Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

Katika hotuba ya kina iliyotolewa kwenye Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Jumamosi, Lavrov alisema kuwa vitisho vya nchi za Magharibi dhidi ya Urusi vinazidi kuwa “vya kawaida.”
Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi Sergei Lavrov amesema nchi yake haina nia ya kushambulia nchi za Umoja wa Ulaya au wanachama wa NATO – lakini akaonya juu ya “kuchukua hatua madhubuti” kwa “uchokozi” wowote unaoelekezwa kwa Moscow.
Katika hotuba ya kina iliyotolewa kwenye Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Jumamosi, Lavrov alisema kuwa vitisho vya nchi za Magharibi dhidi ya Urusi vinazidi kuwa “vya kawaida”.
Pia aliikosoa Israel, akisema kwamba wakati Urusi ililaani mashambulizi ya Hamas mnamo Oktoba 7, 2023, hakuna “uhalali” wa “mauaji ya kikatili” ya Wapalestina huko Gaza, au kwa mipango ya kunyakua Ukingo wa Magharibi.
Awali Israel ilikuwa imesema kwamba operesheni yake huko Gaza ilikuwa muhimu ili kuwashinda Hamas.
Takriban watu 65,926 wameuawa katika mashambulizi ya Israel, kwa mujibu wa Wizara ya Afya ya Gaza, huku takriban watu 1,200 wakiuawa na wengine 251 kuchukuliwa mateka katika mashambulizi ya Oktoba 7.
Trump ana matumaini ya kufikiwa kwa mpango wa amani wa Gaza

Rais wa Marekani Donald Trump anatarajia kukamilisha pendekezo la mpango wa amani wa Gaza katika mkutano wa Jumatatu na Waziri Mkuu wa Israel, Trump aliambia Reuters siku ya Jumapili, wakati vifaru vya Israel vikisonga mbele zaidi katika mji wa Gaza huku Hamas ikisema imepoteza mawasiliano na mateka wawili waliokuwa wameshikiliwa huko.
Hatima ya mateka hao wawili, waliosababisha hisia kali ndani ya Israel, inaweza kuwa na athari mbaya kwenye mkutano kati ya Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu na Trump siku ya Jumatatu.
Kikosi cha kijeshi cha Hamas, Al-Qassam Brigedi, kiliitaka Israel siku ya Jumapili kuwarudisha nyuma wanajeshi wake na kusitisha mashambulizi ya anga katika mji wa Gaza kwa saa 24 ili wapiganaji waweze kuwapata mateka.
Trump aliliambia shirika la habari la Reuters katika mahojiano ya simu kuwa amepokea “jibu la kutia moyo” kutoka kwa Israel na viongozi wa Kiarabu kuhusu pendekezo la mpango wa amani wa Gaza na kwamba “kila mtu anataka makubaliano yafikiwe.”
Hamas ilisema bado haijapokea pendekezo lolote kutoka kwa Trump wala kutoka kwa wapatanishi.
Israel imefanya shambulio kubwa la ardhini katika mji wa Gaza, na kusambaratisha wilaya nzima huku ikiamuru mamia kwa maelfu ya Wapalestina kukimbilia katika kambi zilizo na mahema, katika kile Netanyahu anasema ni kutaka kuangamiza Hamas.
Raia wa Marekani aachiliwa na Taliban baada ya kuzuiliwa kwa miezi tisa

Raia wa Marekani aliyeshikiliwa na kundi la Taliban nchini Afghanistan kwa muda wa miezi tisa ameachiliwa huru kufuatia mazungumzo yaliyoongozwa na wapatanishi wa Qatar, maafisa wanasema.
Mwanamume huyo aliyetambulika kwa jina la Amir Amiry, ni Mmarekani wa tano kuachiliwa kutoka kizuizini nchini Afghanistan mwaka huu. Alikuwa njiani kurejea Marekani siku ya Jumapili.
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Marco Rubio aliishukuru Qatar kwa “juhudi zake za kidiplomasia zisizochoka”, ambazo alisema ni muhimu katika kufanikisha kuachiliwa kwa Bw Amiry.
Sababu ya kuzuiliwa kwa Bw Amiry bado haijafahamika. Rubio alisema kuwa “alizuiliwa kimakosa”.
Waziri huyo wa mambo ya nje ameongeza kuwa raia zaidi wa Marekani bado “wanazuiliwa kinyume cha sheria” nchini Afghanistan na kwamba utawala wa Trump ulikuwa ukifanya kazi ya kuwaachilia huru.
Wizara ya mambo ya nje ya Qatar ilisema iliwezesha kuachiliwa kwa Bw Amiry na kwamba alikuwa njiani kuelekea Doha kabla ya kusafiri kwenda Marekani.
Boti ndogo yaweka rekodi ya kubeba wahamiaji wengi zaidi kwenye kivuko

Boti ndogo ilivuka kivuko siku ya Jumamosi ikiwa imebeba wahamiaji 125, idadi kubwa zaidi kuwahi kusafari katika chombo kimoja cha aina hiyo.
Rekodi hiyo imepita ile iliyowekwa mwezi Agosti wakati watu 106 walipojaribu kuvuka kwa kutumia boti moja.
Takwimu kutoka Ofisi ya Mambo ya Ndani zinaonyesha wahamiaji 895 walivuka kivuko kwa boti 12 siku ya Jumamosi, wakati karibu watu 33,000 wamefanya hivyo tangu kuanza kwa 2025.
Hili linatokea baada ya mhamiaji mwingine kufariki akijaribu kuvuka kivuko, na mwili kupatikana Jumapili asubuhi kwenye ufuo karibu na Boulogne-sur-Mer kaskazini mwa Ufaransa, kulingana na shirika la habari la AFP.
Takriban watu wanne wafariki na wengine kujeruhiwa katika tukio la ufyatuaji risasi kanisani huko Michigan

Takriban watu wanne wameuawa na wengine kadhaa kujeruhiwa baada ya mtu mwenye silaha kuliendesha gari katika kanisa la Michigan, kufyatua risasi na kuchoma jengo hilo, polisi wanasema.
Maafisa walisema shambulio dhidi ya Kanisa la Jesus Christ of Latter-day Saints huko Grand Blanc, mji ulio umbali wa maili 60 (kilomita 100) kaskazini magharibi mwa Detroit, lilitokea wakati wa ibada ya Jumapili iliyovutia mamia ya watu.
Mshukiwa huyo aliyetambulika kwa jina la Thomas Jacob Sanford, 40, kutoka Burton, Michigan, baadaye aliuawa kwa kupigwa risasi na polisi katika eneo la kuegesha magari la kanisa.
Mamlaka inachunguza tukio hilo kama “kitendo cha vurugu zilizolengwa”, lakini wanasema nia bado haijafahamika.
Tazama: China yafungua daraja kubwa zaidi duniani

China imefungua rasmi daraja kubwa zaidi duniani kwa umma.
Daraja la Grand Canyon la Huajiang lina urefu wa 625m (2,083ft) juu ya bonde katika mkoa wa Guizhou.
Wenye mamlaka wanasema daraja hilo linapunguza muda wa kusafiri kati ya pande mbili za bonde hilo kutoka saa mbili hadi dakika mbili.
Mapema mwaka huu mnamo mwezi Agosti, timu husika ilifanya majaribio kwa kuendesha malori 96 kwenye sehemu zilizotengwa ili kuangalia uadilifu wa muundo wa daraja.
Daraja hilo sasa limeweka rekodi ya daraja kubwa zaidi ulimwenguni lililojengwa katika eneo lenye mlima.
All Rights Reserved © The Cantona Group PLC||2025
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.