Afrika Leo Jioni -Habari Kamili

BAADHI ya vyama tanzu katika muungano wa Azimio la Umoja-One Kenya sasa vimeanzisha kampeni inayolenga kufanikisha kuondolewa kwa ODM kutoka muungano huo baada ya Raila Odinga kuamua kufanya kazi na serikali ya Rais William Ruto.

Viongozi wa vyama vya; Wiper, Jubilee, DAP-K na PNU wamefichua kuwa mwenyekiti wa Baraza Kuu la Azimio, Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta ameitisha kikao ambacho kitatumiwa kupitisha pendekezo la kufurushwa kwa ODM na kuratibu mustakabali wa Azimio.

Wakiongozwa na kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, viongozi hao wanashikilia kuwa ODM haifaa kuendelea kusalia ndani ya Azimio ilhali wanachama wake wanahudumu katika serikali ya Rais Ruto.

“Haitawezekana kwa ODM kuhakiki utendakazi wa serikali ilhali wanachama wake wanashikilia nyadhifa kuu za uwaziri katika serikali hiyo hiyo. Ingawa ni haki ya wenzetu kuamua kufanya kazi na serikali au mrengo wa upinzani, itabidi chama chao kuamua kusalia upinzani au kuwa sehemu ya serikali,” Bw Musyoka akasema Jumapili, Agosti 19, 2024 alipoandamana na wenzake kuhudhuria ibada katika Kaunti ya Kirinyaga.

“Suala hili ni miongoni mwa yale yatakayojadiliwa katika mkutano ujao wa Baraza Kuu la Azimio utakaoongozwa na mwenyekiti wetu Uhuru Kenyatta,” akaongeza.

Hata hivyo, Bw Musyoka hakutaja siku wala tarehe ya kufanyika kwa mkutano huo. Hata hivyo, duru zimeiambia Taifa Dijitali kuwa mkutano huo utafanyika wiki hii.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Jubilee Jeremiah Kioni ameisuta ODM kwa kuendeleza undumakuwili katika nyanja ya siasa na uongozi, hali aliyosema ni kinyume cha moyo wa Katiba ya sasa.

“ODM haiwezi kuwa ndani ya serikali na wakati huo huo inadai ingali katika upinzani. Hii ni kwa sababu wanachama wake wanashikilia nyadhifa za uwaziri katika serikali hii ya William Ruto,” akasema Mbunge huyo wa zamani wa Ndaragua.

Bw Kioni alisema ODM imekosea kwa kushirikiana na serikali, ambayo kwa mtazamo wake, inanyanyasa Wakenya.

“Katika mkutano ujao wa Baraza Kuu la Azimio, tutataka ODM iondolewe Azimio ili tupate nafasi ya kuweka mikakati ya kuihakiki serikali hii ya Kenya Kwanza,” Bw Kioni akasema.

“Kwa kuvuta viongozi wa upinzani upande wake, Rais William Ruto ameonyesha wazi kuwa anapania kuendelea kuwadhulumu Wakenya. Hatuwezi kukubali kuendelea kwa mwenendo huo,” akaongeza.

Kiongozi wa DAP- Kenya Eugene Wamalwa alisema Rais Ruto anaendesha serikali inayokiuka Katiba kwa sababu inashirikisha viongozi wa upinzani bila kufuata mwongozo wa kisheria.

“Baraza la mawaziri lililoundwa juzi na Rais William Ruto sio halali kwa sababu halitambuliwi na Katiba yetu. Hili sio baraza la mawaziri chini ya serikali ya muungano, serikali ya mseto au ile inayofuata mifumo inayotambuliwa na sheria yoyote nchini au sheria za kimataifa. Kwa hivyo, hii sio serikali halali,” akasema Bw Wamalwa.

“Ikiwa wenzetu wa ODM wanataka kushirikiana na serikali kama hii, basi waondoke Azimio,” akaongeza Bw Wamalwa, ambaye mbunge wa zamani Saboti na aliyehudumu kama Waziri wa Ulinzi chini ya serikali ya Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta.

Migawanyiko ilianza kushuhudiwa katika muungano wa Azimio baada ya Rais Ruto kuteua viongozi watano wa ODM katika baraza lake jipya la mawaziri.

Walioteuliwa ni manaibu wa Bw Odinga; Wycliffe Oparanya na Ali Hassan Joho, aliyekuwa Mwenyekiti wa zamani wa kitaifa John Mbadi, aliyekuwa Katibu wa Masuala ya Kisiasa James Opiyo Wandayi na alikuwa mwanachama wa Kamati Shirikishi ya Kusimamia Uchaguzi katika ODM Beatrice Askul Moe.

Azimio
Kutimuliwa
raila odinga
Uhuru Kenyatta

BAADHI ya wadau wamepinga mpango wa serikali wa kurejesha baadhi ya mapendekezo katika Mswada wa Fedha wa 2024 uliotupiliwa mbali Juni 28 kufuatia maandamano ya vijana wa Gen Zs.

Rais William Ruto Jumamosi, Agosti 17, 2024 alidokeza kuwa serikali inalenga kurejesha baadhi ya sehemu za mswada huo ili kuisadia serikali kupata angalau Sh130 bilioni za kufadhili utekelezaji wa miradi ya maendeleo kama vile ujenzi wa barabara.

Naye Waziri wa Fedha John Mbadi amedokeza kuwa wizara yake itarejesha pendekezo la utozaji ushuru wa mazingira kwa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje (Eco levy), kama mswada maalum.

Kauli hizi za Rais Ruto na Waziri Mbadi zimewafanya wadau katika sekta mbali kuingiwa na wasiwasi kwamba ni kisingizio cha kurejeshwa kwa baadhi ya mapendekezo ya ushuru yatakayoumiza wananchi.

Chama cha Wauzaji Magari yanayotumia Stima Nchini (Emak) ndicho cha kwanza kuibua hofu hiyo, kikisema kurejeshwa kwa ushuru kwa sekta hiyo kutayumbisha ununuzi na matumizi ya magari ya kutumia kawi hiyo (EVs).

Mwenyekiti wa chama hicho Hesbon Mose ameelezea hofu kwamba serikali itarejesha ushuru wa ziada ya thamani (VAT) ya asilimia 16 kwa mabasi na pikipiki zinazotumia stima uliopendekezwa katika Mswada wa 2024.

Mswada huo pia uliondoa msamaha waVAT kwa vifaa vinavyotumiwa kuzalisha kawi kutokana na upepo na jua.

“Wakati huu bei ya magari yanayotumia stima (EVs) ni kati ya asilimia 10 na asilimia 15 ghali, ikilinganishwa na magari yenye injini ya kutumia petroli na dizeli (ICEs). Ukianzisha ushuru wa VAT na aina zingine za ushuru kwa EVs, bei ya magari hayo itaongekeza kwa asilimia 35 kuliko magariya ICEs,” akasema Bw Mose.

Aliongeza kuwa sekta hiyo, ya magari yanayotumia stima, ilivutia uwekezaji wa kima cha Sh13 bilioni mwaka jana, 2023, akisema kiwango hicho kitashuka ikiwa ushuru wa VAT utaanzishwa.

“Kati ya mwaka wa 2022 na 2023, tulishuhudia nyongeza ya asilimia 500 katika ununuzi wa pikipiki kwa sababu vyombo hivi vya usafiri havikutozwa ushuru wa VAT au aina nyingine za ushuru. Kurejesha ushuru huu katika sekta hii kutadumaza ukuaji wake na uwezo wake wa kutoa nafasi za ajira,” Bw Mose akasema.

Kwa upande wake, mwenyekiti wa Chama cha Waagizaji Bidhaa na Wafanyabiashara Wadogo Nchini (ISTA) Samuel Karanja amepinga mpango wa Waziri wa Fedha John Mbadi wa kurejesha ushuru kwa bidhaa zilizopakiwa kwa plastiki na vitu vingine vinavyoharibu mazingira.

Kulingana na Bw Karanja, kurejeshwa kwa ushuru wa “Eco Levy) kutachangia kuongezeka kwa bei ya bidhaa nyingi za kimsingi.

“Bidhaa zinazotumika nchini na raia wa kawaida ni zile zilizoagizwa kutoka ng’ambo na ambazo hupakiwa kwa vifaa vinavyoathiri mazingira kama vile plastiki. Kwa hivyo, ikiwa Waziri Mbadi atarejesha ushuru wa asilimia 10 kwa bidhaa zilizoagizwa nje, bei ya bidhaa hizo zitapanda. Hatua hiyo bila shaka itaongeza gharama ya maisha,” Bw Karanja akaambia Taifa Dijitali kwa njia ya simu.

“Kurejeshwa kwa ushuru huo kutachangia kuongezeka kwa gharama ya maisha na mahasla ndio wataumia,” akaongeza.

Lakini Bw Mbadi anashikilia kuwa kujeshwa kwa ushuru wa “Eco-levy) kutaisaidia serikali kupata pesa za kufadhili mipango ya utunzaji mazingira.

“Ikiwa bidhaa zinazoingizwa nchini zimepakiwa vitu kama plastiki zinazoharibu mazingira, sharti tutafute pesa za kuzuia uharibifu huu,” Bw Mbadi akasema Jumatatu, Agosti 19, 2024 kwenye mahojiano na wanahabari afisini mwake.

Akiongea katika eneo bunge la Malava, Kaunti ya Kakamega, Rais Ruto alielezea wazi nia ya serikali yake kurejesha baadhi ya mapendekezo ya mswada wa Fedha uliokataliwa, kuhusu ushuru, ili kupata pesa za kufadhili miradi ya maendeleo.

“Ingawa Mswada wa Fedha wa 2024 ambao ungetusaidia kupata Sh347 bilioni, hatutakufa moyo. Tutarejea bungeni tena na kuwasilisha mapendekezo ya kutusaidia kupata pesa za kutusaidia kutekeleza miradi ya maendeleo. Kama mzazi, ikiwa unapanga kupata mtoto lakini kwa bahati mbaya mimba ikaharibika, hauvunjiki moja, unajaribu tena. Nimemwambia Bw Malulu (mbunge wa Malava Malulu Injendi) na wabunge wetu kwamba tutarejea bunge na mapendekezo kadhaa ya kutuwezesha kupata pesa za kujenga barabara na kuunganisha stima,” Dkt Ruto akasema.

Wakati huo huo, Wakenya wanafaa kujiandaa kwa kupanda kwa bei ya chakula kufuatia uamuzi wa Mamlaka ya Kilimo na Chakula (AFA) kuanza kutekeleza ushuru wa asilimia mbili (2) kwa bidhaa za chakula zilizoagizwa kutoka nje kama vile mahindi na mchele.

AFA imepuuza kilio cha wafanyabiashara wanaopinga hatua hiyo wakisema itaongeza gharama ya kuendesha biashara ya bidhaa za chakula, kando na kufanya bei ya bidhaa hizo kuwa ghali mno.

PENDEKEZO la baadhi ya wanasiasa wa ODM kuwa kinara wao Raila Odinga awanie urais mnamo 2027 ni hadaa tu ili wamtumie kupata nyadhifa zao.

Kwa sasa juhudi zote zinastahili kuelekezwa kwa kampeni ya Bw Odinga kunasa uenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika (AUC), badala ya kushiriki siasa za 2027.

Mwishoni mwa wiki jana, Gavana Simba Arati wa Kisii na mwenzake wa Mombasa, Abdulswamad Sheriff Nassir, walidokeza kuwa Bw Odinga bado anatosha kuwania urais katika uchaguzi wa 2027.

MaBw Arati na Nassir waliteuliwa kama manaibu viongozi wa Bw Odinga katika ODM, baada ya ycliffe Oparanya na Hassan Joho kujiuzulu ili kutwaa nafasi za uwaziri katika serikali ya Kenya Kwanza.

Kabla ya uteuzi huo, Bw Arati alikuwa akihudumu kama naibu mwenyekiti wa ODM, japo Bw Nassir hakuwa na wadhifa wowote chamani kando na kuwa jemedari halisi wa Bw Odinga.

Mwanzo, magavana hawa wawili wafahamu kuwa kinara huyo wa upinzani kwa sasa anaelekea kupoteza umaarufu hasa miongoni mwa kizazi cha sasa cha vijana, Gen Z, ambacho kinamlaumu kwa kusambaratisha mchakato wao wa mageuzi.

Gen Z walikuwa wakiendeleza maasi ya kubandua utawala wa Rais William Ruto, lakini ni dhahiri yamefifia baada ya Bw Odinga kuanzisha ushirikiano na Rais.

Iwapo vijana watachukua kura kwa wingi na 2027 waamue kuondoa wanasiasa wakongwe na wale wanaohisi wameshindwa kustawisha taifa, basi Bw Odinga na Rais Ruto hawatakuwa na lao.

Kuwaambia Wakenya kwamba ODM haishirikiani kivyovyote na utawala wa sasa ni hadaa tupu.

Itakumbukwa kuwa Bw Odinga alipinga vikali uteuzi wa marehemu Joseph Nkaissery kwenye Baraza la Mawaziri la utawala wa Jubilee mnamo Desemba 2014.

Wakati huo alisema hatua ya kuteua wabunge au viongozi wa upinzani ililenga kulemaza upinzani ili usitekeleze wajibu wake kuiweka serikali kwenye darubini.

Sasa kipi kimebadilika kiasi cha yeye kusema amekodisha wandani wake walioteuliwa mawaziri serikali eti wasaidie kuokoa chombo cha Kenya Kwanza kilichokuwa kikizama?

Pili, Bw Odinga atakuwa ametimu miaka 82 na japo urais hauna kigezo cha umri, ujana umempa kisogo na mwili hautakuwa na nguvu za kustahimili kukurukakara za kupiga kampeni na kisha kuongoza taifa; heri aunge mkono mgombea mwingine atakayemrithi.

Kigogo huyo wa kisiasa ameshindwa urais mara tano; mara nne kati yazo amesisitizia wafuasi wake kuwa alichezewa shere.

Mara nyingi wanasiasa wametumia jina la ‘baba’ kupata viti lakini yeye anashindwa. Hii ni mbinu nyingine ambayo sasa inatumiwa na magavana Arati na Nassir.

Bw Odinga asipowahi kiti cha AUC asiwanie urais Kenya bali apishe mwaniaji mwingine. Kama hana kismati kuwa rais hata akiwania 2027 bado hatashinda.

Wawili hawa wanajua kuwa ODM itakuwa imara tu kama Raila yupo debeni huku nao wakilenga kuhifadhi viti vyao vya ugavana. Wanajua kuwa ODM isipokuwa imara na Raila akiwa AUC basi wanaweza kushindwa kupata muhula wa pili.

Kile Raila anastahili kufanya ni kumakinikia kampeni ashinde AUC ili ahudumu kwa miaka minne na akiona kuwa bado yupo ngangari atetee wadhifa huo mnamo 2028.

Asipowahi kiti cha AUC basi asiwanie urais bali apishe mwaniaji mwengine ambaye atazingatia maslahi ya ngome zake za kisiasa. Kama hakuandikiwa urais hata akiwania 2027 bado hataupata.

Mnamo 2027 asiwanie urais bali atumie ushawishi wake kuunga mkono mrengo utakaoshinda kwa sababu ni wazi kivyovyote vila yeye huishia kuwa serikalini baada ya uchaguzi.

PENGO la uongozi limetokea katika serikali ya Kaunti ya Uasin Gishu baada ya Naibu Gavana John Barorot kujiuzulu ghafla.

Bw Barorot alitoa tangazo hilo Jumatatu, Agosti 19, 2024 wakati wa mkutano wa maafisa wa ngazi za juu katika kaunti hiyo ulioongozwa na Gavana Jonathan Bii katika mkahawa mmoja jijini Eldoret.

Naibu huyo wa Gavana amejiuzulu siku chache baada ya kufutilia mbali uvumi kwamba anapania kujiondoa.

Hata hivyo, uvumi huo ulionekana kupata mashiko Jumatano wiki iliyopita alipokwepa kuhudhuria sherehe ya kupandishwa hadhi ya manisipaa ya mji wa Eldoret kuwa jiji.

Licha ya kupuuzilia mbali uvumi kuhusu kujiuzulu kwake, Bw Barorot hakueleza ni kwa nini alifeli kuhudhuria hafla hiyo iliyoongozwa na Rais William Ruto katika uwanja wa Eldoret Sports Club.

Dkt Ruto alikuwa ameandamana na naibu wake, Rigathi Gachagua.

Duru zinasema kuwa uhusiano kati ya Gavana Bii na Mhandisi Barorot haujakuwa mzuri katika siku za hivi karibuni.

Inakisiwa kuwa hiyo ndio sababu naibu huyo wa Gavana amekuwa akijitenga na shughuli kuu za Kaunti ya Uasin Gishu, haswa maandalizi ya sherehe ya kuipandisha hadhi Eldoret kuwa jiji la tano nchini Kenya.

Kulingana na Sehemu ya 33 ya Sheria ya Serikali za Kaunti, Gavana anapaswa kuteua Naibu Gavana mpya siku 14 baada ya nafasi hiyo kusalia wazi, kwa njia zinatombuliwa kisheria.

Njia hizo ni; kifo, kuondolewa afisini, kushindwa kutekeleza majukumu ya afisi au kujiuzulu.

NAIBU Rais Rigathi Gachagua amewaonya wanasiasa wa Mlima Kenya ambao hakuwataja majina, ambao anasema wamekuwa wakipanga njama dhidi yake.

Kwa sababu hiyo, Naibu Rais amesema hatawaunga mkono katika uchaguzi mkuu wa 2027.

Bw Gachagua alisema wanaomtesa watamtafuta 2027, na ikifika wakati huo, atazima simu yake wasimfikie.

Alifichua kuwa watu wengi aliowasaidia wakati wa Uchaguzi Mkuu uliopita ili kuchaguliwa, wamempa kisogo na wanapanga njama za kumporomosha.

“Kuna watu wengi niliowasaidia wakati wa kampeni wakashinda viti wanavyoshikilia leo. Lakini niligundua kuwa ni watu wale wale wanaopanga kuniangusha na kunishambulia,” akasema Bw Gachagua.

“Lakini jambo zuri ni kwamba uchaguzi unadumu kwa miaka mitano tu. Kwa hiyo watu hao watahitaji msaada wangu 2027. Nitawaunga mkono wale wanaoniunga mkono kwa sasa. Kuna watu wanasaidiwa na wanasaliti wengine. Mmoja wao hivi majuzi alikuwa na ujasiri wa kuuliza kwa nini sitambui kazi yake kila ninapotembelea eneo bunge lake,” aliongeza.

Bw Gachagua ambaye alizungumza sana kuhusu usaliti na udanganyifu katika siasa, hasa ndani ya muungano unaotawala wa Kenya Kwanza alisema : “Mimi binafsi nimeshuhudia siasa za usaliti na ujanja. Watu ambao nilisaidia kuchaguliwa ni baadhi ya watu ambao wamenisaliti. Lakini siasa ni hivyo, lazima uwe na uvumilivu.”

Akizungumza Jumamosi, wakati wa kumbukumbu ya marehemu David Chepkwony, mume wa Mbunge wa Njoro Charity Kathambi, Gachagua, alisema kuwa katika siasa, watu huwa na tabia ya kusahau kirahisi baada ya kupanda ngazi licha ya kusaidiwa na watu kufikia kiwango cha kuwatusi.

Alisikitika kuwa wanasiasa ni wepesi kuwasahau waliowasaidia kupanda ngazi lakini badala ya kuwaheshimu wanaanza kuwatukana, wakisahau uchaguzi ni baada ya miaka mitano.

Bw Gachagua hata hivyo alisema kuwa ataendelea kuwa rafiki na kufanya kazi na wale walio na ari ya kufanikisha na kusaidia mwananchi wa kawaida waliomchagua mamlakani.

Ufichuzi huo unajiri huku muungano unaotawala ukikumbwa na mzozo wa ndani, kukiwa na hali ya kutoelewana kati ya Rais William Ruto na naibu wake Rigathi Gachagua.

Bw Gachagua amekuwa akiwasuta baadhi ya viongozi ambao anawashutumu kwa kuhujumu juhudi zake za kuunganisha eneo la Mlima Kenya.

Haya pia yanajiri huku kukiwa na madai ya kumuondoa madarakani Bw Gachagua, mchakato unaosemekana kuongozwa na wabunge kutoka eneo la Mlima Kenya.

Wiki iliyopita, aliyekuwa Katibu Mkuu wa United Democratic Alliance (UDA) Cleopas Malala alishutumu maafisa wakuu wa chama kwa kupanga kumtimua Naibu Rais Rigathi Gachagua.

Bw Malala alilaumu Kiongozi wa Wengi Kimani Ichung’wa na Gavana wa Embu Cecily Mbarire kwa masaibu yake.

Huku akitaja kutimuliwa kwake ‘kinyume cha sheria’, mwanasiasa huyo mwenye msimamo mkali alidai kuwa wawili hao pamoja na washirika wengine walipanga njama ya kumuondoa kwanza, kabla ya kushinikiza kutimuliwa kwa Gachagua.

Cleophas Malala
Naibu Rais Rigathi Gachagua
Serikali ya Kenya Kwanza
Wanasiasa wa Mlima Kenya

KIONGOZI wa Chama cha Wiper Kalonzo Musyoka ameanzisha mikakati ya kisiasa inayolenga kuunganisha ngome yake ya Ukambani na Mlima Kenya na ambayo hatimaye itaishia jamii ya Wakamba kujiunga na muungano wa Gema unaoleta pamoja jamii za Gikuyu, Embu, Meru.

Duru zinasema kuna uwezekano wa Bw Musyoka kuungana na Bw Gachagua katika uchaguzi mkuu ujao, hatua ambayo wadadisi wanasema inaweza kupiga jeki azma ya urais ya kiongozi huyo wa Wiper akiungwa na Gema.

Bw Musyoka anataka kutumia hali ya sasa ya malalamishi ya wakazi wengi wa eneo la Mlima Kenya dhidi ya Rais William Ruto kwa kushindwa kutimiza ahadi za kabla ya uchaguzi mkuu wa 2022 na tetesi za njama ya kumhujumu Naibu Rais Rigathi Gachagua ili kujipendekeza katika eneo hilo kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Makamu rais wa zamani ambaye anaongoza mrengo wa upinzani wa Azimio baada ya wanasiasa wanne wakuu kutoka chama cha ODM cha Bw Raila Odinga kuteuliwa kuwa Mawaziri katika utawala wa Ruto amezuru kaunti za Kiambu, Nyeri, Kirinyaga na Embu kama sehemu ya mikakati yake.

Seneta wa Kitui Enoch Wambua, mshirika wa karibu wa Bw Musyoka, aliambia Taifa Leo kwamba ajenda yao ni kuhakikisha eneo la Ukambani linamuunga mkono Bw Musyoka na kuunganisha eneo hilo na Gema.

“Hivi karibuni kutakuwa na sherehe kubwa ya kurudisha mto kwenye mkondo wake. Tumetenganishwa na kaka na dada zetu ili kudhulumiwa. Ni wakati wa kurejea na kudai nafasi yetu halali,” akasema Bw Wambua.”Tutapigana vita vyovyote kuhakikisha tunachukua nafasi yetu halali na kupata sehemu yetu ya haki ya rasilimali. Tumeanza kuungana na ndugu zetu kutoka mlimani na nchi itakuwa ikishuhudia mengi zaidi.”

Aliyekuwa Gavana wa Kiambu Ferdinand Waititu, ambaye amekuwa akihudhuria baadhi ya hafla za Bw Musyoka maeneo ya Mlima Kenya, alithibitisha kwamba kuna mipango ya kuifanya jamii ya Wakamba kuwa sehemu ya GEMA.

Alimtaja Bw Musyoka kuwa mwanasiasa aliye na rekodi safi, na kutoa mfano wa ukuaji wa uchumi wakati wa utawala wa Rais Mwai Kibaki, ambapo Bw Musyoka alihudumu kama Makamu wa Rais kati ya 2008 hadi 2013.

“Tunataka kuwa na GEMA ya zamani kwa kuwajumuisha Wakamba. Mpango wetu ni jamii kuwa na sauti moja kisiasa kabla ya uchaguzi ujao,” akasema Bw Waititu.

Naibu Rais alisema katika mahojiano na televisheni wiki jana kwamba Bw Musyoka hajadhulumu eneo hilo.

Pia amekuwa akishinikiza kujumuishwa kwa eneo la Ukambani kuwa sehemu ya GEMA.

Naibu Gavana wa Machakos Francis Mwangangi alimtaja Bw Musyoka kuwa kiongozi wa kitaifa ambaye ana mitandao ya kisiasa kote nchini.

Alisema mpango huo ni kuunganisha ngome yake huku akifufua upya mitandao yake ya zamani katika maeneo yote ya nchi, ikiwa ni pamoja na eneo Mlima Kenya lililo na wapiga kura wengi.

“Kama mgombea urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2027, inabidi aunganishe ngome yake kwanza kabla ya kwenda kutafuta kuungwa mkono na maeneo mingine. Pia ameweka wazi kuwa atasimama na vijana, ambao wamelalamika kuhusu jinsi nchi inavyotawaliwa,” akasema Bw Mwangangi.

Kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka
Muungano wa GEMA
Naibu Rais Rigathi Gachagua
Rais William Ruto na Raila Odinga ODM

BAADHI ya vyama tanzu vya Muungano wa Azimio vinajipanga kutwaa jukumu rasmi la upinzani baada ya baadhi ya wanachama wa ODM kukabidhiwa majukumu katika serikali ya Kenya Kwanza.

Viongozi wa vyama vya Wiper Democratic Party, Jubilee na Democratic Action Party of Kenya (DAP-K) wamesema wanachukua hatua hii kuepusha taifa na uongozi wa udikteta.

Waliongozwa na vinara wa Azimio wakiwemo Kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, Katibu Mkuu wa Jubilee Jeremiah Kioni na Kiongozi wa DAP-K Eugene Wamalwa.

Vinara hawa walifichua kuwa wote wamekuwa na mikutano ya baraza la kitaifa na kuamua kusimama na Wakenya wanaopinga sera dhalimu za matozo ya juu ya ushuru.

“Hatuwezi kujiunga na serikali kwa sababu tumeamua kusimama na Wakenya. Tumewaruhusu waingie serikalini na tutabaki na kiongozi wetu Kalonzo Musyoka,” alitangaza Bw Wamalwa.

Pamoja nao katika kikao katika Kaunti ya Embu Jumapili, viongozi hao waliungana na aliyekuwa Gavana wa Kiambu Ferdinand Waititu.

Bw Waititu alisema kuwa aliwakilisha sehemu ya viongozi wa chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA) wasioridhishwa na sera za serikali.

Bw Waititu alisema wao wanajiunga na upinzani ili kushinikiza uwajibikaji serikalini.

Bw Kalonzo ambaye ametajwa kuwa ‘kiongozi’ wa muungano huo, amesema wameamua kuwa katika upande wa vijana ambao walifaulu kuzima Mswada wa Fedha wa 2024.

Amesema atapinga jaribio lolote la kuongeza ushuru uliopendekezwa katika mswada wa fedha ulioibua utata.

“Tumeona serikali ikiingiza kodi mpya kama ile ya Ushuru wa Ukarabati wa Barabara na nyongeza ya ada ya umeme. Haya ni matukio ambayo hatutayaruhusu,” aliwaka.

Kadhalika, Bw Kalonzo alisema kuwa muungano huo umepinga kuanzishwa kwa ada ya usafiri katika barabara kuu kama inavyopendekezwa na serikali.

“Kama unataka kuanzisha ada ya barabara, jengeni barabara zenu na usitoze ushuru zile zilizojengwa na Rais Mwai Kibaki. Mkifanya hivi mnavamia mifuko ya Wakenya na tutapinga mpango huo,” Bw Kalonzo aliambia Rais Ruto.

Viongozi hao walishinikiza Wakenya wawe waangalifu wakidai serikali inaelekea katika mfumo wa uongozi wa kiimla.

Wote kwa moto mmoja waliradidi kauli zao za awali kuwa Rais William Ruto ameteka bunge na itakuwa rahisi kwao kupitisha sheria ambazo ni dhalimu kwa wananchi.

Raila hayuko nasi

Akimtakia kheri Kiongozi wa ODM Raila Odinga anapolenga kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika, Bw Jeremiah Kioni alisema wamejipanga kuwa na kiongozi mpya.

“Sisi ndio upinzani na sisi ni serikali ambayo inatarajiwa (2027). Kiongozi wa Azimio (Kalonzo Musyoka) yuko nasi hapa. Tumekuwa naye kila mahali na tutaendelea,” alisema.

Alirejelea kauli ya Raila Odinga kuwa alishauriwa na Mwenyekiti wa Azimio Uhuru Kenyatta ‘kumsaidia Ruto’ hadi baadhi ya viongozi wa ODM wakajumuishwa katika baraza la mawaziri.

“Uhuru alituonya dhidi ya serikali ya UDA. Hajatuelekeza kuungana na serikali ambayo imeundwa kinyume cha Katiba. Yeye (Uhuru Kenyatta) anasikitishwa kwa nini Wakenya wametelekezwa na serikali,” alisema.

Uongozi bungeni

Bw Kalonzo alitangaza kuwa baraza la usimamizi wa Azimio litakutana Jumatatu kuamua kiongozi mpya rasmi wa upinzani katika Bunge la Kitaifa.

Hii ni baada ya kiongozi wa wachache bungeni Opiyo Wandayi kuteuliwa na kuidhinishwa kuwa Waziri wa Kawi katika serikali.

Kiongozi wa Wiper alieleza kuwa walioteuliwa serikalini hawawezi kuwa katika mrengo wa upinzani.

NAIBU Rais Rigathi Gachagua amelaumu utekelezaji wa matimbo kwa visa vya fisi kuvamia na kuua wakazi wa Juja, Kaunti ya Kiambu.

Wakati uo huo, Bw Gachagua ametangaza serikali itasaka na kunasa fisi hao wanaohangaisha watu.

“Vifo hivi vinasikitisha. Tunatuma kikosi kukamata fisi na kuwahamisha fisi hao ili wasilete usumbufu. Matimbo yaliyotelekezwa yamekuwa sehemu zao za kujificha,” alisema katika sherehe ya harusi shuleni Juja Preparatory School Jumamosi.

Kadhalika, Naibu Rais alihofia kuwa matimbo hayo pia ni hatari kwa usalama na afya ya wakazi.

Alisema visa vya malaria vinaweza kuibuka kwa sababu yanaweza kuwaumbia makao mazuri ya kuzaa na kuongezeka.

“Matimbo haya yanaweza kusaidia fisi kujificha kabla ya kushambulia watu,” aliendelea. “Maafisa wa usalama watawafukuza wanyamapori na kuangazia visa vya mashambulizi.”

Bw Gachagua alikuwa anamjibu Mbunge wa Juja George Koimburi aliyetaka serikali iingilie kati kuokoa wakazi.

Haya yanajiri baada ya mwanamke mwenye umri wa miaka 52 kuuliwa na fisi mnamo Agosti 7, 2024.

Mashambulizi ya fisi

Baada ya mwanamke huyo kuuliwa na fisi, Shirika la Wanyamapori (KWS) lilizindua awamu ya pili ya ‘Oparesheni Ondoa Fisi Juja.’

Mnamo Januari 2024, KWS ilianzisha awamu ya kwanza ya ‘Oparesheni Ondoa Fisi Juja’ sambamba na kampeni dhidi ya kichaa cha mbwa.

Huu ni mpango unaohusisha wakazi wa Juja ili kumaliza mashambulizi ya fisi.

Oparesheni hiyo ilifaulu kuhamisha fisi 12 kutoka sehemu mbalimbali za Kaunti Ndogo ya Juja.

Maeneo hayo yanajumuisha Munyaka katika Wadi ya Theta, Mwireri eneo la Juja House, Athi, Kikumari Zone, Kimich na Mwalimu Farms.

Aghalabu fisi ni wanyama ambao hujishughulisha usiku lakini pia hushambulia mapema asubuhi.

Makundi ya fisi huzurura katika vijiji vya Nyacaba, Malaba, Athi, Juja Farm, Muthaara, Magomano, Mukuyu na vitongoji vingine maeneo ya Witeithie and Kalimoni.

Licha ya serikali kuanza mikakati ya kuangazia matatizo haya ya mashambulizi, visa hivi vingali vinashuhudiwa.

LONDON, Uingereza

KOCHA Pep Guardiola amesema kuwa vijana wake wa Manchester City walicheza kama mabingwa baada ya kubomoa Chelsea 2-0 katika mechi ya kwanza wanapofukuzia taji la tano mfululizo kwenye Ligi Kuu.

Ingawa amekiri ushindani mkali katika vita vya kuwania taji msimu huu wa 2024-2025 utatoka kwa Arsenal, Liverpool, Manchester United na Chelsea, Mhispania huyo alifichua kuwa hakutarajia kabisa City kunyamazisha vijana wa kocha Enzo Maresca ugani Stamford Bridge.

City walishinda mechi hiyo yao ya 16 ya kuanza msimu kati ya 28 kupitia mabao ya Erling Haaland na Mateo Kovacic.

Brighton, Arsenal, Liverpool, Aston Villa, Brentford, Manchester United na Newcastle pia walifungua msimu kwa ushindi.

Licha ya kuwa bila kiungo muhimu Rodri nao Phil Foden, John Stones, Kyle Walker na Nathan Ake walianza kutoka benchi, City walifuatiliza ushindi wa Kombe la Ngao kwa kunyamazisha Chelsea na kumpa Guardiola furaha tele.

“Sikutarajia kabisa. Najua vile vijana wangu wanaweza kufanya, lakini nashangaa katika siku ya kwanza na pia bila kufanya mazoezi.

Nakumbuka msimu jana hatukuweza kupata ushindi Stamford Bridge kwa hivyo ni dalili nzuri. Ni hatua kubwa tumepiga mbele. Ubaya tu ni kuwa bado michuano inasalia mingi, lakini kuanza msimu kwa kushinda kunatuongeza motisha,” akasema Guardiola.

Mhispania huyo alikiri kuwa wako juu kidogo ya wapinzani wengine kutokana na kuwa wamekuwa pamoja kwa misimu tisa kwa hivyo wanajuana vyema.

“Wote ni rafiki, familia zao pia ziko nao mara nyingi. Hiki ni kitu kinanifurahisha sana,” akasema Guardiola na kuwataka wachezaji wake waendelee kukaza kamba katika msimu unaoweza kuwa mrefu zaidi baada ya Klabu Bingwa Duniani kupanuliwa kutoka timu saba hadi 32 mwaka 2025.

Haaland sasa ana mabao 64 kutokana na kuchezea City mara 67 ligini.

City watakuwa wenyeji wa washiriki wapya Ipswich Town hapo Jumamosi.

Chelsea watavaana na Servette katika mkondo wa kwanza wa Europa League Conference ugani Stamford Bridge hapo Alhamisi kabla ya kurejelea majukumu ya ligi dhidi ya Wolves ugenini Jumapili.

All Rights Reserved © Cantona Group Ltd||2024


Discover more from cantonadigital

Subscribe to get the latest posts sent to your email.

Leave a comment