Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

Shirika la Ujasusi la Marekani FBI limewafuta kazi kundi la askari waliopigwa picha wakiwa wamepiga magoti kwenye maandamano ya kupinga mauaji ya George Floyd, vyombo vya habari vya Marekani vimeripoti, wakinukuu vyanzo ambavyo havikutajwa vinafahamu suala hilo.
Inasemekana kuwa maajenti hao walipiga goti pamoja na wengine wakati wa maandamano huko Washington DC mwaka wa 2020.
Floyd, mtu mweusi, aliuawa na afisa wa polisi aliyepiga magoti kwenye shingo yake Mei mwaka huo, na hivyo kuzua gumzo duniani kote.
Kati ya maafisa 15 hadi 20 wanadhaniwa kufutwa kazi siku ya Ijumaa, ingawa idadi kamili haijulikani.
Shirikisho la maajenti wa FBI limelaani kusitishwa kazi kwao katika taarifa, likisema haki zao zimekiukwa. FBI ilikataa kuzungumzia ripoti hizo ilipofuatwa na BBC.
Wachambuzi kadhaa wa mrengo wa kulia walikuwa wamekosoa maafisa wa polisi ambao walionekana wamepiga magoti kwenye mitandao ya kijamii wakati huo.
Lakini wafuasi wao wanasema kupiga magoti ilikuwa mbinu ya kupunguza mivutano na waandamanaji, badala ya kuashiria kwamba mawakala walikubaliana na maoni yao.
Kitendo hicho kiligeuka kuwa ishara ya upinzani dhidi ya ubaguzi wa rangi, kwani picha za mtandaoni zilionesha muuaji wa Floyd, afisa wa polisi mweupe Derek Chauvin, akipiga magoti shingoni mwake huku akiwa amebanwa sakafuni kwa zaidi ya dakika tisa.
Uchunguzi rasmi uligundua Floyd alifariki kutokana na mshtuko wa moyo uliosababishwa na kubanwa kwa shingo.
Kwa sasa Chauvin anatumikia kifungo cha miaka 22 na nusu kwa mauaji ya Floyd. Kupiga goti pia kulitumika Marekani kama maandamano dhidi ya dhuluma ya rangi na ukatili wa polisi kabla ya mauaji ya Floyd, hasa na mchezaji wa zamani wa NFL Colin Kaepernick.
Polisi wavunja genge linalosafirisha Wakenya ili kuipigania Urusi nchini Ukraine

Zaidi ya watu 20 wameokolewa nchini Kenya kutoka kwa watuhumiwa wa ulanguzi wa binadamu ambao uliwarubuni kwa ofa za kazi nchini Urusi lakini walinuia kuwatuma kupigana nchini Ukraine, polisi walisema.
Inafuatia uvamizi ulioongozwa kijasusi kwenye nyumba ya makazi nje kidogo ya mji mkuu, Nairobi, ambapo maafisa walinasa vifaa vya kuajiri, hati za kusafiri, na barua za ofa ya kazi.
Mshukiwa mmoja, anayetuhumiwa kuratibu safari ya wahasiriwa kwenda Urusi mnamo Septemba na Oktoba, amekamatwa. Alifikishwa mahakamani, jambo ambalo lilimruhusu kuzuiliwa kwa siku 10 huku polisi wakikamilisha uchunguzi wao.
Kumekuwa na wasiwasi kuhusu kuongezeka kwa idadi ya Wakenya wanaosafirishwa nje ya nchi kwa ahadi za uongo za kazi.
Mwanariadha mchanga wa Kenya alikamatwa hivi karibuni nchini Ukraine, akisema alidanganywa kujiunga na jeshi la Urusi.
Mamlaka zilisema kukamatwa siku ya Jumatano kulifuatia operesheni iliyoratibiwa ya mashirika mengi ya usalama inayolenga mtandao wa wahalifu, ambao umekuwa ukitumia pesa nyingi kutoka kwa watu wanaotafuta kazi nchini Kenya.
Jumla ya Wakenya 22 walipatikana katika orofa moja katika eneo la Athi River, “wakisubiri kupelekwa hadi Urusi”.
Polisi walisema “kundi hilo la ajabu la ulanguzi” lilikuwa likiwarubuni Wakenya kwa ofa za kazi huko Moscow, na kuwatuma tu kupigania jeshi la Urusi nchini Ukraine.
Wapelelezi walisema waathiriwa walifichua kuwa walikuwa wametia saini kandarasi na wakala wa uajiri wa ng’ambo ambao hawakutajwa, wakijitolea kulipa hadi $18,000 (£13,000) kwa visa, usafiri, malazi, na vifaa vingine.
Baadhi ya waathiriwa pia walionesha kuwa tayari walikuwa wamelipa amana za $1,500.
Mara baada ya kuajiriwa, polisi walisema wengi wanarudi nyumbani wakiwa wamejeruhiwa, wakiwa na kiwewe, au katika visa vingine, hawarudi tena.
Wakenya wawili wanaripotiwa kurejea hivi karibuni, huku mmoja kwa sasa amelazwa katika hospitali ya jiji.
Afisa mkuu wa wizara ya mambo ya nje hivi karibuni alisema serikali ya Kenya inafuatilia ripoti za raia kadhaa wa Kenya ambao walidaiwa kusafirishwa kwenda Urusi na sasa wanashikiliwa kama wafungwa wa vita nchini Ukraine.
Raia wa Somalia, Sierra Leone, Togo, Cuba na Sri Lanka, miongoni mwa wengine, kwa sasa wanazuiliwa katika kambi za wafungwa wa vita vya Ukraine, Petro Yatsenko, msemaji wa Ukraine kuhusu matibabu ya wafungwa wa vita, hivi karibuni aliiambia BBC.
Hata hivyo, akizungumzia wafungwa wengine wa vita, aliongeza kuwa “nchi nyingi za Afrika zinaonesha nia ndogo ya kurejea kwa raia kama hao na hazitaki kuwarudisha”.
Marekani yafutilia mbali visa ya rais wa Colombia kutokana na matamshi ya ‘uchochezi’

Marekani imesema itamnyima viza Rais wa Colombia Gustavo Petro, baada ya kuwataka wanajeshi wa Marekani kutomtii rais wa Marekani Donald Trump wakati wa matamshi yake katika mkutano wa hadhara mjini New York.
Wizara ya Mambo ya Nje ilielezea maoni ya Petro katika maandamano ya mitaani yanayounga mkono Wapalestina siku ya Ijumaa kama “ya kutojali na ya uchochezi”.
Kiongozi huyo wa Colombia alikuwa Marekani kwa ajili ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, ambapo mapema wiki hii alitoa wito wa kufanyika uchunguzi wa uhalifu kuhusu mashambulizi ya anga ya utawala wa Trump dhidi ya boti zinazodaiwa kusafirisha dawa za kulevya katika visiwa vya Caribbean.
Tayari alikuwa njiani kurejea Bogota wakati Marekani ilipotangaza kufuta visa yake, vyombo vya habari vya Colombia vinaripoti.
Petro alichapisha video kwenye mitandao ya kijamii akihutubia umati mkubwa kupitia megaphone kwa Kihispania siku ya Ijumaa.
Alitoa wito wa kuundwa kwa “jeshi la wokovu duniani, ambalo kazi yake ya kwanza ni kuikomboa Palestina”.
“Ndio maana, kutoka hapa New York, ninawaomba wanajeshi wote katika Jeshi la Marekani wasielekeze bunduki zao kwa wanadamu,” alisema.
“Usiitii amri ya Trump! Tii amri ya ubinadamu!” Petro aliongeza: “Kama ilivyotokea katika Vita vya Kwanza vya Dunia, nataka vijana, wana na mabinti wa wafanyakazi na wakulima, wa Israeli na Marekani, waelekeze bunduki zao si kwa ubinadamu, bali kwa madhalimu na kwa mafashisti.”
Wizara ya mambo ya nje ya Marekani ilikosoa vikali matamshi hayo, ikisema “amewataka wanajeshi wa Marekani kutotii amri na kuchochea ghasia”. Iliandika kwenye mtandao wa kijamii kwamba kufutwa kwa visa yake “kutokana na vitendo vyake vya uzembe na vya uchochezi”.
Wapalestina 40 wauawa katika Ukanda wa Gaza

Wapalestina 40 wameuawa katika eneo lote la Ukanda wa Gaza tangu alfajiri ya Jumamosi, “huku mashambulizi makali ya anga na ubomoaji wa nyumba yakiendelea” na vikosi vya Israel, kwa mujibu wa shirika la habari la Palestina WAFA.
Duru za kitabibu ziliiambia WAFA kuwa “mashahidi 40 wameuawa katika Ukanda wa Gaza tangu alfajiri ya leo.
Mashahidi tisa walifika katika Hospitali ya Al-Shifa, 14 katika Hospitali ya Al-Ahli Arab Baptist, 10 katika Hospitali ya Al-Awda, mmoja katika Hospitali ya Nasser, na sita katika Hospitali ya Al-Aqsa.”
Alibainisha kuwa “miongoni mwa mashahidi, kulikuwa na shahidi aliyekuwa akitafuta msaada katika eneo la Netzarim.”
Rais wa Marekani Donald Trump alisema Ijumaa kuwa mazungumzo kuhusu Gaza na nchi za Mashariki ya Kati yalikuwa ya kina.
Ameongeza kuwa Israel na Hamas wanafahamu kuhusu mazungumzo hayo, na kusema kuwa mazungumzo hayo yataendelea kadiri inavyohitajika ili kufikia makubaliano.
Trump alikutana na viongozi na maafisa kutoka nchi kadhaa zenye Waislamu wengi wiki hii kujadili hali ya Gaza, ambayo inashambuliwa na mshirika wa Washington, Israel.
Mjumbe Maalumu wa Marekani Steve Witkoff alisema kuwa Trump aliwasilisha mapendekezo kwa viongozi hao, ikiwa ni pamoja na mpango wa amani wa Mashariki ya Kati wenye vipengee 21.
Watu 100 wahofiwa kupoteza maisha kwa kufukiwa mgodini Nigeria
Takribani watu 100 wanahofiwa kufariki dunia baada ya kufukiwa na vifusi vya mgodi wa dhahabu katika jimbo la Zamfara, kaskazini magharibi mwa Nigeria.
Mgodi huo uliopo katika eneo la Kadauri, wilaya ya Maru, uliporomoka Alhamisi wakati wachimbaji wa kawaida wakifanya kazi chini ya ardhi, kwa mujibu wa Reuters.
Operesheni za uokoaji ziliendelea hadi Ijumaa. Sanusi Auwal, mkazi wa eneo hilo aliyehusika katika juhudi za uokoaji, alisema kwamba miili 13 tayari imetolewa kutoka kwenye mabaki ya mgodi, ikiwa ni pamoja na mwili wa binamu yake.
“Zaidi ya wachimbaji 100 walikuwepo chini wakati mgodi ulipoporomoka,” Auwal alisema kwa simu. “Tuna bahati tumeokolewa hai. Tulikuwa zaidi ya watu 100, sisi 15 tu ndio tuliookolewa,” alisema Isa Sani, ambaye kwa sasa anapatiwa matibabu kutokana na majeraha.
Muhammadu Isa wa chama cha wachimbaji wa jimbo la Zamfara alithibitisha tukio hilo, akiongeza kwamba baadhi ya waokoaji walipata Dhoruba wakati wakijaribu kutoa waathirika.
Msemaji wa polisi wa Zamfara, Yazid Abubakar, hakutoa maelezo alipoombwa kwa simu na ujumbe wa maandishi kutoa maoni yake. Uchimbaji haramu ni wa kawaida Zamfara, ambapo makundi yenye silaha mara nyingi hushikilia uongozi wa migodi ya dhahabu, hali inayochochea vurugu na ajali zinazosababisha vifo.
Nuno Santo kumrithi Graham Potter West Ham

West Ham inatarajiwa kumtangaza aliyekuwa kocha wa Nottingham Forest, Nuno Espirito Santo, kuwa kocha mkuu mpya baada ya kumtimua Graham Potter.
Nuno, 51, anatarajiwa kuiongoza timu hiyo katika mchezo wa ligi kuu dhidi ya Everton Jumatatu, kufuatia mazungumzo mazuri aliyofanya na uongozi wa klabu hiyo.
Potter amefungashiwa virago Jumamosi asubuhi baada ya kuiongoza timu hiyo kwa miezi minane, na kuiacha timu hiyo ikiporomoka hadi nafasi ya 19 kwenye msimamo wa ligi.
Chini ya Potter, West Ham ilipata alama tatu pekee katika mechi tano za kwanza za msimu huu. Uongozi wa klabu ulisema mabadiliko yalikuwa ya lazima ili kuinusuru haraka timu hiyo.
Nuno alitimuliwa na Nottingham Forest msimu huu baada ya kuiongoza katika mechi tatu pekee, ingawa msimu uliopita aliwaongoza kufika nafasi ya saba, nafasi ya juu zaidi ya klabu hiyo tangu msimu wa 1994-95 na kuirejesha kwenye michuano ya Ulaya kwa mara ya kwanza baada ya miongo mitatu.
Uzoefu huo umeonekana kama nguzo muhimu katika jukumu jipya analolianaza London.
Kwa upande mwingine, Potter aliongoza West Ham katika mechi 25 pekee tangu alipoteuliwa Januari mwaka huu, akishinda sita, na timu kumaliza katika nafasi ya 14 msimu uliopita.
Licha ya kuamini alikuwa na uungwaji mkono wa bodi, matokeo na mwenendo wa timu yameelezwa kushindwa kutimiza matarajio ya klabu.
Mchambuzi wa soka na nahodha wa zamani wa Wales, Ashley Williams, aliambia BBC kwamba mashabiki wa West Ham wanataka kuona timu yenye juhudi na ujasiri uwanjani.
Alisema Nuno anaweza kuibadilisha klabu hiyo na kuipa nguvu upya, akiongeza kuwa chini ya Potter kikosi kilikuwa “hoi” na rahisi sana kushambuliwa na wapinzani.
Simbu azawadiwa nyumba na Rais Samia kwa ushindi wa dhahabu Tokyo

Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amemzawadia nyumba ya kuishi jijini Dodoma mwanariadha Alphonce Simbu, kufuatia ushindi wake wa medali ya dhahabu katika mashindano riadha ya dunia yaliyofanyika Tokyo wiki iliyopita.
Ushindi huo umeelezwa kama hatua muhimu kwa historia ya michezo nchini Tanzania, ambapo mara chache wanariadha wa taifa hilo wamefanikiwa kutwaa medali za kiwango cha juu katika mashindano ya kimataifa.
Akizungumza katika hafla ya kumpongeza Simbu iliyofanyika jijini Dar es Salaam katika Hoteli ya Hyatt Regency, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alisema Rais ameelekeza mchakato wa makabidhiano ufanyike haraka, mbele ya familia ya mwanariadha huyo.
“Mheshimiwa Rais anatoa zawadi ya nyumba jijini Dodoma, ambayo itakabidhiwa na Katibu Mkuu wa Wizara. Zoezi hilo lisichukue muda mrefu kuanzia leo,” alisema Majaliwa.
Ameongeza kuwa serikali inafurahia kuona vijana wa Kitanzania wakishiriki katika michezo ya kimataifa na kulipatia taifa heshima kupitia mafanikio makubwa wanayoyapata.
Simbu, ambaye amekuwa miongoni mwa wanariadha wanaopeperusha vyema bendera ya Tanzania katika riadha za kimataifa, alipokelewa kwa shangwe baada ya kurejea nyumbani akitokea Tokyo.
All Rights Reserved © The Cantona Group PLC||2025
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.