotumikia kifungo cha maisha jela. Hiyo ni pamoja na kuwaachilia zaidi ya wafungwa 1,700 waliokuwa wakizuiliwa bila kufunguliwa mashtaka katika kipindi cha vita – wakiwemo karibu Watoto zaidi ya kumi.
Kwingineko, malori yaliyobeba misaada yanavuka mpaka na kuingia Gaza huku Wapalestina, waliohamishwa kwa nguvu kuelekea kusini kutokana na mashambulizi ya Israel, wakiendelea kurejea eneo la kaskazini mwa eneo hilo. Wanakumbana na uharibifu uliotokea, maeneo makubwa ya Jiji la Gaza yakiwa vifusi.
Hamas imeanza kuwaachilia huru mateka wa Israel huko Gaza

Mateka wa kwanza wa Israel sasa wamehamishwa kutoka Hamas hadi kwenye Shirika la Msalaba Mwekundu huko Gaza, afisa aliyehusika katika operesheni hiyo ameliambia shirika la habari la Reuters.
Mateka saba wa Israel waripotiwa kukabidhiwa na Hamas
Bado tunasubiri uthibitisho rasmi kutoka kwa jeshi la Israeli na ICRC, lakini vyombo vya habari vya Israeli vinaripoti kwamba mateka saba wa Israeli wameachiliwa huru na Hamas na sasa wako chini ya Shirika la Msalaba Mwekundu
- Eitan Mor
- Gali Berman
- Ziv Berman
- Matan Angrest
- Omri Miran
- Alon Ehal
- Guy Gilboa Dallal
IDF yapokea mateka saba wa kwanza

Jeshi la Israeli limethibitisha kuwa mateka saba wa kwanza sasa wamepokelewa na Jeshi la Ulinzi la Israeli (IDF).
Wizara ya mambo ya nje ya Israel imethibitisha majina ya mateka saba wa kwanza walioachiliwa kutoka Hamas asubuhi ya leo:
- Eitan Mor
- Gali Berman
- Ziv Berman
- Omri Miran
- Alon Ohel
- Guy Gilboa-Dalal
- Matan Angrest
Imeshiriki majina hayo katika machapisho kwenye mitandao ya kijamii, na picha za mateka kando yake na nukuu inayosomeka: “Karibu nyumbani.”





Mateka ambao bado wako Gaza wazungumza na wapendwa wao

Nimrod Cohen akizungumza na mama yake kwenye simu

Ndugu David na Ariel Kunio pia walizungumza na wapendwa wao
Mateka wengine 13 walio hai wanatarajiwa kuachiliwa leo, pamoja na saba ambao tayari wameachiliwa.
Bado hatujapata uthibitisho kwamba wameachiliwa, lakini picha zimeshirikiwa zinazoonyesha baadhi ya mateka wakizungumza na wapendwa wao kupitia Video.
Mapigano yamezuka kati ya vikosi vya Hamas na wanaukoo wenye silaha katika mji wa Gaza

Takriban watu 27 wameuawa katika mapigano makali kati ya vikosi vya usalama vya Hamas na watu wenye silaha wa familia ya Dughmush katika mji wa Gaza, katika moja ya makabiliano makali zaidi ya ndani tangu kumalizika kwa operesheni kuu za Israel katika eneo hilo.
Wanachama wa Hamas waliokuwa wamejifunika yuso walirushiana risasi na wapiganaji wa koo karibu na hospitali ya mji wa Jordan, walioshuhudia walisema.
Afisa mkuu katika wizara ya mambo ya ndani inayoongozwa na Hamas alisema vitengo vya usalama viliwazingira na kushiriki katika mapigano makali kuwazuilia.
Wizara hiyo ilisema wanachama wake wanane waliuawa katika “shambulio la silaha na wanamgambo”.
Duru za kimatibabu zilisema watu 19 wa ukoo wa Dughmush na wapiganaji wanane wa Hamas wameuawa tangu mapigano yaanze siku ya Jumamosi.
Trump asema huenda akatuma makombora ya Tomahawk nchini Ukraine

Rais wa Marekani Donald Trump anafikiria kutuma makombora ya masafa marefu ya Tomahawk nchini Ukraine, akisema itakuwa “hatua mpya” katika vita vyake na Urusi.
Alipoulizwa kwenye Air Force One kama angetuma Tomahawks nchini Ukraine, Trump alijibu “tutaona… naweza”.
Hii inafuatia simu ya pili mwishoni mwa juma kati ya Trump na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky, ambaye alishinikiza kuwepo kwa uwezo mkubwa wa kijeshi kuanzisha mashambulizi ya kukabiliana na Urusi.
Hapo awali Moscow iliionya Washington dhidi ya kutoa makombora ya masafa marefu kwa Kyiv, ikisema kuwa hatua hiyo itasababisha kuongezeka kwa mzozo huo na kuzorotesha uhusiano kati ya Marekani na Urusi.
China yaishutumu Marekani kwa ‘uonevu’ juu ya tishio la ushuru

Tishio la hivi punde la Donald Trump la kutoza ushuru wa ziada wa 100% kwa bidhaa za China ni “mfano wa kawaida wa uonevu wa Marekani”, serikali ya China imesema.
Msemaji wa wizara ya biashara pia alisema China inaweza kuanzisha “hatua” zake ambazo hazijabainishwa ikiwa rais wa Marekani atatekeleza tishio lake, akiongeza kuwa “haiogopi” uwezekano wa vita vya kibiashara.
Siku ya Ijumaa, Trump alijibu hatua ya Beijing ya kutekeleza sheria kali za mauzo ya madini adimu, akiishutumu kwa “kuwa na uadui” na kujaribu “kushikilia” ulimwengu. Pia alitishia kujiondoa katika mkutano na Rais wa China Xi Jinping baadaye mwezi huu.
Lakini siku ya Jumapili, Trump aliandika: “Usijali kuhusu China, yote yatakuwa sawa!”
Mali yaweka ada ya viza ya $10,000 kwa wageni wa Marekani

Mali imetangaza kuwa raia wa Marekani wanaotembelea nchi hiyo ya Afrika Magharibi watatakiwa kulipia ada ya hadi $10,000 (£7,500) kwa ajili ya viza za biashara na utalii, ili kukidhi matakwa sawa na hayo ambayo utawala wa Trump umeweka kwa raia wake.
Ubalozi wa Marekani nchini Mali ulisema siku ya Ijumaa ada hiyo ilianzishwa ili kuimarisha “dhamira ya Marekani ya kulinda mipaka ya Marekani na kulinda usalama wa taifa la Marekani”.
Wizara ya mambo ya nje ya Mali ilisema Jumapili kwamba ada hiyo iliwekwa kwa kuegemea upande mmoja, na imeamua “kuanzisha mpango wa viza sawa na huo” kwa raia wa Marekani.
Mabadiliko ya sera ya viza yanakuja licha ya hatua za kuboresha uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.
All Rights Reserved © The Cantona Group PLC||2025
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.