Radio Fortune Africa -Na Cantona Joseph
https://zeno.fm/radio/radio-fortune-africa
Baraza la kikatiba nchini Msumbiji, hapo jana, 24 Disemba 2024 lilithibitisha ushindi wa chama tawala kufuatia uchaguzi wa mwezi Octoba uliogubikwa na utata, upinzani ukidai kulikuwa na udanganyifu hali iliyosababisha maandamano ya nchi nzima.
Kufuatia uamuzi huu hofu kubwa imetanda ndani na nje ya nchi hiyo ambapo punde baada ya tangazo la baraza la kikatiba, kuliripotiwa makabiliano kati ya wafuasi wa upinzani na idara za usalama kwenye baadhi ya miji.
Awali hata kabla ya uamuzi wenyewe, upinzani ulitishia kuitisha maandamano na migomo ya nchi nzima kupinga kile unasema kupokwa kwa demokrasia na utashi wa raia.
Nchi ya Marekani na washirika wake, zimetoa wito wa utulivu baada ya baraza hilo kuthibitisha ushindi wa mgombea wa chama tawala Daniel Chapo, aliyetajwa kupata asilimia 65 ya kura zote tofauti na takwimu zilizokuwa zimetangazwa na tume ya uchaguzi iliyodai alipata asilimia 71.

Aidha kwa upande wa kinara wa upinzani Venancio Mondlane ambaye kwa sasa yuko uhamishoni, matokeo yake yalibadilishwa kutoka asilimia 20 alizopewa na tume ya uchaguzi hadi asilimia 24.
Madai ya upinzani kuibiwa kura pamoja na uchaguzi wenyewe kuwa na dosari, yaliungwa mkono na baadhi ya waangalizi wa ndani na wale wa kimataifa waliotaka zoezi kurejelewa upya.
All Rights Reserved © Cantona Group PLC||2024
Discover more from cantonadigital
Subscribe to get the latest posts sent to your email.