Trump aunga mkono mazungumzo ya kusitisha mapigano Gaza huku akikutana na Netanyahu

Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph

https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa

Rais wa Marekani Donald Trump amesema anafikiri mazungumzo ya kumaliza vita huko Gaza yamekuwa “yakiendelea vizuri” alipokuwa akimkaribisha Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu mjini Washington DC.

Trump pia alionyesha imani kuwa Hamas iko tayari kumaliza mzozo huo uliodumu kwa miezi 21.

“Wanataka kukutana na wanataka kuwa na usitishaji huo wa mapigano,” alisema katika matamshi ambayo hayakutarajiwa kwa waandishi wa habari katika Ikulu ya White House.

Mkutano huo umekuja baada ya duru za hivi punde za mazungumzo ya kusitisha mapigano yasiyo ya moja kwa moja kati ya Israel na Hamas nchini Qatar kumalizika bila mafanikio, ingawa mazungumzo yalitarajiwa kuendelea wiki hii.

Katika matamshi ya Jumatatu, Trump aliulizwa na mwandishi wa habari ni nini kinazuia makubaliano ya amani huko Gaza, na akasema: “Sidhani kama kuna kuna kizuizi. Nadhani mambo yanakwenda vizuri sana.”

Viongozi wote wawili waliulizwa kuhusu mipango inayowezekana ya kuwahamisha Wapalestina, huku Trump akisema ana ushirikiano kutoka nchi jirani za Israel.

Netanyahu, wakati huo huo, alisema anafanya kazi na Marekani katika kutafuta nchi ambazo “zitawapa Wapalestina maisha bora ya baadaye”. “Ikiwa watu wanataka kubaki, wanaweza kubaki, lakini kama wanataka kuondoka, wanapaswa kuondoka,” Netanyahu alisema.

Ofisi ya rais wa Palestina hapo awali ilikataa mipango ya kuwahamisha Wapalestina, ambayo ilidokeza kuwa ingekiuka sheria za kimataifa.

Netanyahu pia alionekana kudharau matarajio ya taifa kamili la Palestina, akisema kuwa Israel “daima” itaweka udhibiti wa usalama katika Ukanda wa Gaza.

All Rights Reserved © The Cantona Group PLC||2025


Discover more from cantonadigital

Subscribe to get the latest posts sent to your email.

Leave a comment